Thursday, December 17, 2009

GAVANA AONGEA KUHUSU MIKOPO BOT

Uongozi wa Benki Kuu (BoT), umetetea mikopo ya mamilioni ya watumishi wake kwa ajili ya ujenzi wa nyumba, ukisema mpango huo, unalenga kuwajengea maisha bora watumishi hao.

Kauli hiyo, inakuja kufuatia kuwepo kwa waraka wa baraza la mikopo la nyumba, ambalo limetaja viwango vya mikopo kwa madaraja tofauti katika matawi yake yote ya Mwanza, Dar es Salaam, Zanzibar, Arusha na Mbeya.

Waraka huo, unaonyesha kila mfanyakazi ataweza kukopa kati ya Sh 100milioni ikiwa ni kiwango cha juu na Sh 30 milioni kiwango cha chini kulingana na wadhifa wa mtumishi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba.

Akizungumzia waraka huo, Gavana wa BoT Profesa Benno Ndulu, alisema ni utaratibu ambao benki imejiwekea ili kuwawezesha wafanyakazi wake kimaisha.

Profesa Ndulu, alisema BoT, ilijiwekea utaratibu huo baada ya kuangalia mahitaji ya msingi ya makazi kwa watumishi wake.

"Ni utaratibu ambao upo kwa karibu miaka 20 sasa, lakini sasa tumeuboresha kwa kuangalia mahitaji ya mikopo kwa umakini," alifafanua Gavana Ndulu.

Profesa Ndulu ambaye amekuwa katika mchakato wa kuisafisha taasisi hiyo ya fedha, aliweka bayana kwamba mikopo hiyo, imekuwa ikitolewa kwa umakini ili kuhakikisha inarejeshwa.

Alisisitiza kabla benki hiyo, haijatoa mikopo, inatafuta taarifa za wahusika ili kubaini kama wana madeni ndani na nje ya benki hiyo.

No comments: