Wednesday, December 16, 2009

GTI Waendesha Mafunzo ya Ujenzi wa Vuguvugu la Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi Ngazi ya Jamii Katika Wilaya za Mbeya Vijijini.

Gender Training Insitute –GTI- wafanya mafunzo ya siku tatu juu ya Ujenzi wa Vuguvugu la Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi katika ngazi ya jamii katika vitongoji vya wilaya ya Mbeya vijijini. Mafunzo hayo ya siku tatu yalifanyika katika Manispaa ya jiji la Mbeya kuanzia tarehe 3-5 Novemba 2009 katika Ukumbi wa Mkapa Hall, na yalihudhuriwa na washiriki takribani mia moja kutoka katika vikundi zaidi ya 30 kutoka wilaya ya Mbeya vijijini. Mafunzo hayo yaliwezeshwa na dada Dina Nkya, Rehema Mwaiteba, na Anna Sangai.

Pamoja na malengo mengine mafunzo hayo yalikuwa na malengo yafuatayo: Kujenga Uelewa wa pamoja wa vuguvugu la Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi; Kujenga msingi wa uanzishwaji wa semina za GDSS katika ngazi ya jamii; Kueneza itikadi ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi; Kujenga uwezo kwa washiriki kufuatilia bajeti kwa mrengo wa kijinsia; Kuandaa mpango kazi wa pamoja; na Kuendendeleza vuguvugu la Ukombozi wa wanawake kimapinduzi.

Katika mafunzo hayo wawezeshaji walitumia mbinu mbalimbali ili kuweza kufikisha ujumbe kwa washiriki kwa urahisi zaidi, ambapo wawezeshaji waliweza kutumia mbinu za nyimbo, maigizo maafupi, visa mkasa, na michoro ambavyo viliandaliwa na washiriki wenyewe. Pia wawezeshaji walitumia mbinu shirikishi ambayo iliweza kuibua visa mkasa vingi kutoka kwa washiriki wenyewe. Mafunzo yalifundishwa ni pamoja na jenda na jinsia, Teknohama na ujenzi wa vuguvugu la maendeleo, itikadi za ukombozi wa wanawake, na ujenzi wa nguvu za pamoja katika harakati za ukombozi wa wanawake.

Mafunzo haya ni sehemu ya mpango wa GTI ya kuibua vuguvugu la Ukombozi wa wanawake kimapinduzi katika ngazi ya jamii, ambayo yanatarajiwa kufanyika kote nchi nzima hapo mwakani.

Habari zaidi, visa mkasa na picha za mafunzo haya zitaendelea kuchapishwa katika blog hii mapema.

No comments: