Thursday, December 3, 2009

TCRA kumbana mwekezaji Loliondo

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imebaini kuwa kampuni ya simu za mkononi yenye makao yake katika Umoja wa Nchi za Kiarabu (UAE), inaendesha shughuli zake za kutoa huduma ya mawasiliano ya simu bila leseni.

Kwa mujibu wa TCRA, kampuni hiyo inatoa huduma hiyo katika eneo la uwindaji liliopo Loliondo wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Profesa John Nkoma, amekataa kutaja jina la kampuni hiyo ya simu.

Kwa mujibu wa Profesa Nkoma, wataalamu wa TCRA wamebaini hilo baada ya kwenda kwenye eneo hilo kuchunguza.

Eneo hilo lipo chini ya kampuni ya uwindaji ya Otterlo Business Corporation Limited (OBC) inayodaiwa kumilikiwa na mwanajeshi wa cheo cha juu kutoka familia ya kifalme,UAE.

OBC ilipewa eneo hilo mwaka 1992 na tangu wakati huo imekuwa ikiongezewa muda kila baada ya miaka mitano.

Bunge limeiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kutoa upya vitalu vya uwindaji ifikapo mwaka 2011 kwa kufuata taratibu mpya.

Wananchi wa eneo hilo wamewahi kulalamika kuwa wanapoingia kwenye eneo hilo simu zao zinabadilika na kuonyesha wanaingia eneo la Uarabuni.

Kwa mujibu wa madai hayo, simu zinakuwa chini ya kampuni ya Etisalat na wanatozwa fedha nyingi wanapopiga simu.

Mkurugenzi Mtendaji wa OBS, Isaack Mollel, aliwahi kukaririwa akisema kuwa, eneo hilo lipo chini ya Etisalat kwa sababu familia ya kifalme ya UAE inahitaji mawasiliano ya uhakika inapotembelea eneo hilo.

Mollel alisema, kwa kuwa Etisalat ni mwanahisa mkuu katika kampuni ya Zantel, hakuna haja ya kuomba leseni TCRA.

No comments: