Wednesday, December 2, 2009

ATCL yapunguza wafanyakazi 155

KAMPUNI ya Ndege Tanzania (ATCL) imetoa barua za kuwapunguza kazi wafanyakazi wake takribani 155 kati ya 333.

Inadaiwa kuwa uamuzi huo una lengo la kuiwezesha kampuni hiyo kutekeleza majukumu ya uendeshaji yaliyokuwa yameshindikana kutokana na kuzidiwa na idadi kubwa ya wafanyakazi.

Chama cha Wafanyakazi wa Mawasiliano na Uchukuzi (COTWU), kimeridhia vigezo vya awali vya serikali na kuachana na azma yao ya awali ya kumtaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda aingilie kati suala hilo.

Hatua nyingine ni ya serikali kuingia ubia na Kampuni ya China iitwayo China Sonangol International Ltd (CSIL) ambayo mbia huyo ameshaonesha nia.

Awali, COTWU ilisema imegomea hatua ya serikali ya kutaka kuwalipa wafanyakazi kwa kigezo cha nusu mshahara (mshahara wa wiki mbili) unatakaozidishwa katika miaka ya utumishi wa mfanyakazi isiyozidi 10.

Wafanyakazi wanataka pamoja na stahili nyingine, anayepunguzwa alipwe mshahara wa miezi miwili utakaozidishwa katika miaka isiyopungua 10 ya kazi.

Jana, gazeti hili lilifika Makao Makuu ya ATCL Dar es Salaam jana na kukuta wafanyakazi wakipishana huku na huko wengine wakiingia katika chumba cha wahasibu kulikoelezwa kutolewa barua na hundi.

“Yaani hapa leo hakukaliki kwa kweli viongozi wote karibu hawapo ofisini, walioko ni wale wanaotekeleza hatua hii ya kutoa barua, hivyo shughuli za kiofisi pengine kesho,” alisikika mmoja wa wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Mfanyakazi ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini alisema,imemlazimu kupokea barua na fedha iliyopo kwa matakwa ya serikali na kubainisha kuwa COTWU walikubaliana na serikali kwa sababu hata hicho kidogo kama wakiendelea kukikataa,watakikosa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Miundombinu, Omari Chambo na Kaimu Ofisa Mkuu wa ATCL, William Hajji, kwa nyakati tofauti walithibitisha kuendelea kwa hatua hiyo.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Balozi Mustafa Nyang’anyi, amesema, malipo (bila kubainisha kiasi) yanafanywa na Shirika la Kusimamia Mali za Mashirika ya Serikali yanayouzwa au kubinafsishwa (CHC).

No comments: