Friday, February 13, 2009

Wabunge kujadili nyaraka za Mkapa


SERIKALI imebanwa na Bunge, kiasi cha kulazimika kuanza kufikiria uamuzi wa kisheria na hata kutafakari fursa ya kumwondolea kinga Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, au kutafuta uwezekano wa kumhoji kuhusu mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira mkoani Mbeya, anaodaiwa kuwa mmoja wa wamiliki, kupitia kampuni ya ANBEN.

Mbinyo huo wa Bunge dhidi ya Serikali unatokana na kile kinachoelezwa kuwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kunasa nyaraka zinazobainisha kuwa Rais Mstaafu Mkapa ni mmoja wa wamiliki wa mgodi wa Kiwira, nyaraka ambazo baadaye zilifanyiwa mabadiliko ili kumwondoa Mkapa katika wingu hilo.

Nyaraka hizo ambazo Raia Mwema imefanikiwa kuziona zinabainisha kuwa Mkapa pamoja na mkewe Anna ni wamiliki wa hisa katika mgodi wa Kiwira kupitia kampuni yao ya ANBEN. Hata hivyo, kutokana na mwenendo wa mambo na hasa baada ya suala hilo kuonekana kumweka pabaya kisiasa na kisheria Mkapa, umiliki wa mgodi huo ulifanyiwa mabadiliko.

Katika mabadiliko hayo, nyaraka za sasa zinabainisha kuwa mgodi huo unamilikiwa na kampuni ya Tanpower Resources Ltd, ambayo ni muungano wa kampuni nne tofauti.

Kampuni hizo ni Fosnick Ltd, ambayo wanahisa wake ni Nick Mkapa, Foster Mkapa na mwingine aliyetambuliwa kama B. Mahembe, kampuni nyingine ndani ya mwavuli wa Tanpower Resources ni Choice Industries ambayo wanahisa wake ni Joe Mbuna na Goodyear Francis, nyingine ni Devconsult Ltd yenye wanahisa D. Yona na Dan Yona jr, wakati kampuni ya nne ni Universal Technologies Ltd ambayo wanahisa wake ni Wilfred Malekia na Evans Mapundi.

Raia Mwema imedokezwa kuwa tayari nyaraka za awali (original) zenye kuonyesha kuwa mgodi wa Kiwira unamilikiwa na kampuni ya ANBEN ambayo ni ya Mkapa, zimefikishwa katika uongozi wa juu wa Bunge.

Kwa mujibu wa habari za uhakika zilizotufikia inaelezwa kuwa nyaraka hizo zimejitosheleza kiushahidi kwamba Mkapa ni mmiliki wa ANBEN kampuni ambayo inahusika katika umiliki wa mgodi wa Kiwira.

Kutokana na hali hiyo na hasa kile kinachobainika kuwa Bunge kupitia Kamati yake ya Nishati na Madini kuridhishwa na ushahidi katika nyaraka hizo, muhimili huo wa Taifa umedhamiria kuibinya Serikali katika mambo makuu mawili.

Jambo la kwanza ni kushinikiza mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira kurejeshwa serikalini kutokana na sababu kadhaa lakini kubwa zaidi ni wawekezaji wanaopaswa kuendesha mgodi huo kubainika kuwa ni wababaishaji walioshindwa kutekeleza ahadi zao kwa Serikali.

Source:Raia Mwema, Februari 11, 2009

No comments: