Wednesday, February 11, 2009

Msamaha wa madeni wanunulia ‘mashangingi’

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), imesema imetumia fedha za msamaha wa madeni na kuamua kununua magari ya kifahari 80 kwa ajili ya viongozi. Akitoa ufafanuzi leo kuhusu ununuzi wa magari hayo ya kifahari ambao umelalamikiwa na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa na wananchi kwa ujumla, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma, alisema fedha hizo hazitokani na kodi ya wananchi.

"Tumenunua magari ya 'mashangingi' aina ya Toyota Prado, jumla yake 80 kutokana na msamaha wa madeni kutoka taasisi za fedha za kimataifa ... hapo tuliamua ni bora kuagiza magari kwa ajili ya matumizi ya viongozi," alisema Hamza. Alisema magari hayo mara baada ya kuwasili nchini yaligawiwa kwa viongozi wa ngazi za juu wakiwamo mawaziri, naibu mawaziri na wakuu wa mikoa Unguja na Pemba.

Hamza alisema si busara kwa mawaziri na watendaji wakuu wa serikali kusumbuka kutokana na tatizo la usafiri ambalo lilikuwa kubwa. Aidha, alisema mbali ya kununua magari hayo, SMZ ilitumia fedha hizo kununua matrekta 12 kwa ajili ya kazi za kilimo Unguja na Pemba.

"Hatukununua mashangingi tu, pia tulinunua matrekta 12 kwa ajili ya kuimarisha sekta ya kilimo kwa wakulima wetu katika kuondokana na ukosefu wa chakula," alisema. Hamza alilazimika kutoa ufafanuzi huo kutokana na malalamiko kutoka kwa baadhi ya wanasiasa na wananchi kuhusu serikali kununua magari ya kifahari yenye kugharimu fedha nyingi, huku wananchi wakikabiliwa na matatizo mengi.

Daily News; Tuesday,February 10, 2009 @20:28

1 comment:

Anonymous said...

Governments role is peoples' welfare and security: what is the right ratio balance between Zanzibar leaders and peoples' welfare? can one enjoy in Mashangingi while majority are swiming in Chai Maharage transport or footing indeterminate distances! It is not belivable!!!