Friday, May 9, 2014

Wananchi wameachwa, hawasikilizwi wamechukua hatua!






Kwa muda mrefu mjadala unaohusu mchakato wa kaundikwa upya kwa katiba mpya umekuwa ukisikika zaidi kupitia kwa watu au makundi yenye majina makubwa kama wanasiasa na wasomi na wale wenye nafasiki ya kuvifikia vyombo vya habari,  lakini jamii ya chini   au makundi ya pembezoni yametawaliwa na ukimya wa ajabu kana kwamba hawana la kusema.

Ukifuatilia vijijini na katika maneo mengine ya kukusanyika wananchi utaona jinsi wanavyoshiriki kutoa sauti zao kwa namna wanavyofuatilia mchakato unaoendelea. Vijiweni, masokoni, vilabuni nako kuna mijadala ya katiba mpya nao wanapokusanyika wanajadili kuwa ni masuala gani wanayataka au wangependa kuona yameingizwa kwenye katiba mpya. Lakini je matokeo ya mjadala ngazi ya jamii ni nini? Je sauti zao zinasikika kwa mamlaka za juu?


Suala la nani anafanya nini  au anasema nini na kwa manufaa ya nani kwenye Bunge la katiba  au mijadala mikubwa kwenye makongamano na matamasha ambayo wanajamii wa ngazi ya kijiji au kitongoji hawaalikwi yanasikika huko ngazi ya chini kabisa. Wananchi hao hao wanafuatilia kupitia redio na magazeti, na tujue kuwa siku hizi watu wengi wanamiliki simu za tochi ambazo zina redio. Wanachokisikia wanajadiliana jinsi wanavyoweza kuhakikisha sauti zao zinasikika au ziwafikie viongozi.

Kutokana na kukosekana kwa jukwaa la kisheria au mijada inayotakiwa kuongozwa kisheria na serikali zetu hasa kwenye ngazi za vijiji na kata, wanajamii sasa wameanzisha kitu kinachoitwa sauti ya jamii (jamii Voice) hii ipo katika kata za Kisarawe (Pwani) Mkambarani (Morogoro Vijijini), Songwa (Kishapu), Songea mjini, na kata ya Mwananyamala (Kinondoni), wananchi wameanzisha mitandao ya vikundi vidogo vidogo, na kuunda mtandao mkubwa unaokusanya sauti za wengi na kuzisambaza.

Mitandao hii kwa ngazi walio nayo ya kata wanashirikiana na  wanajamii kupaaza sauti zao kwa nguvu kuwasiliana na  Wajumbe wa Bunge maalum la Katiba moja kwa moja bila kuandika barua au kuwafuata huko Dodoma, wanawaeleza wanataka kitu gani kifanyike na waseme nini kwenye mchakato wa Katiba mpya.

Wakati wa uendeshaji wa mabaraza ya katiba uliofanyika katikati ya mwaka 2013 wanajamii hawa walitumia mfumo huu wa kupeana taarifa kupashana habari juu ya ushiriki wao kwenye mabaraza ya katiba na kinachoendelea, baadaye walijiunga na kuandaa mabaraza ya katiba ya asasi ambayo nayo walitumia sms kupashana habari na kupata maoni ya wengi.

 Nilibahatika kukutana na baadhi ya wananchi wanaoshiriki kwenye mpango huu wa kupaaza sauti za jamii, mmoja wao ni Janeth Mawinza kutoka Mwananyamala ambaye anasema kuwa wao wanamtambo mdogo wa kurusha ujumbe mfupi wa simu (SMS) kwenda kwa watu zaidi ya 1000 kwa mara moja. Wanafuatilia mjadala wa Bunge la Katiba na kuandika ujumbe mfupi  ambao wanaurusha kwenda kwenye simu za wajumbe wa Bunge maalum la Katiba kwa wakati mmoja wakidai wanataka mjadala wa namna gani na wanataka nini kwenye mchakato.


“Mpango huu unasaidia sasa kuweka msukumo na kuonesha kuwa sisi wananchi wa ngazi ya mtaa huku chini tunafuatilia kile wawakilishi wetu wanachokijadili kwenye Bunge la katiba, tunasema na tunawaeleza mmoja mmoja anasoma ile meseji kwenye simu yake kama anampango wa kupoteza muda au kufifisha masuala ya wananchi masikini kwenye Katiba anaacha..”anasema Janeth.

Mara nyingi wananchi wamekuwa wakilalamika kuwa mchakato umewatenga haswa kutokana na  wajumbe wa Bunge kugawanyika kimakundi na kiitikadi ndani ya Bunge hilo na kuwaacha wananchi bila kiongozi wao.

Janath anasema kuwa  wametambua kuwa wanawake wengi wanamiliki siku lakini hawana uwezo wa kutazama TV au kusikiliza redio, wanatumia njia hiyo kuwafikia wanawake wakiwa jikoni wakipika na badaye wanachukua hatua. “mfano ukituma ujumbe kuwa kesho tuna mkutano wa kuhamasisha kuhusu jambo fulani, wataikia wengi kuliko tungetangaza kwenye chombo cha habari..”anasema.

Huko Kisarawe wananchi  wa kituo cha taarifa na maarifa kutoka vijiji vya Kisarawe mjini na  Visegese,  wanatumia njia hii ya ujumbe mfupi kuhamasishana juu ya kampeni yao ya utunzaji misitu na mapambano dhidi ya Ukatili wa Kijinsia kwa jamii na upatikanaji wa huduma za msingi kama maji, afya, elimu na miundombinu kwa jamii hasa wanawake.
Wanatumia mfamo huu wa upashanaji habari kusambaza meseji kwa wanavijiji zaidi ya 5000 kwa mara moja, pamoja na viongozi wa kijamii na wanaona mwitikio wa jamii kutokana na ujumbe unaotumwa. Wakiwa mjini wanafikia wananchi walio katika vijiji ambavyo magari hayafiki.

“hapa Kisarawe mfumo huu umetusaidia kwa kiasi kikubwa kupashana habari, kwanza tunawatumia viongozi wetu ujumbe kwa njia ya sms, tukiwakumbusha kutimiza ahadi zao huko vijijini, baadaye tunafuatilia utekelezaji. Tumekuwa na kampeni yetu ya kupinga ukatili wa kijinsia kwenye vijiji nyetu ambavyo vingine havififikiki kiurahisi, tunatuma ujumbe” anasema  Simon Mpunga mratibu wa IGN Kisarawe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kituo cha Taarifa na Maarifa na Maarifa.

Aidha wametumia njia hiyo kuhamasisha viongozi wa vijiji kuwachukulia hatua watu wanaowazuia watoto wa kike kupata elimu kwa kuwapa mimba. Katika mfumo huu ambao pia wameshiriki kuwahamasisha wananchi kufuatilia  mjadala wa Bunge la katiba wakati linaanza mjini Dodoma, wakati rasimu ya Pili ya Katiba ilipotoka walihamasisha wananchi wote wa Kisarawe kujitahidi kufuatilia na kupata rasimu ya pili ya Katiba mpya ili wajue ni masuala gani ya wananchi yameingizwa humo na kuyatetea ili yasiondolewe na wajumbe wa Bunge maalum  la Katiba.

Tuna kila sababu ya kupongeza mpango huu wa wananchi kusimama na kudai mabadiliko wao wenyewe. Kuchukua hatua ni jambo la msingi kuliko kusubiri kusemewa na watu ambao wakati mwingine wanaongozwa na itikadi za kisiasa au maslahi binafsi.
Tumeona matokeo ya kuwa na Bunge la katiba lenye zaidi ya watu 600 tena wanaotokana na Bunge la kawaida ambalo limezoea kujiendesha kisiasa. Lakini wananchi wanapoona wameachwa na sauti zao hazisikiki wanaamua kuchukua hatua ya kupaaza sauti zao wenyewe.

 Wajumbe hawa wa Bunge la katiba wanaamua kutumia muda na rasilimali za wananchi kutetea vyeo na nafasi zao za uongozi siziondolewe kupitia katiba mpya. Lakini hali ilivyo sasa wananchi wameamka na wanajua haki zao wanadai mabadiliko yanayoonekana. 

No comments: