Tuesday, August 28, 2012

Watu 73 kizimbani vita ya ardhi Dar

Watu 73 wamefikishwa mahakamani kwa kosa la kuwashambulia, kuwazuia polisi kufanya kazi yao, kuvamia maeneo ya watu na makosa mengine kufuatia operesheni ya kuwaondoa wananchi waliovamia maeneo yanayomilikiwa na wengine iliyoendeshwa na manispaa ya Kinondoni, huko Nakasangwe, Kata ya Wazo wilayani Kinondoni.

Aidha watu wengine 50 wanashikiliwa na polisi kufuatia operesheni hiyo, kwa ajili ya mahojiano zaidi wakituhumiwa kutokuwa na uraia wa Tanzania.

Kamanda wa Polisi wa Kinondoni, Charles Kenyela, aliiambia NIPASHE jana iliyotaka kufahamu maendeleo ya operesheni hiyo, ambayo mwishoni mwa wiki ililikumba pia eneo la Benaco lililoko katika kata ya Wazo jijini Dar es Salaam.

“Kwa hawa 50, kuna timu maalumu iliyoundwa kwa ajili ya kuwafanyia mahojiano zaidi kutokana na kuwepo kwa taarifa kuwa huenda si Watanzania, bali raia kutoka nchi jirani, na kwa hali hiyo, timu inayofanya kazi hii ya kuwahoji, inawajumuisha pia maofisa uhamiaji ambao ndiyo haswa wenye eneo lao,” alisema.

Kamanda Kenyela alisema kimsingi watu hao walikamatwa katika eneo walilolibatiza kwa jina la ‘Mungiki no go area’ lililoko kitongoji cha Kaza Raha huko Nakasangwe ambacho kilikuwa hakifikiwi na mtumishi yeyote wa serikali, mfanya biashara au mwananchi asiyefahamika nao kwa kuwa walikuwa wakiwakamata, kuwapiga na wengine kuwabaka.

Alisema kuwa kitendo cha watu hao kuwarushia mishale, mashoka na mapanga polisi kama ilivyotokea siku ya kwanza ya operesheni si tabia ya Watanzania na kwamba, miogoni mwa watu waliofanya kitendo hicho ni hao 53 wanaoshikiliwa.

Aliwaasa wananchi wote waliovamia maeneo katika Manispaa ya Kinondoni kuondoka kwa amani kwa kuwa, polisi wapo kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa sheria.

No comments: