Tuesday, May 22, 2012

Umbali wazuia wanafunzi kuripoti shuleni

WANAFUNZI 200 wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari ya Ulyankulu wilayani hapa mkoani Tabora, hawajaripoti shuleni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo hofu ya kutembea umbali mrefu kwenda shuleni hapo.

Akizungumza na waandishi wa habari wilayani hapa, Mkuu wa Shule Msaidizi, Alphonce Makaza alisema kuwa mwaka huu walitegemea kuwa na wanafunzi 602 wa kidato cha kwanza na kwamba walioripoti hadi sasa ni wanafunzi 400.

Alisema umbali uliopo kati ya shule na makazi ya watu, unawakatisha tamaa baadhi ya wanafunzi hususani wa kike ambao wanapolazimika kutembelea umbali mrefu wanaweza kukutana na watu wenye tabia ya unyanyasaji wa kijinsia.

Mwalimu Makaza alitaja sababu nyingine za wanafunzi kutoripoti shuleni kuwa ni mtazamo wa jamii kuhusu watoto wa kike kuwa hawana umuhimu wa kusoma kama ilivyo kwa watoto wa kiume.

Aidha alibainisha kuwa mfumo wa maisha katika ngazi ya familia unawanyima watoto hao fursa ya kushiriki kikamilifu katika masuala ya elimu na kwamba wanatumika zaidi katika shughuli za kilimo na uzalishaji mali.

Mkuu huyo wa shule msaidizi alisema pamoja na kwamba shule hiyo ina bweni la wanafunzi wa kike lenye uwezo wa wanafunzi 80, lakini waliopo kwa sasa ni 46.

Mwalimu wa nidhamu shuleni hapo, Bahati Msengi alisema kuwa wanafunzi wengi wanaishi kwenye nyumba za kupanga jambo ambalo linahatarisha usalama wa wanafunzi wa kike.

No comments: