Monday, May 14, 2012

BoT- Nchi ina ‘dola’ za kutosha

BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imesema hazina ya Taifa inazo fedha za kigeni za kutosha za kuendesha nchi kwa miezi minne ijayo.

Aidha, imehadharisha kwamba taarifa zozote zisizo na ukweli zinazotolewa kuhusu hali ya fedha za kigeni ya nchi, zinaweza kuleta matatizo makubwa ya kiuchumi.

Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndulu alisema jana kwamba hazina ya taifa ina akiba ya Dola za Marekani bilioni 3.6 inayotosheleza mahitaji ya kuendesha nchi kwa miezi minne ijayo.

“Akiba ya fedha za kigeni hivi sasa ni Dola za Marekani bilioni 3.6, hizi zinatosheleza kuendesha nchi kwa miezi minne ijayo.

Tumewahi kulisema hili, tumezungumzia haya katika Kamati ya Bunge na hata taarifa hizi zipo IMF (Shirika la Fedha la Kimataifa),” alisema Profesa Ndulu alipozungumza na gazeti hili kwa simu.

Profesa Ndulu alisema kiasi hicho cha hazina ya taifa kinakidhi vigezo vya IMF ambavyo vinataka akiba hiyo itosheleze mahitaji ya nchi husika siyo chini ya miezi mitatu. Aliongeza kuwa hata pamoja na ukweli kwamba thamani ya Euro imeshuka duniani, lakini hali hiyo haijaathiri hazina hiyo ya Taifa, na kwamba uingizaji wa bidhaa ndani ya nchi umeongezeka.

Gavana huyo alitoa ufafanuzi huo baada ya gazeti hili kutaka kujua ukweli wa hazina ya taifa na hasa kutokana na taarifa ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema), akihoji ukimya wa BoT katika masuala mbalimbali ikiwamo hazina hiyo na taarifa zinazohusu uchumi hasa suala la mfumuko wa bei.

“Kuna tetesi kwamba Hazina ya Taifa (Hifadhi ya Fedha za kigeni – foreign reserve) inakauka, kwamba tuna hifadhi ya kuagiza bidhaa nje kwa mwezi mmoja tu. Niliposikia tetesi hizi sikuamini. Nilipoenda katika tovuti ya Benki Kuu ili kupata habari rasmi (authoritative) nimekuta takwimu za Novemba 2011,” alieleza Zitto katika taarifa hiyo aliyoituma kwa vyombo vya habari. Hata hivyo jana jioni BoT iliongeza taarifa za Januari mwaka huu.

“Takwimu ya Mfumuko wa Bei iliyoko kwenye tovuti ya Benki Kuu ya Tanzania ni ya Novemba mwaka 2011! Ukitaka kujua mwenendo wa Bajeti ya Serikali kama makusanyo ya Kodi na Matumizi utapata Taarifa ya Novemba mwaka 2011.

“Ukitaka kujua manunuzi ya Mafuta (fuel imports) kwa miezi 3 ya mwanzo ya mwaka 2012 ili kuweza kuona namna Umeme wa dharura umeathiri urari wetu wa Biashara ya Nje hupati taarifa hiyo katika tovuti ya Benki Kuu.Taarifa zinafichwa,” alidai Zitto na kumshauri Profesa Ndulu.

“Prof. Ndulu hakikisha Taarifa ya Mapitio ya Uchumi wa kila Mwezi imewekwa kwenye tovuti kwa muda mwafaka. Ifikapo mwisho wa Wiki inayoanzia Jumatatu Mei 14, tovuti ya Benki Kuu iwe na Taarifa za miezi yote (Desemba, Januari, Februari, Machi na Aprili). Taarifa hizi ni muhimu ili nasi tutekeleze majukumu yetu ya Kikatiba kama Wabunge, Mawaziri vivuli na Wananchi wa Tanzania.”

Hata hivyo, katika ufafanuzi wake Profesa Ndulu alisema wamebadilisha mfumo wa utoaji wa taarifa kila mwezi na sasa wanatoa kila baada ya miezi miwili na kwamba Kamati maalumu ilikutana Februari mwaka huu na taarifa zake zilitarajiwa kuwekwa katika tovuti ya benki hiyo jana.

“Tumebadilisha mfumo wa Kamati ya Sera ya Fedha ambayo sasa inakutana kila baada ya miezi miwili…mara ya mwisho ilikutana Februari na leo (jana) taarifa zao zitakuwa katika website (tovuti). Kulikuwa na matatizo ya kiufundi, lakini taarifa hizo zitakuwapo pamoja na taarifa rasmi kuhusu hazina ya taifa,” alisema Gavana.

Lakini Profesa Ndulu alionya kuwa si vyema kutoa taarifa zisizo sahihi zinazoweza kusababisha matatizo ya kiuchumi, ikiwamo soko la kubadilisha fedha kwenda ovyo na hivyo thamani ya Shilingi kuporomoka ghafla.

No comments: