Thursday, May 3, 2012

TGNP Yawapiga Msasa Waandishi wa Habari


Na Deogratius Temba
WAANDISHI wa habari wameaswa kubeba sauti za wananchi walioko pembezoni katika  kudai haki zao hasa wakati wa  mchakato wa kukusanya maoni ya wananchi kwaajili ya kuandaa katiba mpya.
Akizungumza Kaimu Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya Jinsia kilichoko chini ya Mtandao wa  Jinsia Tanzania (TGNP) Dorothy Mbilinyi, amesema watanzanzia masikini walioko pembezoni wanategemea kupata taarifa na kutoa taarifa kupitia vyombo mbalimbali vya habari.

“ Wananchi wameamka  wameanza kujieleza  vyombo vya habari vinatakiwa kufanya kazi yake kuwa sauti ya wanyonge, viwe mdomo kwa makundi yaliyowekwa pembezoni, ili kuibua changamoto zilizojificha na kuyafanya makundi haya kuwa na haki sawa na wengine,” amesema Mbilinyi.

Mbilinyi amesema kuwa vyombo vya habari vya Tanzania vimefanya kazi kubwa ya kuibua kero  za wananchi na ufisadi, ikiwepo kudai uwajibikaji katika misingi ya demokrasia na haki za biandamu.
Aidha amewataka waandishi wa habari kufanya  kazi kwa bidii mwaka huu kwasababu ni mwaka wenye changamoto nyingi ambazo zitahitaji  weledi, uadilifu, ukweli na uwazi.” Huu nini mwaka wa kukusanya maoni ya katiba, mwaka wa kudai uwajibikaji kwa viongozi wasio waadilifu, na ni mwaka wa Sensa ya idadi ya watu…” amesema Mbilinyi.

Akieleza malengo ya mafunzo hayo ya siku tatu yaliyoanza mei 3 hadi 5, Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na habari, Lilian Liundi amesema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia waandishi wa habari kujitadhimini upya jinsi ambavyo wanaandika habari za kijinsia.
Pamoja na kujitadhimini waandishi wa habari watajifunza juu ya hali ya sasa ya  ujenzi wa vuguvugu la ukombozi wa wanawake kimapinduzi, kampeni ya haki uchumi,  mfumo dume na mfumo uleberali mambo leo.

Pia watajifunza namna ya kuandika habari za kijinsia na kuchambua maoni yanayotolewa na wananchi juu ya katiba mpya, kufanya  habari za kiuchunguzi vijijini na kuibua changamoto za wananchi.
Mafunzo haya yanafanyika ikiwa ni siku chache baada ya TGNP kukutana na wahariri wa vyombo vya habari jijini Dar es alaam wiki iliyopita.

No comments: