Wednesday, January 19, 2011

Tume Utawala Bora kutoa tamko vurugu Arusha

KAMISHNA mpya wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Ali Hassan Rajab ameahidi kutoa tamko kuhusu vurugu zilizojitokeza jijini Arusha kati ya polisi na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ili kufafanua kama kulikuwa na uvunjifu wa haki za binadamu na utawala bora.

Kamishna huyo aliyasema hayo jana Ikulu Dar es Salaam mara baada ya kuapishwa na Rais Jakaya Kikwete, yeye pamoja na Katibu wake Mtendaji, Mary Massay.

Alisema, anafahamu kuwa suala hilo limeanza kushughulikiwa na wenzake walioko kwenye Tume hiyo kuahidi kuhakikisha mambo yaliyosababisha vurugu hizo yanafuatiliwa.

“Wananchi wasiwe na wasiwasi, ingawa naamini wenzangu tayari wameanza kulifanyia kazi suala hili, tutafuatilia na kuchukua hatua iwapo itabainika kulikuwa na uvunjifu wa haki za binadamu na utawala bora,” alisema Rajab.

Massay alisema kazi yake ya kwanza itakuwa kuhakikisha Tume hiyo inafanya majukumu yake kwa mujibu wa Katiba, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha Serikali inawezesha Tume katika upande wa rasilimali watu na vitendea kazi.

“Pia kazi kubwa itakuwa ni elimu kwa umma ili wananchi watambue haki zao pamoja na kufuatilia matukio ya uvunjifu wa haki za binadamu na utawala bora,” alisema.

Aliwataka wale wote wanaokiuka haki za binadamu kuwa macho kwani Tume hiyo kamwe haitowavumilia lakini pia aliahidi kushughulikia malalamiko yaliyowasilishwa katika Tume hiyo na kuhakikisha haki inatendeka.

Hivi karibuni mkoani Arusha wakati Chadema ikifanya maandamano yaliyozuiliwa na Polisi, vurugu ziliibuka baina ya wafuasi wa chama hicho na polisi ambapo watu watatu waliuawa baada ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa kuagiza wafuasi hao kuvamia kituo cha Polisi kuwatoa watuhumiwa.

No comments: