Thursday, January 27, 2011

Hukumu ya kesi ya EPA kutolewa Aprili 29, 2011

HUKUMU ya kesi ya katika kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), inayomkabili aliyekuwa Mweka Hazina wa CCM Mkoa wa Kigoma Rajabu Maranda na binamu yake Farijala Hussein itatolewa hukumu Aprili 29, mwaka huu.

Mbele ya jopo la mahakimu Sauli Kinemela, Ilvin Mgetta na Focus Bampikya wa Mahakama ya Hakimu mkazi Kisutu, Wakili wa washitakiwa hao Majura Magafu alidai kuwa kesi hiyo imefikia ukomo wake jana ambapo Mahakama imesikiliza ushahidi wa pande zote mbili na kwamba wanaiachia Mahakama ifanye kazi yake.

Wakili Mkuu wa Serikali Boniface Stanslaus alidai anaungana na upande wa utetezi kwamba upande wa mashitaka hauna la kuongeza na wanaiachia Mahakama iamue lini itatoa hukumu dhidi ya shauri hilo.

Katika kesi hiyo upande wa mashitaka uliwasilisha mashahidi tisa na vielelezo 17 ambapo washitakiwa hao pia walijitetea wenyewe.

Kwa mujibu wa kesi hiyo, Maranda na Farijala wanadaiwa kuwa kati ya Aprili Mosi na Septemba 2, mwaka 2005 katika Mkoa wa Dar es Salaam, waliiba kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Sh 1,864,949,294.45 baada ya kudanganya kuwa kampuni yao ya Kiloloma & Brothers ililipwa deni na kampuni ya BC Cars Export ya Mumbai nchini India.

Maranda anakabiliwa na kesi nne za aina hiyo katika Mahakama hiyo wakati Farijala anakabiliwa na kesi tatu za aina hiyo mahakamani hapo na wote wapo nje kwa dhamana.

No comments: