Thursday, January 27, 2011

Zisikumbatiwe NGOs zisizowajali wanawake, Tanzania yaiasa UN

TANZANIA imeutaka Umoja wa Mataifa (UN) kutozikumbatia taasisi zisizo za kiserikali (NGOs) zinazojinufaisha kupitia matatizo ya wanawake.

Balozi wa Tanzania UN, Ombeni Sefue alisema hayo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kwanza wa Bodi ya chombo kipya cha UN, kinachoshughulikia masuala ya wanawake, UN-Women.

Balozi Sefue alisema wakati Tanzania ikiunga mkono na kukaribisha ushirikiano wa wadau mbalimbali zikiwamo NGOs katika kuchagiza maendeleo na haki za wanawake, tahadhari ichukuliwe dhidi ya wale wanaotaka kujinufaisha kupitia matatizo hayo.

“Tunakaribisha wazo hili la kushirikiana na wadau mbalimbali zikiwamo NGOs, na hasa waliodhamiria kuonesha kwa vitendo nia hiyo na si wale wanaolenga kujinufaisha,” akasisitiza Balozi.

Aidha Mwakilishi huyo wa Tanzania, ambayo ni kati ya nchi za kwanza kuunda Bodi ya UN-Women, amekitaka chombo hicho kukidhi kiu na matarajio ya nchi wanachama na hasa wanawake.

Alisema licha ya watendaji wa chombo kuwa na ubunifu na wanaojituma, lakini pia wanapaswa kujielimisha kuhusu mazingira watakayofanyia kazi.

Alisema kila nchi ina changamoto zake linapokuja suala la kushughulikia haki, usawa na maendeleo ya wanawake zikiwemo za mila, desturi na tamaduni hivyo ni vyema watendaji wa chombo hicho wakafahamu kuyazingatia hayo.

Balozi Sefue amesema ni vyema chombo hicho katika utekelezaji wa majukumu yake na hasa kwa kuzingatia kwamba kitalenga zaidi kufanya kazi ndani ya kila nchi husika, kizingatie mipango ya kila nchi na vipaumbele ambavyo nchi hizo imevichagua.

Pia alielezea hatua mbalimbali za kisera, kisheria na kimipango ambazo zimefanywa na Serikali ya Tanzania katika kutatua kero za wanawake.

Alisema Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete ameonesha utashi mkubwa wa kisiasa katika kushughulikia haki za wanawake ambao upo pia kwa viongozi wengine wa Serikali.

No comments: