Monday, January 24, 2011

Sumaye atetea mawaziri kupingana

WAZIRI Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye, ametetea hoja ya mawaziri kuzungumza na kupingana hadharani kama jambo linalozungumziwa halikujadiliwa ndani ya Baraza la Mawaziri.

Sumaye alisema hayo jana Dar es Salaam katika mahojiano na waandishi wa habari baada ya kumalizika kwa sherehe za kuukaribisha mwaka mpya za Chama cha Maendeleo ya Wilaya za Mbulu, Hanang, Babati na Karatu.

Alisema yapo mambo ya pamoja ya Serikali, lakini pia kila mtu ana uhuru na utashi wa kuzungumza analoona linafaa.

“Tatizo ni kwamba suala la Dowans (kampuni inayotarajiwa kulipwa Sh bilioni 94 baada ya Serikali kuvunja mkataba wake wa kufua umeme) halikwenda katika Baraza la Mawaziri ambako mtu angetoa dukuduku lake kule, kila mtu ana utashi, si kwamba ukiwa Waziri ndio usizungumze,” alisema Sumaye.

Hivi karibuni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utawala Bora, Mathias Chikawe, alisema ni kosa kwa mawaziri kupingana hadharani na kuongeza kuwa kama kuna mwenye dukuduku kuna namna ya kuwasilisha maoni yao.

Kwa mujibu wa Chikawe, taratibu hizo ni kwa mawaziri husika kuwasiliana na kushauriana na inapotokea anayeshauriwa haelewi, upo utaratibu wa kupeleka maoni hayo kwa Waziri Mkuu.

Waziri huyo alitoa kauli hiyo, kufafanua kauli ya Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe kupingana na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.

Mawaziri hao walipingana na tamko la Ngeleja kwamba Serikali itailipa Dowans deni lake na waziri huyo alifanya hivyo baada ya kushauriwa na Mwanasheria Mkuu, Jaji Frederick Werema.

Katika hatua nyingine, Sumaye pia aliunga mkono kauli ya Rais Jakaya Kikwete ya kuunda tume ya kukusanya maoni kuhusu Katiba Mpya.

Lakini pia aliunga mkono hoja ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema), ya kupeleka hoja hiyo bungeni ili ijadiliwe na kuongeza kuwa hata yeye angekuwa mbunge, angepeleka hoja hiyo bungeni.

Alifafanua kuwa wakati hoja hiyo ikijadiliwa na wakati wananchi wakipewa elimu kuhusu uzuri na upungufu wa Katiba iliyopo, hali hiyo itatoa fursa kwa wananchi kufanya uamuzi wa kuwepo kwa Katiba mpya au la na maundhui ya katiba hiyo.

No comments: