Tuesday, January 25, 2011

KESI YA JERRY MURO ILIVYOUNGURUMA JANA

MHASIBU wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo aliyesimamishwa kazi na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa ubadhirifu wa fedha za Umma Michael Wage, ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa alikubali kutoa Sh milioni 10 alizoombwa na aliyekuwa mtangazaji wa shirika la Habari Tanzania (TBC1) Jerry Muro kwa kuogopa kubambikiziwa kesi kama Liyumba.

Wage, ni shahidi wa tatu katika kesi ya kuomba rushwa ya Sh milioni 10, inayomkabili Muro na wenzake Edmund Kapama na Deogratius Mgassa, walidai mahakamani hapo kuwa alitishiwa maisha na washitakiwa hao na alikiri kutoa Sh milioni moja kwa ahadi ya kumalizia nyingine tisa
kesho yake.

Akitoa ushahidi wake mbele ya Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo Gabriel Mirumbe, alidai kuwa mfululizo wa matukio hayo ulianza Januari 28, mwaka 2010 jioni, akiwa nyumbani kwake Bagamoyo ambapo alipokea simu kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kuwa jina la Jerry Muro na mtangazaji
wa TBC1.

Alidai Muro alimtaka kufika Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya naye mahojiano kwamba kuna taarifa za tuhuma zinazomkabili zilizoanza kusambaa ambazo alitaka kuweka sawa ambapo alikuja na kukutana na Muro katika mgahawa wa Carlifonia kama walivyoahidiana ambapo baada ya kukutana Muro alimwambia alikua akiandaa kipindi kuhusiana na tuhuma zake ambapo alimtaka waende katika Hoteli ya Seacliff ambako mahojiano hayo yangefanyika.

Alidai wakiwa njiani kwenye gari ya Muro kuelekea Seacliff Muro alimpigia mtu simu na katika maongezi yake alimtaja yeye (Wage) na alipokata simu alimuuliza alikuwa akiongea na nani, Muro akamjibu kuwa huyo ni Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ambaye pia alikuwa na maongezi na yeye.

Wakiwa bado njiani Wage alidai kuwa Muro alimwambia kuwa yeye ni Ofisa wa jeshi, ana nyota tatu na amesomea Marekani, ambapo alifungua ‘dashboard’ ya gari akatoa pingu na kumwambia kama akifanya vurugu au fujo ya aina yoyote angemfunga pingu na kisha alitoa bastola yenye
kitako cha rangi ya damu ya mzee na kumwambia kama yote yangeshindikana basi angempiga risasi na kumuua.

Alidai walipofika Seacliff walipokelewa na mtu mmoja mrefu, mweupe na mnene aliyejitambulisha kuwa yeye ni Kaimu mkurugenzi wa TAKUKURU anaitwa Mussa na baada ya muda akaja mwingine aliyejitambulisha kuwa ni msaidizi wa Kaimu Mkurugenzi wa TAKUKURU.

Wakiwa wamekaa meza moja Kaimu Mkurugenzi akamwambia kuwa ana tuhuma za ufisadi na kwamba hajafikishwa mahakamani aseme kama atahitaji msaada wao ambapo aliwajibu kuwa yeye sio fisadi.

Wage alidai Kaimu Mkurugenzi alimwambia kuwa hata Liyumba hakufanya kosa bali alimuambukiza Ukimwi bibi wa jamaa yake ambaye wanafanya naye kazi.

Alidai baada ya maelezo hayo alimuomba Muro amsaidie ambapo alimuomba atoe Sh milioni 10, naye akawajibu hakuwa nayo pale alikuwa na Sh. milioni moja tu, na hizo nyingine angekwenda kuwatafutia na kuziwasilisha kesho yake.

Alieleza akiwa na watu hao aliamua kumpigia mke wake aliyekuwa Morogoro simu na kuweka kipaza sauti ambapo alimtaka kumletea Sh. milioni tisa kesho, mkewe huyo alidai asingeweza kupata milioni tisa kwa kesho badala yake angeleta milioni nne tu.

Alidai kutokana na matukio ya siku hiyo aliwapigia simu ndugu zake ambao walimshauri kuripoti polisi ambapo kesho yake alienda kuripoti katika kituo cha polisi kati jijini Dar es Salaam, ambapo walimwambia ampigie simu Muro amwambie wakutane katika mgahawa wa City Garden maeneo ya Posta mpya mkabala na klabu ya Billicanas.

Wage alidai alimpigia simu Muro na kukubaliana kukutana hapo ambapo alifika saa 4:30 asubuhi na kumpigia simu kumfahamisha kama ameshafika na ndipo akajitokeza akiwa na polisi waliovalia kiraia ambapo Muro alipowatambua akataka kukimbia lakini polisi wakalizuia gari lake.

Shahidi huyo aliwatambua washitakiwa hao mahakamani na pingu, bastola na miwani ambavyo viliwasilishwa na upande wa mashitaka kama utambulisho katika kesi hiyo. Shauri litaendelea kusikilizwa tena leo kwa mashahidi upande wa mashitaka kuendelea kutoa ushahidi wao.

No comments: