Thursday, January 20, 2011

Serikali yafunga kesi ya Mramba, Yona na Mgonja leo

Upande wa Serikali leo umefunga kesi inayomkabili Waziri wa zamani wa Wizara ya Fedha, Basil Mramba, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Daniel Yona na Katibu Mkuu wa zamani wa Fedha, Gray Mgonja.

Maelezo hayo ya kufunga kesi hiyo yametolewa leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, na mwendesha mashtaka Wakili Mkuu wa Serikali Boniface Stanslaus alipotakiwa na kiongozi wa jopo la majaji watatu wanaosikiliza shauri hilo, Jaji John Utamwa kumleta kizimbani Shahidi wa 14 aendelee kutoa ushahidi wake.

Jaji Utamwa aliwataka mawakili wa pande zote mbili kuongea lolote kama wana hoja yoyote ya msingi kabla jopo halijatoa uamuzi wake.

Wakili wa Mgonja, Profesa Leonard Shahidi alidai kwa niaba ya mawakili wenzake upande wa utetezi hauna pingamizi juu ya hilo lakini aliiomba Mahakama kuwapatia nakala ya mwenendo wa kesi ili waweze kuongea kupitia majumuisho hayo.

Jaji Utamwa alikubali maombi hayo ambapo alisema shauri hilo litatajwa Februari 18, mwaka huu na kwamba kama uchapwaji wa nakala hizo utakuwa umekamilika itapangwa tarehe ya kusikiliza shauri hilo.

Hata hivyo, Prof. Shahidi aliutaka upande wa utetezi kuwapatia majumuisho ya ya hoja za mashahidi kwa ushahidi uliotolewa mahakamani hapo, ambapo alidai atawasilisha hoja kuitaka Mahakama iwaone wateja wao hawana kesi ya kujibu.

Kesi hiyo Namba 1200 ya mwaka 2008, ilianza kusikilizwa Novemba 2009, imefungwa baada ya kupitiwa kwa vielelezo 26 na mashahidi 14 kukamilisha ushahidi wao mahakamani hapo.

Katika kesi hiyo, mawaziri hao wa zamani kwa pamoja wanatuhumiwa kuingia mkataba na kuisamehe kodi kinyume cha sheria kampuni ya Alex Stewart jambo linalodaiwa kuisababisha Serikali hasara ya Sh bilioni 11.

No comments: