Wednesday, January 19, 2011

Siri hadharani


WAKATI Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) leo kinatikisa mji wa Arusha kuomboleza mauaji ya raia yaliyofanywa na polisi, hali bado si shwari kutokana na kuendelea kuibuka kwa mambo kadhaa yaliyofichwa katika tukio hilo la aibu katika mji huo wa kitalii.

Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrord Slaa na Mbunge wa Ubungo kupitia chama hicho, John Mnyika, kwa nyakati tofauti wiki hii wamekuwa wakisema chama hicho leo kimeandaa maombolezo ya wahanga wa vurugu za Arusha katika viwanja vya NMC ambako nako kulikumbwa na ghasia wiki iliyopita.

“Tutawaaga marehemu katika viwanja vya NMC Arusha Januari 12 siku ya Mapinduzi (leo). Ombi langu kwenu tujitokeze kuadhimisha mapinduzi ya kweli ya madai yetu,” unaeleza ujumbe mfupi wa Dk. Slaa katika mtandao na kupata wachangiaji karibu 300; huku kwa upande wake Mnyika akisema;

“Heshima ya mwisho ya ndugu zetu waliopoteza maisha Arusha itafanyika Januari 12 Uwanja wa NMC. Kwa rambirambi au mchango wa matibabu kwa wahanga wasiliana na kamati kupitia 0764150747."

Tayari imeelezwa kwamba Polisi imekataa CHADEMA kufanyia maombolezo katika viwanja vya NMC ingawa taarifa za maombolezo hayo zilikwishakutangazwa.

Mwenyekiti wa CHADEMA mkoani Arusha, Samson Mwigamba, amenukuliwa akisema kwamba hawatabadili eneo na kwamba walikuwa wakiendelea na mazungumzo na Polisi kuhusiana na suala hilo hali inayoashiria mvutano mwingine kati ya CHADEMA na Polisi.

Mauaji hayo yaliyofanywa na Polisi wakati wa kuzima maandamano ya amani ya viongozi na wanachama wa CHADEMA wiki iliyopita na kusababisha vifo vya watu kadhaa yamekuwa yakiibua utata na sasa yanaelezwa kugusa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na nchi jirani ya Kenya baada ya kubainika kuwa mmoja wa watu hao watatu waliouawa kwa kupigwa risasi za moto na polisi, ni raia wa Kenya.

Katika maandamano hayo ya amani yaliyofanyika Januri 5 mwaka huu, Polisi wanataja watu watatu ndio waliopoteza maisha baada ya kupigwa risasi za moto na polisi huku wengine zaidi 30 wakijeruhiwa vibaya kwa risasi na vipigo kutoka kwa polisi wa kutuliza ghasia lakini hakuna taarifa huru juu ya idadi kamili ya watu walioathirika na tukio hilo.

Marehemu hao walitambuliwa kuwa ni Denis Michael Ngowi (30) mkazi wa Songambele-Sakina, ambaye alipigwa risasi moto ubavu wa kulia, Ismael Omary (40) ambaye pia alipigwa risasi ya moto ubavuni na raia mmoja wa Kenya.

Raia huyo wa Kenya ametambuliwa kuwa ni Paul Njuguna Kaiyehe (26) ambaye maelezo yake yanayopatikana katika kitambulisho chake yanaonyesha kuwa ni mkazi wa wilaya ya Kajiado eneo la Ngong na mwili wake bado uko katika chumba cha maiti cha hospitali ya mkoa wa Arusha ya Mount Meru.

Njuguna amefahamika baada ya kupatikana kwa kitambulisho hicho katika nyumba aliyokuwa akiishi katika eneo la Sakina ambapo kitambulisho chake kinamtambulisha kama raia wa Kenya kina namba 25066938 na seriel namba yake ni 218733089.

Awali polisi katika taarifa yao walimtaja marehemu huyo kwa jina la George Mwita Waitara huku ikihofiwa kwamba lengo ni kuficha jina lake kuepuka mgogoro wa kidiplomasia na nchi hiyo jirani na mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hata hivyo wakati polisi katika maelezo yao wakidai kuwa marehemu huyo ni Mtanzania na mkazi wa mkoa wa Mara, viongozi wa CHADEMA wakioongozwa na Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema, siku ya Ijumaa, walifanya juhudi za ziada kwa kutafuta nyumba aliyokuwa akiishi marehemu huyo.

Viongozi hao wakishirikiana na viongozi wa mtaa huo walivunja mlango wa nyumba hiyo na kupekua ambapo walifanikiwa kupata kitambulisho hicho na hivyo kubaini kuwa alikuwa raia wa nchi hiyo jirani.

Habari zilizopatikana mwishoni mwa wiki mjini hapa zilieleza kuwa lengo la polisi kubadilisha jina la marehemu huyo ilikuwa ni kukwepa fedheha na kujaribu kuepusha kuingia dosari kwa uhusiano wa kidiplomasia na Kenya.

Mmoja wa maafisa wa polisi ambaye si msemaji wa jeshi hilo aliimbia Raia Mwema kwamba taarifa zilizoibuliwa baadaye na viongozi wa CHADEMA kuwa marehemu huyo ni raia wa Kenya zimelifedhehesha sana jeshi hilo na sasa maafisa wa polisi wanahaha kutoa maelezo ya kutosholeza kwa ubalozi wa Kenya kuwafahamisha jinsi raia huyo alivyopoteza maisha kwa kupigwa risasi.

“Kwa kweli wakubwa wa jeshi letu wameshtushwa sana na taarifa hizo kufahamika….na kuna vikao vinaendelea katika makao makuu ya polisi pale mkoani ili kuweka mambo sawa maana tayari ubalozi wa Kenya umeshaanza kufuatilia kifo cha raia huyo,” alisema mtoa taarifa wetu kutoka ndani ya jeshi la polisi.

Aidha taarifa zaidi zinaeleza kuwa Kenya imechukulia mauaji hayo kwa uzito wake hasa kutokana na nchi hiyo kupitisha Katiba yake mpya mapema mwaka jana na Katiba hiyo mpya imetoa nafasi kubwa kwa masuala ya haki za msingi za binadamu.

“Tumepata taarifa kuwa Ofisa wa Ubalozi wa nchi hiyo na mshauri wa masuala ya siasa wa Rais Mwai Kibaki hapa nchini ambaye ana ofisi ya kudumu mjini Arusha atakutana na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Thobias Andengenya siku ya Jumatatu kupata maelezo ya msingi jinsi raia huyo wa Kenya alivyoauwa kwa kupigwa risasi na polisi,” alieleza ofisa huyo.

Kwa mujibu wa Afisa huyo, Kenya inataka maelezo ya kuridhisha kuhusu mauaji ya raia wake ambaye habari zinaeleza kuwa alipigwa risasi katika eneo la Kaloleni akitembea barabarani kwa shughuli zake na hakuwa katika maandamano yaliyovunjwa.

“Kwa kuwa wenzetu sasa wana Katiba hiyo mpya ambayo imeweka bayana haki za msingi kuhusu maisha ya watu wake, basi, suala hilo wamelichukulia kwa uzito wa juu sana na wiki hii itakuwa moja ya wiki ngumu kwa maofisa wa polisi mkoani Arusha kueleza sababu za msingi za mauaji hayo,” alieleza ofisa huyo.

Raia Mwema ilifanikiwa kuzungumza na Balozi mdogo wa Kenya anayeshughulikia masuala ya siasa ambaye yuko mjini Arusha, Robert Mathenge, Januari 9 (Jumapili) na alithibitisha kuwa ni kweli marehemu Paul Njuguna ni raia wa nchi hiyo jirani na kuongeza kuwa wamesikitishwa sana na mauaji ya raia yaliyotokea.

“Ni kweli siku ya Ijumaa nilifika chumba cha maiti baada ya kupewa taarifa kuhusu marehemu kuwa ni raia wa Kenya na nimethibitisha kutokana na vitambulisho alivyokutwa navyo na tayari nimetoa taarifa kwa ubalozi wetu mjini Dar es Salaam”, alisema Mathenge.

Alisema pia ametoa taarifa hiyo nchini mwake ili mamlaka zinazohusika ziwatafute ndugu zake ili wakabidhiwe mwili wa marehemu huyo kwa ajili ya maziko na serikali ya nchi hiyo itatoa msaada unaohitajika kufanikisha mazishi ya raia huyo.

Mathenge alieleza kuwa kwa ujumla Kenya imesikitishwa sana na mauaji hayo ya raia lakini ni kwasasa ni mapema kusema kuwa mauaji hayo yataathiri uhusiano uliopo baina nchi hizo mbili ambazo zote ni wanachama waanzilishi wa jumuiya ya Afrika Mashariki.

“Ni kweli nitakuwa na kikao na Kamanda wa Polisi mkoani Arusha (Thobias Andengenye) ili kupata taarifa kamili ya kipolsi kuhusu mauaji hayo na baada ya hapo tutakuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kuzungumzia jambo hilo,” alisema Mathenge.

Wakati wananchi Arusha wakiwa bado na kumbukumbu ya kutisha kuhusu mauaji hayo ya polisi, madai mapya yamezidi kuibuka kuhusu mbinu mbalimbali za kutisha zilizotumiwa na askari hao, ambapo sasa inadaiwa kuwa askari hao waliwapiga risasi baadhi ya watu hata katika nyumba za ibada na pia kuwapora majeruhi, na wale waliokamatwa.

Madai mazito yalitolewa juzi na watumishi na watawa wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Theresia iliyopo jirani na Kituo kikuu cha polisi cha mjini Arusha ambapo walidai kuwa polisi walimpiga risasi mmoja wa vijana waliokimbilia kanisa hapo kuomba hifadhi.

Mmoja wa watawa wa Kanisa hilo akielezea mkasa huo kwa mwandishi wa gazeti hili alieleza kuwa kijana huyo alipigwa risasi majira ya saa 10:30 za jioni katika eneo la Kanisa hilo na kuvunjwa mguu na baadaye walimwacha hapo akivuja damu na maumivu makali.

“Baada ya kumpiga risasi sisi tulikuwa tumekimbilia ndani ya moja ya majengo ya Kanisa kutokana na hofu ya milipuko ya mabomu na risasi za moto kutoka kwa askari hao na askari hao walikuja kutuamua tufungue milango la sivyo wangelipua nyumba nzima”, alieleza Mtawa huyo.

Aliongeza: “Tulipofungua nyumba wakaanza kuwapiga makofi watumishi (wafanyakazi) wa kiume waliowakuta ndani wakiwatuhumu kuwa ni waandamanaji waliokimbilia huku kujificha…..ikabidi mmoja wetu aingile kati na kuwatetea ndipo walipowaacha.”

Mtumishi huyo wa Kanisa alieleza kuwa kijana aliyejeruhiwa aliachwa katika eneo la Kanisa bila msaada kwa zaidi ya nusu saa hadi polisi walipoitwa tena na Padre Elkana Tenges ambaye ni mkuu wa idara ya mawasiliano katika jimbo Katoliki la Arusha.

“Padre Tenges aliwaita ili wamchukue majeruhi huyo wampeleka hospitali na wasimwache katika eneo la Kanisa….na kwa bahati walirejea wakiwa na gari na kumchukua majeruhi huyo ambaye tulikuwa hatujapata jina lake,” alieleza.

Habari zaidi zinaeleza kuwa tukio hilo ndilo lililowasukuma maaskofu wa madhehebu ya Kikristo mkoani Arusha, wakioongozwa na Askofu Josephat Lebulu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, kutoa tamko na kali kulaalni mauaji hayo na pia Polisi kutumia nguvu nyingi kuzima maandamano ya amani.

Maaskofu hao pia walitamka kuwa hawako tayari kushirikiana na Meya ambaye uchaguzi wake uligubikwa na utata na ndiyo chanzo cha kutokea kwa machafuko hayo ya kisiasa ambayo yamepeleka maisha ya watu na mali kuteketea.

Aidha katika hatua nyingine ambayo imelitia doa jeshi la polisi mkoani Arusha, majeruhi na wahanga wa tukio hilo wanadai kuwa pamoja na vipigo walivyopata kutoka kwa polisi pia walitumia mwanya wa vurugu hizo kuwapora fedha na vitu vingine vya thamani kama simu, saa na mikufu ya dhahabu.

Miongoni mwa waliotoa madai hayo mazito ni Mbunge wa viti maalumu wa CHADEMA, Lucy Owenya ambaye anadai kuporwa simu zake mbili za mkononi zote zikiwa na thamani ya zaidi ya Shilingi 900,000.

Mbunge huyo juzi alikaririwa katika mkutano wa waandishi wa habari akieleza kuwa atafungua mashitaka dhidi ya jeshi hilo kufuatia askari wake kuhusika na uporaji huo.

Aidha madai kama hayo pia yametolewa na majeruhi Joackim Andrew (31) aliyelazwa katika hospitali ya mkoa ya Mount Meru ambaye anadai kuwa aliporwa kiasi cha shilingi 490,000 na simu yake ya mkononi ambayo ina thamani ya Shilingi 200,000.

Madai ya majeruhi huyo pia yameorodheshwa katika taarifa ya tukio hilo iliyokusanywa na viongozi wa CHADEMA ambayo iliwasilishwa kwa waandishi wa habari mwishoni mwa wiki.

Hata hivyo Kamanda wa Polisi Mkoani Arusha, Thobias Andengenye hakupatikana kuthibitisha au kukanusha madai hayo kwani kila alipopigiwa simu tangu kutokea kwa tukio hilo amekuwa hapokei simu yake na jeshi hilo limeshindwa kutoa ushirikiano kwa waandishi wa habari wanaotaka kufahamu taarifa mbalimbali kuhusu tukio hilo.

Tayari matamko mbalimbali yametolewa na viongozi wa dini na wale wa kisiasa kulaani vurugu hizo huku jeshi la polisi likitakiwa kujisafisha na tuhuma zinazoelekezwa kwake ikiwa ni pamoja na kuundwa kwa tume huru kuchunguza chanzo cha vurugu hizo zilizopeleka mauaji hayo.

Moja ya kauli kali zilizotolewa ni ile ya Maaskofu wa Makanisa ya Kikristo mkoani Arusha ambapo pamoja na kulaani mauaji ya wananchi hao walieleza wazi kuwa hawatakuwa tayari kushurikiana na Meya aliyechaguliwa Gaudance Lyimo kwani uchaguzi huo unalalamikiwa na wananchi.

Baada ya kauli hiyo kali ya Maaskofu Katibu wa CCM mkoa wa Arusha Mary Chatanda ambaye anaelezwa kama kiini cha machafuko hayo aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kuwataka Maaskofu hao wavue majoho yao na kuingia katika ulingo wa siasa.

Hata hivyo kauli hiyo ya Chatanda nayo ilipingwa na Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa CCM, Mzee Samwel Malecela ambaye alisema kauli hiyo ya Chatanda ni utovu wa nidhamu kwa Maaskofu hao ambao wanaheshimika sana katika jamii na alikwenda mbali kwa kumtaka Katibu huyo wa CCM awaombe radhi viongozi hao wa dini.

Akizungumza na Raia Mwema, juzi, Chatanda alisema bado anasimamia kauli yake kwake Maaskofu hao waliingilia siasa pale walipohoji uchaguzi wa Meya ambao kimsingi ulikuwa halali na ufafanuzi wake ulishatolewa na msimamizi wa uchaguzi ambaye ni Mkurugenzi wa Halmashauri.

“Kwa Maaskofu kulaani mauaji mimi sina malalamiko juu ya hilo ila sikubaliani nao pale wanapohoji kuhusu uchaguzi wa Meya kwani kwa kufanya hivyo wanaingilia siasa……na kama kuna wanafikiri kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu basi waende mahakamani, wakati tafsiri ya kisheria badala ya kuleta vurugu mtaani,” alisema Chatanda.

Akizungumzia kauli ya Chatanda mmoja wa Maafisa wa Idara ya Mawasiliano katika jimbo Katoliki la Arusha aliimbia Rai Mwema kuwa Askofu Josephat Lebulu ambaye ndiye aliyewaongoza maaskofu kutoa kauli ya kulaani mauaji na kutotambua uchaguzi wa Meya, hawezi kulumbana na Katibu wa Mkoa wa CCM kwa kuwa ni mtu mdogo sana katika mamlaka ya nchi.

“Baba Askofu hayuko tayari kujibizana na Katibu wa Mkoa wa CCM. Ni mtu mdogo….kimsingi Maaskofu walikuwa na ujumbe wao kuhusu yaliyotokea na ujumbe wao umefika kwa hiyo kama watawala wamesikia wayafanyie kazi waliyoelezwa”, alisema Afisa huyo.

Mauaji ya watu hao watatu huku wengine zaidi ya 30 wakiachwa na majeraha makubwa ya risasi za moto, kipigo na mabomu ya machozi yameweka historia mpya ya kuwa mauaji ya kwanza kutokana na vurugu za kisiasa kwa upande wa Tanzania Bara tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi nchini ulirasimishwa miaka ya 90.

Tukio la aina hiyo liliwahi kutokea visiwani Zanzibar Januari 26 na 27 ambapo polisi wenye silaha walipambana na wafuasi wa Chama Cha Wananchi (CUF) waliokuwa wakipinga matokeo ya uchaguzi Mkuu wa visiwa hivyo uliofanyika Oktoba mwaka 2000.

Wanachama hao wa CUF walikuwa wakipinga matokeo ya uchaguzi huo uliokuwa na utata ambapo Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ilimtangaza Aman Abeid Karume kuwa mshindi hivyo kuzua malalamiko kutoka kwa mgombea wa CUF Maalim Seif Shariff Hamad na wafuasi wake.

Katika tukio hilo la Zanzibar watu 21 waliuawa na polisi na wengine zaidi ya 1000 walikimbilia eneo la Shimoni Mombasa nchini Kenya na kuweka historia ya Tanzania ambayo ilikuwa maarufu kupokea wakimbizi kutoka nchi jirani zilinazokumwa na vita ya mara kwa mara nayo kuzalisha wakimbizi.

Tukio la Arusha nalo sasa limeingia katika kumbukumbu mbaya za kihistoria nchini kutokana na kumwagika kwa damu ya wananchi wasio na hatia huku mali za mailioni fedha nazo zikiteketea kufuatia vurugu kubwa zilizodumu kwa siku nzima.

Maandamano hayo yaliitishwa na CHADEMA kwa lengo la kupinga uchaguzi wa Meya wa Jiji la Arusha uliofanyika Desemba 18 mwaka jana ambapo madiwani wa CCM na TLP walimchagua Gaudance Lyimo kuwa Mstahiki Meya wa jiji hilo huku Diwani wa TLP Michael Kivuyo akichaguliwa kuwa Naibu Meya.

Uchaguzi hupo uligombewa na madiwani wa CHADEMA wakipinga hatua ya msimamizi wa uchaguzi huo ambaye Mkurugenzi wa Jiji la Arusha kumruhusu Mbunge wa Viti maalumu kutoka mkoa wa Tanga ambaye pia Katibu wa CCM mkoa wa Arusha Mary Chatanda kuwa mjumbe na kupewa fursa ya kupiga kura.

Awali maandamano hayo yalikuwa yafanyike Desemba 22 mwaka jana lakini yaliahirishwa baada ya kukosa kibali cha polisi na ndipo CHADEMA walipopanga kuyafanya Januria 5 huku wakitoa masharti kwa serikali kukaa mezani na kufanya mazungumzo nao kabla ya muda huo pia kutengua uchaguzi wa nafasi ya umeya.

Katika kipindi hicho chote kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa CHADEMA chama hicho kilikuwa katika mawasiliano na ofisi ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda,Waziri wa TAMISEMI George Mkuchika na Msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa na lengo la mawasiliano hayo ilikuwa ni kufikia muafaka wa suala hilo.

Alisema alisema mwishoni mwa wiki mjini Arusha kuwa pamoja na mawasiliano hayo Jeshi la Polisi mkoani Arusha liliwapatia barua ya kufanya maandamano Januari 4 na barua hiyo ilisainiwa na Kamanda wa Polisi wilaya ya Arusha, Zuberi Mwombeji.

Barua hiyo ambayo nakala yake tunayo ina kumbukumbu namba AR/B.5/VOL.11/63 na inaeleza kuwa:”Kimsingi mmekubaliwa kufanya maandamano na mkutano wenu wa hadhara tarehe 5 Januari na pia rejea mazungumzo yetu ya tarehe 3 saa 6 mchana ofisini kwa Kamanda wa polisi wa mkoa…….Katika mazungumzo hayo tuliona kuna umuhimu wa kuchagua route moja itakayotumika kwa maandamano.

Barua hiyo inaeleza kuwa maandamano hayo yataanzia eneo la Philips na kupita barabara kuu ya Arusha-Moshi ,Sanawari kushuka AICC,Sokoine Road,Friends Corner hadi viwanja vya NMC.

Dk. Slaa aliimbia Raia Mwema kuwa baada ya viongozi wa wilaya ya Arusha wa chama chake kupata barua hiyo waliendelea na maandalizi ya mkutano huo hadi jioni yake IGP Mwema alipotangaza kupitia vyombo vya habari kuwa hawataruhusiwa kuandamana na badala yake wamekubaliwa kufanya mkutano wa hadhara tu.

“Sisi hatukukubaliana na kauli hiyo ya IGP na kwanza hakuandika barua yoyote kama taratibu zinavyoeleza kwani sisi ni chama cha siasa na hatufanyi kazi kwa kutumia vyombo vya habari”alieleza Slaa.

Maandamano hayo Januari tano yalianza majira ya saa 6:20 za mchana nje ya hoteli ya kitalii ya Mount Meru iliyopo eneo la Sekei katika Manispaa ya Arusha na yalioongozwa na viongozi wa ngazi za juu wa CHADEMA Dk. Wilbroad Slaa, Freeman Mbowe,P hilemon Ndesamburo, na Wabunge Godbless Lema (Arusha Mjini) na Peter Msigwa (Iringa Mjini).

Waandamanaji wote walikuwa wamefunga vitambaa vyeupe katika mikono yao kuashiria kuwa maandamano yao ni ya amani na vijana wa chama hicho walikuwa wakilinda usalama kuhakikisha kuwa hakkuna waandamanaji wanaoingia miongoni mwao na kuanzisha vurugu.

Wengine ni Wabunge wa viti maalumu Lucy Owenya, Grace Kiwelu, Suzan Lyimo, Rebeca Mngodo, Joyce Mukya na viongozi wa ngazi ya wilaya, Mkoa na na madiwani wote wa chama hicho.

Viongozi hao waliandamana na wafuasi wao wachache waliopata ujasiri wa kujitokeza kufuatia vitisho vya polisi kuwa maandamano yalikuwa haramu , hadi eneo la Kaloleni na muda wote polisi walikuwa wanawatangazia kupitia vipaza sauti kuwa wavunje maandamano hayo na ndipo walipofika eneo hilo polisi walianza kurusha mabomu ya kutoa machozi na kupiga risasi kadhaa hewani kwa lengo la kutawanya maandamano hayo.

Katika eneo hilo polisi waliwatia mbaroni baadhi ya viongozi wa chama hicho ambao ni Mbowe, Godbless Lema, Lucy Owenya, Basil Lema,Joseph Selasini na wafusi kadhaa.

Wakati viongozi hao wakitiwa mbaroni Slaa na Mbunge wa Moshi Mjini Philemon Ndesamburo walikuwa wameshatangulia katika viwanja vya NMC kwa lengo la kuwapokea waandamanaji na pia kuendelea kuwahamasisha wananchi kuhudhuria mkutano huo.

Ni baada ya kubainika kuwa viongozi wengine wamekamtwa wananchi walioko katika mkutano huo walipoanza kuhamasishana kwenda polisi kwa lengo la kuwatoa na ndipo vurumai ilipoanza upya ambapo polisi walianza kukabiliana na umati mkubwa wa watu kwa kupiga mabomu ya machozi eneo hilo lote.

Vurugu hizo zilisambaa haraka mpaka katikati ya mji wa Arusha ambapo shughuli nyingi za kuchumi zilisimamama huku polisi ambao walionekana kuzidiwa nguvu wakitumia risasi za moto kuwathibiti waandamanaji ambao nao walikuwa wakirusha mawe, matofali na vipande vya mbao.

Hadi kufikia jioni tayari vurugu hizo zilikuwa zimegharimu maisha ya watu na mali ambazo hata hivyo ilikuwa vigumu kufahamu hasara iliyosababishwa na ghasia hizo lakini tayari Arusha ilikuwa imeingia katika historia mbaya ya kuwa mji wa kwanza watu wake kupoteza maisha kwa sababu za kisiasa.

Chanzo: www.raiamwema.co.tz

No comments: