Friday, January 28, 2011

DOWANS YAWASILISHA MAOMBI YA MADAI YA USAJILI WA TUZO MAHAKAMA KUU


Kampuni ya Dowans leo imewasilisha rasmi maombi ya madai ya usajili wa TUZO katika Mahakama Kuu kanda ya Dar es Salaam na kusajiliwa kwa kupewa namba ya usajili nane ya mwaka huu.

Kampuni ya Dowans ilishinda kesi ya madai dhidi ya TANESCO katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara (ICC) na kuamuliwa TANESCO kumlipa Dowans Sh Bilioni 94.

Naibu msajili mwandamizi wa mahakama hiyo Mh. Salvatory Mwongole,ameiambia Globu ya Jamii kwamba maombi hayo yameifikia mahakama hiyo januari 25 mwaka huu na yamewasilishwa na wakili wa kampuni hiyo hapa nchini kutoka kampuni ya uwakili ya Kennedy Fungamtama.

Mh. Mwongole amesema maombi hayo yamekwishapangiwa jaji lakini kulingana na unyeti wa suala hilo jina la jaji linahifadhiwa kwa sababu ndio kwanza ameteuliwa kushughulikia maombi ya usajili huo na jalada halijamfikia.

Alisema maombi hayo ya usajili yameombwa na kampuni ya Dowans Holdings S.A na Dowans Tanzania dhidi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Kwa mujibu wa sheria TUZO hiyo haitasajiliwa hadi mahakama itoe nafasi kwa mdaiwa kuwasilisha pingamizi kupinga usajili wa Tuzo hiyo kama anaona haifai kusajiliwa, na kama hana pingamizi itasajiliwa kama imekidhi sheria na mdaiwa kulazimika kulipa fedha hizo.

Wadau wengine pia wana nafasi ya kuwasilisha maombi yao kama wanadhani usajili wa TUZO hiyo haustahili nayo pia yatapokelewa, Mahakama ikishasikiliza kama kuna mapingamizi itatoa maamuzi kama ni kuisajili au la.

No comments: