Wednesday, January 26, 2011

KESI YA JERRY MURO YAZIDI ILIVYOUNGURAMA LEO

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana imepokea risiti ya pingu kama kielezo cha ushahidi katika kesi ya kuomba rushwa ya sh. milioni 10 inayomkabili aliyekuwa mtangazaji wa TBC 1 Jerry Muro na wenzake Edmund Kapama na Deogratius Mgasa.

Risiti ya Pingu hiyo iliwasilishwa na shahidi wa tano katika kesi hiyo ofisa mpelelezi Anthony Mwita (45), ambaye aliieleza Mahakama kuwa risiti hiyo yenye namba 341573B, aliipata katika duka la silaha la Mzinga lililoko Upanga jeshini jijini Dar es Salaam.

Alisema alifika katika duka hilo kupata uthibitisho kama pingu aliyokutwa nayo Jerry ilinunuliwa kwao ambapo nao walithibitisha kumuuzia pingu hiyo yenye thamani ya sh.25000 Mei 26, mwaka 2009 .

Mbali na kuwasilisha risiti hiyo pia shahidi huyo alidai katika upelelezi wake alienda katika Hoteli ya Seacliff ili kuthibitisha kama Jerry alifika hotelini hapo Januari 29, mwaka 2010.

Alidai alifika hotelini hapo Januari 31, mwaka jana na kumuona mlinzi wa KK Security aliyemtaja kwa jina la Brightone Babamika na kumuomba daftari la kuandikisha magari yaliyoingia hotelini hapo Januari 29 ambapo aliwapatia na kuona gari ya Jerry yenye namba za usajili T 545
TEH aina ya Cresta ambayo iliingia saa 7:33 mchana na kukabidhiwa kadi namba 673 na kuondoka saa 8:44 mchana.

Mwita alidai aliingia hotelini na kuuomba uongozi kuwaonyesha picha katika kamera ya CCTV ya matukio ya Januari 29 ambayo walionyeshwa na kupatiwa nakala ya picha hizo, lengo likiwa ni kuthibitisha kama kweli Jerry alifika hapo siku hiyo.

Naye shahidi wa nne alidai mahakamani hapo kuwa malalamikaji Michael Wage alikuja na fedha kiasi cha Sh milioni 10 kwenye ‘briefcase’ lakini hakuzihesabu.

Kesi hiyo itaendelea tena kesho mbele ya Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo Gabriel Mirumbe.

No comments: