Wednesday, September 29, 2010

UZINDUZI WA ILANI YA UCHAGUZI YA WAPIGA KURA 2010 KWA MAANDISHI YA NUKTA NUNDU

TANZANIA GENDER NETWORKING PROGRAMME (TGNP)
P.O. Box 8921, Dar es Salaam, TANZANIA; Gender Resource Centre, Mabibo Road, Adjacent to the National Institute of
Transport (NIT) Tel. 255 22 244.3450/ 244.3205/ 244.3286; Mobile 255 7 0754 784050/ 0754 788706; Fax 255 22 244.3244; Email
tgnp@tgnp.co.tz; Website www.tgnp.co.tz


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

UZINDUZI WA ILANI YA UCHAGUZI YA WAPIGA KURA 2010 KWA MAANDISHI YA
NUKTA NUNDU

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) unatarajia kuzindua Ilani ya Uchaguzi ya Wapiga Kura 2010 kwa maandishi ya nukta nundu, maalum kwa ajili ya wasioona, kesho Jumatano tarehe 29 Septemba 2010 kuanzia saa nne asubuhi katika viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo, karibu na Chuo cha Usafirishaji.

Ilani ya Uchaguzi ya Wapiga Kura 2010 ilizinduliwa rasmi mwezi Juni mwaka huu, kutokana na madai ya wapiga kura na kwa kutambua umuhimu wa ushiriki wa wenzetu wasioona, TGNP ikishirikiana na Sauti ya Wanawake wenye Ulemavu Tanzania ( SWAUTA) wametoa nakala za Ilani ya Wapiga Kura 2010 kwa maandishi ya nukta nundu ili nao waweze kutoa sauti zao, washiriki na kuchangia mijadala mbalimbali ya uchaguzi inayoendelea nchini kote.

Kuzinduliwa kwa Ilani kwa maandishi ya nukta nundu kutasaidia kuboresha ufikiaji na kufahamika kwa madai ya wapiga kura katika uchaguzi mkuu ujao hususan kwa makundi ya walemavu wasioona.

Aidha ilani hii itawezesha wenzetu wasioona, kutumia haki yao ya msingi kuweza kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi mkuu ujao mwezi Oktoba kwa kuhoji sera za wagombea; kutoa madai yao katika kampeni na midahalo inayoendelea nchini kote; na kuweka mikakati ya kufuatilia na kudai uwajibikaji wa serikali na viongozi watakaoingia madarakani katika kuhakikisha haki , usawa na kuboresha huduma kwa watu wenye ulemavu wa aina zote.

TGNP inakuwa mojawapo ya mashirika machache sana kuandaa nyaraka muhimu kama hizi katika mfumo wa maandishi ya nukta nundu ukiacha vitabu vya kufundishia vinavyoandaliwa na serikali kwa ajili ya kutumika mashuleni. Aidha huu ni mwendelezo wa mipango ya TGNP ya kuyafikia na kushirikiana zaidi na makundi yaliyoko pembezoni katika ujenzi wa tapo la harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi.

Wanajamii wote wanahamasishwa kushiriki katika tukio hili la kihistoria.

Imendaliwa na Mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP)
Na kusainiwa na Mkurugenzi wa TGNP – Usu Mallya
28 Septemba 2010

Tuesday, September 28, 2010

Wanamtandao wampa Dk. Slaa ushindi 76%

-Daily News walimkubali kwa 60%
-Synovate wakana madai ya CHADEMA kumpa 45%
WAKATI kampuni ya kibiashara inayojihusisha na tafiti ya Synovate Limited ikikanusha taarifa za kubaini kwamba mgombea wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Dk. Wilbroad Slaa sasa anakubalika zaidi, Watanzania wanaotumia mitandao wamempa mwanasiasa huyo asilimia kubwa ya ushindi kulinganisha na wagombea wengine.

Ufuatiliaji wa Raia Mwema, katika mitandao mbalimbali ukiwamo ule wa gazeti la Serikali la Daily News (Daily News Online Edition) na mtandao maarufu kwa mijadala wa Jamiiforums unaonyesha kwamba Dk. Slaa anakubalika zaidi katika mtandao kuliko wagombea wengine akiwamo wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete.

Hata hivyo, kumekuwa na angalizo katika mitandao kwamba si Watanzania wengi wanaotumia mitandao hata kama kuna ongezeko kubwa la matumizi ya mtandao kupitia simu za mikononi, hoja ambayo bado inaweza kutoa taswira tofauti katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, kutokana na wapiga kura wengi kuishi vijijini na wanaoishi mijini kutofahamu chochote kuhusu mtandao kama anavyosema na mchangiaji mmoja katika mtandao wa Jamiiforums:

“Ingekuwa JF (Jamiiforums) inasomwa na asimilia 50% tu ya Watanzania wote, basi, Dk. Slaa angepita kiurahisi sana. Lakini kwa kuwa wengi hawapiti humu inabidi juhudi za ziada zifanyike kushinda”.

Kura za maoni zilizokuwa zikiendeshwa na Daily News zikiwa na swali: ‘Will Dr. Slaa win the presidential race? ‘ (Je, Dk. Slaa atashinda urais?) zilionyesha kwamba kati ya watu 161 wa mwanzo waliopiga kura walionyesha kumpa Dk. Slaa asilimia 60.87 na ‘Hapana’ walikuwa asilimia 28.57, kabla ya kura hizo kusitishwa, kutokana na taarifa za kuwapo hofu ya ‘uchakachuaji’ uliodaiwa kufanywa na wafuasi au wapinzani wa Dk. Slaa.

Kwa upande wa mtandao wa Jamiiforums, zaidi ya watu 6,420 wamepiga kura hizo za maoni na kuonyesha kwamba Dk. Slaa amekubalika kwa watu 4, 895 sawa na asilimia 76.25 akifuatiwa na Kikwete ambaye anaonekana kukubalika kwa watu 779 katika mtandao huo, sawa na asilimia 12.13 akifuatiwa kwa karibu zaidi na Hashim Rungwe wa NCCR-Mageuzi aliyepata kura 448 (6.98%) wakati mgombea urais wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba akikubalika kwa watu 205 (3.19%) na Mutamwega Mugahywa wa TLP akikubalika kwa watu 93 (1.45%).

Mwazilishi wa mada hiyo ya kura za maoni aliweka swali “Je,Mtanzania gani anafaa kuwa Rais wetu 2010?” Kabla hata ya majina ya wagombea kutangazwa na yeye mwenyewe kutangaza kuwania nafasi hiyo, Dk. Slaa alikuwa akitajwa kuwania nafasi hiyo na orodha ya majina kubandikwa mtandaoni badaa ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutangaza orodha ya wagombea hao.

Wachangiaji wengi katika mtandao huo wa Jamiiforums ambao baadhi ya watu wanautuhumu kupendelea wapinzani, wamekuwa wakitoa sifa kuu za mtu anayestahili kuwa Rais wa Tanzania na kumchambua Kikwete kuwa amepoteza sifa za kuendelea na nafasi hiyo kutokana na kushindwa kupambana na ufisadi kikamilifu kama alivyoahidi wakati akiingia madarakani mwaka 2005.

Miongoni mwa sifa walizoanisha katika mtandao huo ni pamoja na kuwa Rais ajaye anatakiwa awe ni msomi, mkimya, mchapa kazi, hana makundi na asiye na chembe ya ufisadi.

Kabla ya majina ya wagombea kutangazwa, wachangiaji waliwataka wagombea wa Upinzani mwaka 2000 na 2005 wasijitokeze tena mwaka huu akiwamo Freeman Mbowe wa CHADEMA, Lipumba wa CUF, Augutine Mrema wa TLP na John Cheyo wa UDP kwa maelezo kwamba matokeo ya nyuma yanaonyesha kwamba hawana jipya mwaka huu.

“Wanachotakiwa kukifanya sasa hivi ni kumchagua mtu tofauti kabisa. CCM hawawezi kubadilika. Rais ni nafasi ya Slaa sasa kwa ajili ya kusafisha na kuziba mianya ya ufisadi mkubwa. Baada ya hapo tunaweza kuchagua Rais mchumi ili ajenge uchumi wa nchi. Kwa sasa lazima tuondoe ufisadi kwanza, CCM hawawezi kuuondoa.

“Kikwete alisema anawajua wala rushwa, wauza madawa ya kulevya, wezi wa EPA waliorudisha fedha na wale wahujumu wa Bandarini lakini kashindwa kuwataja wala kuchukua hatua ilhali yeye tumempa mamlaka yote kikatiba ili ailinde nchi hii na mali zake.

“Slaa ni mzalendo wa kweli maana pamoja na kuwa hana mamlaka ya kuwafanya lolote mafisadi lakini kawataja hadharani bila woga au kuumauma maneno ingawa anajua hatari inayomkabili kupambana na watu wa aina hiyo. Huyu akipewa mamlaka ya kuongoza nchi mafisadi, wezi wa mali za umma nk, itabidi wakajichimbie makaburi wajizike wenyewe. Slaa ndio Rais anayefaa kwa wakati huu tulionao,” anasema mchangiaji mmoja wa Jamiiforums.

Baadhi ya vyombo vya habari wiki hii vilimnukuu Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe akisema kuwa CHADEMA ina matokeo ya kura za maoni za Synovate yanayoonyesha kuwa Dk. Slaa anakubalika kwa asilimia 45 akifuatiwa na Rais Kikwete mwenye asilimia 41, kauli iliyowalazimu Synovate kukanusha.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi Jumatatu, Meneja wa Synovate Limited, Aggrey Oriwo alisema taarifa hizo ni za kughushi, hazina ukweli wowote na zinaupotosha umma kwa kuwa hawajawahi kufanya utafiti wowote unaohusu kukubalika kwa wagombea wa urais.

Oriwo alisema kwa kawaida kampuni yao hufanya utafiti wa hali ya kisiasa kila baada ya miezi mitatu na kwamba wanatarajia kufanya hivyo kabla ya Oktoba 31 na kutoa taarifa yao, kauli iliyotolewa pia na Taasisi ya Mpango wa Utafiti na Elimu Demokrasia Tanzania (Redet), ambao nao wanatarajia kufanya utafiti wa mgombea anayekubalika.

Monday, September 27, 2010

CUF, Chadema vyafanya mdahalo wa wagombea vijana

MDAHALO wa wagombea wa ubunge vijana wa vyama vya CUF na Chadema umefanyika na kufana bila kuwepo kwa wagombea ubunge wa CCM.

Mdahalo huo ulioongozwa na mwanaharakati Jenerali Ulimwengu, ulitoa nafasi kwa wagombea hao kuonesha uwezo wao wa kutetea ilani za vyama vyao tofauti na ilivyokuwa ikidaiwa na CCM ambayo imekataza wagombea wake wasigombee.

Katika mdahalo huo, wagombea hao walipewa nafasi ya kuelezea sera za vyama vyao na ahadi zilizopo katika ilani za vyama vyao kuhusu changamoto kadhaa za kijamii na kiuchumi kabla ya wananchi kupewa fursa ya kuwauliza maswali.

CCM katika maelezo yake ya kukataa kushiriki katika midahalo yote ya wagombea, moja ya sababu za kufikia uamuzi huo ilisema kuwa ni kutokana midahalo hiyo na kutawaliwa na malumbano na matusi kuliko fursa ya wagombea kutangaza sera.

Lakini jana katika mdahalo huo uliorushwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha ITV, kila chama kilipewa muda sawa na kingine kujibu hoja kwa kueleza ahadi zilizoko katika ilani zao za uchaguzi kwa wananchi na kuonesha uwezo wa vijana hao kujibu hoja.

Katika hoja ya Muungano, mgombea wa Chadema katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ambaye aliongoza upande wa chama hicho, alisema chama hicho kitaimarisha Muungano ili utumike kama mfano katika kujenga muungano wa Afrika Mashariki na hatimaye Muungano wa Afrika.

Alisema lengo la kuimarisha Muungano, ni kutimiza ndoto za waasisi wa dhana ya Muungano wa Afrika, Kwame Nkrumah na Mwalimu Julius Nyerere.

Kwa upande wa CUF, mgombea wa ubunge wa Ubungo kupitia chama hicho, Julius Mtatiro ambaye alionekana kuongoza upande wa chama hicho, alisema wamedhamiria kuanzisha serikali tatu ili kuondoa malalamiko ya kero za Muungano.

Kuhusu serikali zao zitakavyotekeleza sera za kutoa elimu na afya bure, Mtatiro aliwataka Watanzania wawape kura wagombea wa CUF, ili waoneshe namna ya kubana matumizi na kupeleka fedha zinazopotea katika kutoa huduma hizo.

Alisema katika Serikali ya CUF, ikibidi mawaziri watapanda teksi ili kubana matumizi.

Kwa upande wa Chadema, Zitto alisema kama Nyerere aliweza kutoa elimu na afya bure kwa kutumia fedha za katani na kahawa, chama hicho kitatoa huduma hizo bure kwa kutumia fedha za dhahabu, gesi na Tanzanite.

Umahiri wa kujibu hoja wa wagombea hao, ambao CUF walikuwepo wawakilishi watatu na Chadema wawakilishi watano, ulimfanya msimamizi wa mdahalo huo, Ulimwengu kuhitimisha kwa kauli kuwa vijana wanaweza.

“Mdahalo huu umeonesha vijana wanaweza kutetea taifa lao...wao ni taifa la leo, kesho na kesho kutwa wakati wazee ni taifa la leo, jana na juzi,” alisema.

Wednesday, September 22, 2010

UNFPA Head Asks World Leaders to Put Women’s Health at Heart of Development Priorities



UNITED NATIONS, New York

UNFPA Executive Director Thoraya Ahmed Obaid today called on world leaders to increase funding for reproductive health, including family planning, and place women’s health at the centre of their national plans.

“Now is the time to move from speech lines to budget lines,” said Ms. Obaid at an event during the MDG Summit which started today at the United Nations. “Women deliver for their families, communities and nations, and now it is time to deliver for women. No woman should die giving life. There are still 1,000 women who die needlessly every day from complications of pregnancy and childbirth. There are still 215 million women with an unmet need for family planning and 2 million women suffering from the devastating childbirth injury of obstetric fistula. ”

“Investments in reproductive health pay high dividends and advance productivity, economic growth and the rights of women,” said Ms. Obaid, stressing: “The health of women is not the focus of the health sector alone. The health of women depends on planning and investments across many sectors—in education, health, nutrition, gender equality, and infrastructure.”

“Roads and electricity, for example, should be directed towards health centres to support women and families,” Ms. Obaid emphasized. “National plans should prioritize community access to an integrated package of affordable and essential health services, including family planning, maternal health care and HIV prevention and treatment.”

Ms. Obaid assured world leaders that UNFPA was committed to helping nations strengthen their health systems and achieve universal access to reproductive health by 2015.

“We are working with WHO, UNICEF, UNAIDS and the World Bank to reduce high rates of maternal and newborn deaths in high priority countries,” said Ms. Obaid. “Together with the Reproductive Health Supplies Coalition, UNFPA aims to expand family planning to 100 million women by 2015. We are supporting national counterparts to train and deploy midwives, and also to prevent and treat fistula.”

“UNFPA fully supports the Global Strategy for Women’s and Children’s Health to be launched by the UN Secretary-General on Wednesday to save 16 million lives by 2015,” Ms. Obaid concluded.

Ms. Obaid received an MDG Lifetime Achievement Award in New York on the eve of the Summit, for promoting gender equality and the empowerment of women. The MDG Awards are given annually to honour exemplary contributions towards the development goals.

Tuesday, September 21, 2010

Synovate:Mbowe muongo

TAASISI ya utafiti ya Synovate imesema haijafanya utafiti wowote kuhusu wagombea wa nafasi za urais unaoonesha kuwa mgombea wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa anakubalika zaidi na wananchi.

Baadhi ya vyombo vya habari (si gazeti hili) jana vilimnukuu Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akisema kuwa Chadema ina matokeo ya kura za maoni za Synovate yanayoonesha kuwa Dk. Slaa anakubalika kwa asilimia 45 akifuatiwa na Rais Kikwete mwenye asilimia 41.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Mbowe anadaiwa kusema kuwa takwimu hizo hazikutolewa Septemba 14 walipotoa taarifa za namna vyombo vya habari vinavyoripoti kampeni za uchaguzi mkuu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Dar es Salaam, Meneja wa Synovate, Aggrey Oriwo alisema taarifa hizo ni za kughushi, hazina ukweli wowote na zinaupotosha umma kwa kuwa hawajawahi kufanya utafiti wowote unaohusu kukubalika kwa wagombea wa urais.

“Kauli ya Mbowe imetukera sana na magazeti yalioandika pia yametukera, hakuna ukweli wowote na sisi ni kampuni huru, hatuwezi kubania taarifa yoyote, hatuegemei upande wowote, tayari tumewasiliana na vyombo husika vya habari na tumeandika barua kwa Baraza la Habari Tanzania (MCT) kulalamikia suala hilo,” alisema Oriwo na kumtaka Mbowe kuweka bayana ushahidi kuhusu takwimu hizo.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya jana, Mbowe alitoa kauli hiyo katika mkutano wa kampeni uliofanyika Sanya Juu, mkoani Kilimanjaro.

Alidai sababu za kutotolewa utafiti huo zinatokana na CCM kuikataza taasisi hiyo kufanya hivyo. Meneja huyo hakuwa tayari kuweka bayana kama watafanya utafiti kuhusu wagombea hao kwa madai kuwa wakati huu wa kampeni utafiti kama huo una hatari.

Alisema kazi zao zina mipaka na utafiti kama huo ukifanyika, watautoa kwa jamii kupitia vyombo vya habari kama ambavyo wamekuwa wakifanya.

Monday, September 20, 2010

Kampeni Pemba kuwa za kitanda kwa kitanda

MGOMBEA mwenza wa urais wa Tanzania kupitia CCM, Dk. Mohammed Gharib Bilal amewaomba wananchi wa Pemba wampigie kampeni ya kitanda kwa kitanda, nyumba kwa nyumba na mtaa kwa mtaa mgombea wa kiti cha urais Zanzibar, Dk. Ali
Mohammed Shein ili aingie Ikulu kwani uwezo wa kuongoza anao.

Naye Dk. Shein amewaambia wananchi hao kuwa safari yake ya kwenda Ikulu imeanza, huku akidai wakimchagua atahakikisha anaweka sawa yale ambayo yamekuwa yakiwatatiza.

Kauli hizo zilitolewa jana kwenye Uwanja wa Gombani ya Kale mjini hapa, ambapo chama hicho kilikuwa kinazindua kampeni za mgombea huyo wa urais upande wa kisiwa cha Pemba baada ya juzi kufanya hivyo Viwanja vya Kibandamaiti upande wa kisiwa cha Unguja.

Huku akishangiliwa na wananchi waliofurika kwenye viwanja hivyo kutoka maeneo mbalimbali ya Pemba, Dk. Shein alisema safari yake ya kwenda Ikulu ilianza jana kwenye viwanja hivyo upande wa Pemba kama ilivyokuwa kwa Rais wa Zanzibar, Amani Karume mwaka 2000 alipoanzia safari yake ya kwenda Ikulu kwenye viwanja hivyo.

"Safari yangu ya Ikulu imeanza leo Gombani ya Kale, sasa ni pakubandika pa kubandua, moja mbili, wahedi thinina (Kiarabu) na Kiingereza one..two mpaka Ikulu.

Nasema mambo ya Pemba sasa yatakuwa bomba," alisema Dk. Shein na kufafanua kuwa mwaka 2000 Rais Karume alifika kwenye eneo hilo na kuwaomba wananchi wampe kazi ya urais awatumikie naye pia amefanya hivyo.

Aliwaomba wakazi wa Pemba wamuombee dua ashinde na pia aweze kuwatumikia Wazanzibari kwani uwezo huo anao na ataendeleza yote yaliyofanywa na Rais Karume.

Alisema huu si wakati wa Wazanzibari kufanya makosa, kwani nchi imefikia hatua nzuri kimaendeleo, hivyo wasirudi nyuma badala yake wampe yeye nafasi afanye mambo mazuri zaidi na kama wapo wanaohitaji kunong'onezwa ili wampigie kura lifanyike, wanaohitaji kupigiwa hodi vyumbani nao pia wafanyiwe hivyo.

Alieleza kuwa kwa jinsi alivyofanya kazi na Rais Jakaya Kikwete na anavyomfahamu Dk. Bilal wakishinda itakuwa ni mteremko tu, ni kama maji kushuka kwenye mlima.

Naye Rais Karume akizungumza kabla ya kumkaribisha Dk. Shein alisema CCM imemteua kuwania nafasi hiyo kwa vile inamuamini kwamba anaweza kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya chama hicho kwa ufanisi.

Aliwaeleza wananchi kuwa Dk. Shein ni mtu mzuri, muungwana, shupavu, hodari na ana uwezo wa kufanya kazi, jambo ambalo ndilo kubwa na kuwakumbusha wananchi wa Pemba jinsi mwaka 2000 Rais mstaafu wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi alivyosimama kwenye viwanja hivyo kumpigia debe yeye akisema ni mtu makini na mwenye uwezo.

"Mzee Mwinyi alisema maneno mazito na namnukuu alisema, namfahamu vizuri Karume ni mtu mzuri, anaweza kusuluhisha nyoyo za Wazanzibari.

Nawauliza nyie hapa leo, tumefanya hilo au hatukufanya?" Alihoji na kuitikiwa na kauli ya ndiyo, hivyo kuongeza kuwa naye ana imani na Dk. Shein.

Alisema mambo mbalimbali yaliyofanywa na serikali yake anaamini Dk. Shein ndiye anayeweza kuyaendeleza, hivyo ni jukumu la kila mmoja kutimiza wajibu wake na kufanya kampeni ili Dk. Shein amiminiwe kura.

Friday, September 17, 2010

CUF ikishinda Chenge kukamatwa

CHAMA cha Wananchi (CUF), kimesema kikichaguliwa kuingia Ikulu, ndani ya siku 11 watamkamata mgombea wa ubunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge na kumuweka chini ya ulinzi.

Mkurugenzi wa Siasa na Naibu Meneja wa Kampeni wa chama hicho, Mbarala Maharagande aliyasema hayo juzi wakati akihutubia mkutano wa kampeni uliofanyika katika eneo la kituo cha basi cha zamani mjini hapa.

Aliilaumu serikali kwa kile alichodai kuwa imewaacha watuhumiwa wa rushwa kuwania nafasi za uongozi za kisiasa jambo linaloisumbua jamii.

“Tayari tumekubaliana kama chama kwamba hatutawavumilia wala rushwa ambao majina yao yameorodheshwa, tutavalia njuga suala hili na kwa kuanza tutamkamata Chenge katika siku kumi na moja baada ya uchaguzi tukiingia madarakani,” alisema.

Maharagande pia alizungumzia hali duni ya maisha ya wananchi sambamba na huduma mbovu za jamii katika jimbo la Bariadi Magharibi ambako mgombea mwenza wa urais wa chama hicho, Juma Duni Haji alikuwepo akifanya kampeni katika vijiji vya Manemhi na Mihango.

Alisema watamshitaki Chenge kwa matumizi mabaya ya madaraka aliyoyafanya wakati akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na Waziri wa Maendeleo ya Miundombinu kwa kuingia mikataba mibovu ikiwa ni pamoja na ule wa ununuzi wa rada.

“Ni aibu kujua kuwa nusu ya watu wa Bariadi Magharibi hawana viatu hasa katika wakati huu wa maendeleo ya sayansi na teknolojia na mbunge wenu hafanyi jitihada zozote kuwakwamua katika hili,” alisema Maharagande.

Katika hatua nyingine, Maharagande alimkosoa Spika wa Bunge, Samuel Sitta kwa maoni yake aliyodai hayakuwa na busara kuhusu baadhi ya ahadi zilizotolewa na wagombea wa urais wa upinzani.

Maharagande alidai Sitta aliidhinisha matumizi ya fedha nyingi katika ujenzi wa ofisi yake na hakutarajiwa kutoa maneno hayo na kulalamika kuwa nchi ni masikini na hakupaswa kutumia kiasi chote hicho cha fedha.

“Tatizo pekee hapa ni matumizi mabaya ya rasilimali za Taifa na kutokuwa na vipaumbele, lakini kama tukitumia hekima katika matumizi ya rasilimali zetu, tungefanya makubwa.

“Haileti maana ni kwa namna gani Sitta aliridhia kiasi hicho cha fedha kwa ujenzi wa ofisi yake wakati barabara ya kwenda jimboni humo imejaa vumbi,” alisema.

Thursday, September 16, 2010

Slaa amuweka pabaya Salma

-Atumia nyenzo za serikali kumkampenia mumewe
-Kinana amtetea
MWENYEKITI wa Kampeni za Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahaman Kinana amekiri kuwa Mke wa Rais, Salma Kikwete, hutumia ndege za Serikali wakati wa kumfanyia kampeni mume wake, Rais Jakaya Kikwete na wagombea wengine wa chama hicho katika nafasi za ubunge na udiwani.

Hata hivyo, Kinana amemtetea Salma Kikwete kwa kusema kwamba hakuna sheria iliyovunjwa kwa kuwa ndege hizo hukodishwa.

Kwa mujibu wa Kinana, hata mgombea urais wa CCM, Kikwete wakati mwingine hutumia ndege za serikali kwa kukodi pindi inapotokea ndege za mashirika binafsi zinazoaminika kwa usalama zimekodiwa na watu wengine.

Ufafanuzi huo wa Kinana unatokana na tukio la Mke wa Rais, Salma, kuwasili mkoani Mara kwa ndege ya Serikali aina ya Focker 50, yenye namba 5H-TGF na kupokewa na viongozi wa Serikali akiwamo Mkuu wa Mkoa, Enos Mfuru, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Maram, Robert Boaz, Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Geofrey Ngantuni na viongozi wengine wa mkoa na ngazi ya wilaya, wote wakifika uwanjani hapo kwa kutumia magari ya Serikali.

Baada ya kuwasili na kupokewa na wana-CCM uwanjani hapo, tofauti na ziara nyingine ambazo zimekuwa zikitangazwa ili wananchi wajitokeze kumpokea, wakati huu haikutangazwa na hivyo alipokewa na watu wanaoaminika wafuasi wa CCM waliopewa taarifa kwa masharti ya kutotangaza ujio huo.

Kiongozi huyo baada ya kupokewa na kukagua vikundi vya ngoma alipanda katika gari lililokuwa na namba za kiraia aina ya VX V8 Land cruiser T206 BJY lakini linaloaminika kuwa ni la serikali; huku ujumbe wake ukitumia pia magari ya serikali kuelekea Ikulu ndogo, Mjini Musoma.

Akizungumzia hali hiyo, Kinana alikiri Salma kutumia ndege ya serikali na kwamba si katika safari yake ya Musoma tu bali hata alipokwenda Mwanza alitumia ndege ya serikali. Alisema ndege hiyo imekuwa ikikodiwa kutoka kwa Wakala wa Ndege wa Serikali na kwamba mtu yeyote anaruhusiwa kukodi ndege hizo.

“Tumekuwa tunatumia ndege za Serikali kwa kukodi hasa pale ndege za mashirika binafsi ambazo tunaziamini kwa maana ya usalama wake zinakuwa zipo kwenye matumizi mengine. Kwa hiyo hatuwezi kutumia ndege nyingine tusizoziamini kiusalama, na kwa hivyo tunakodi ndege hizo. Tunazo risiti za malipo na mtu yeyote anaweza kukodi ndege hizo,”

“Kuna upotoshaji tu unafanywa na watu ambao wanajua ndege hizo zinaweza kukodiwa na yeyote. Kwa hiyo mgombea wetu wa urais aliwahi kutumia ndege hiyo katika baadhi ya kampeni na Mama Salma ameitumia mara kadhaa,” alisema Kinana na kusisitiza kuwa CCM inatambua vyema masharti ya sheria zote za Uchaguzi Mkuu na haiwezi kufanya kinyume kwa kuwa sheria hizo zimepitishwa chini ya Serikali ya chama hicho.

Hata hivyo, Kinana hakufafanua matumizi ya magari ya serikali katika mikutano ya kampeni ya Kikwete ambayo Mama Salma anaifanya akiandamana na viongozi wa mikoa.

Wakati CCM ikitoa ufafanuzi huo wa matumizi ya Salma Kikwete ya ndege ya serikali, taarifa zaidi kutoka mkoani Mara kuhusu ziara ya mama huyo zinaeleza kuwa, alizuru Wilaya ya Bunda baada ya kumaliza shughuli zake wilayani Musoma.

Akiwa wilayani Bunda alifanya mkutano wa ndani wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) na pia ratiba ilimuelekeza kwenda Jimbo la Mwibara, Jumatatu wiki hii, lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana na eneo hilo kuwapo mgombea wa urais wa CHADEMA, Dk Willbrod Slaa.

Taarifa hizo zinabainisha kuwa pamoja na kuwapigia debe wagombea wa CCM akiwamo mumewe Rais Jakaya Kikwete, Salma amekuwa akijitahidi kufanya usuluhishi wa makundi ili kuvunja kambi zilizoibuka wakati wa mchakato wa kura za maoni ndani ya CCM.

Hoja ya ufisadi inayotumiwa kumtambulisha Dk. Slaa ikionekana kumbeba katika taswira ya kukubalika zaidi kwa wapiga kura, imekuwa pia ikitolewa ufafanuzi na Salma Kikwete katika ziara zake hizo.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotufikia, Salma amekuwa akizungumzia hoja ya ufisadi kwa maelezo kuwa Serikali ya CCM imefanya na inaendelea kufanya kazi kubwa kupambana na vitendo hivyo ambavyo alidai vilikuwapo tangu enzi za TANU. TANU ndiyo moja ya chama kiasisi cha CCM, kikiwa na rekodi ya kuongoza mapambano ya kudai uhuru.

“Jamani hata nyumba haiwezi kujengwa kwa siku moja. Nawaomba sana kuvunja makundi na kuwa pamoja na walioshindwa kura za maoni ili kuhakikisha CCM inashinda na hili ndilo lengo kuu la ziara yangu hapa. Muende nyumba hadi nyumba kueleza mafanikio ya Serikali ya Rais Kikwete ili wananchi watambue pumba na mchele ni upi,” alisema

Soma zaidi

Wednesday, September 15, 2010

Slaa awasha moto upya

- Ataka majibu ya Kagoda, Tangold
- Asisitiza hatanyamaza hadi kieleweke
Mgombea urais kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibroad Slaa, ameibua mzimu wa kampuni ya Kagoda inayodaiwa `kukwapua’ Sh. bilioni 40 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (Epa) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Dk. Slaa amemtaka mgombea wa nafasi kupitia CCM, Rais Kikwete, kutafuta suluhu dhidi ya kashfa ya Kagoda, ili awatendee haki Watanzania.

Alikuwa akihutubia katika mkutano wa hadhara kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Mukendo mjini hapa.

Dk. Slaa alisema kikao kilichofanikisha ‘kuchotwa’ fedha hizo katika benki ya CRDB, kilifanyika chini ya uenyekiti wa Rais wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa.

Kwa mujibu wa Dk. Slaa, kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mbunge wa Igunga aliyemaliza muda wake, Rostam Aziz.

Alidai kuwa Chadema imeshatoa ushahidi wa kina kuhusiana na wizi wa Epa, lakini katika hali ya kushangaza, Rais Kikwete amekuwa na kigugumizi kwa kampuni ya Kagoda.

“Kukaa kwako kimya kunamaanisha kuwa fedha hizo ndizo zilikuingiza madarakani...tunataka kujua, Kagoda ni kampuni ya nani, mbona unapata kigugumizi,” alihoji.

Dk. Slaa alisema hawezi kufunga mdomo bila asizungumzie kashfa hiyo mpaka hatua zitakapochukuliwa dhidi ya Kagoda na kampuni ya Tangold.

“Tangold ambayo tulielezwa ni ya serikali ilisajiliwa Mauritius na mmoja wa wanahisa ni Andrew Chenge, lakini tunaambiwa mwenye hisa anaweza kuzimilikisha kwa mke, mtoto au mpwa...hivi mpwa wa serikalini nani,” alihoji.

Dk. Slaa alifafanua kuwa Sh. bilioni 155 zilizopelekwa katika mgodi wa Buhemba kupitia Tangold, zingeweza kuboresha sekta ya elimu nchini.

Sitta ashutumiwa ‘kulindana’ Pia Dk. Slaa alimshukia mgombea ubunge wa jimbo la Urambo Mashariki (CCM), Samuel Sitta, na kumwita mnafiki katika masuala yanayohusu maslahi ya umma.

Alidai kuwa Sitta aliyekuwa Spika wa Bunge lilimaliza muda wake, alitumia cheo hicho vibaya kuizima kashfa ya Richmond bungeni.

Pia alidai kuwa Sitta alimkataza (Dk. Slaa) kuzungumzia mishahara minono ya wabunge.

“Niliposimama bungeni kuhoji ni sehemu gani Tanzania petroli inauzwa Sh 2,500, Sitta alinitaka nikae kimya na akasema taarifa yangu isiingie kwenye hansard ...wabunge wanaelea kwenye anasa, Sitta anataka posho iongezwe,” alisema.

Alidai kumpigia simu Sitta, lakini hakupokea hivyo akalazimika kumwandikia ujumbe mfupi kumkumbusha namna elimu ilivyokuwa bure enzi za Mwalimu Julius Nyerere.

Akizungumzia mabango ya CCM, alidai kuwa na ushahidi kwamba yametengenezwa kwa fedha ya Ikulu ambazo ni kiasi cha Dola za Marekani milioni 1.5.

Makamba alipuliwa

Dk. Slaa alidai kuwa Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, ndiye aliyesaini mkataba huo na kampuni ya Mediapix ya Canada, chini ya uratibu wa Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu, Salva Rweyemamu.

Jimbo la Musoma Mjini ni moja kati ya majimbo yenye ushindani mkubwa hasa kwa kuzingatia kuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya Chadema, Vincent Kiboko Nyerere ni mwanafamilia ya Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Tutaboresha gongo iwe halali

Wakati huo huo, Dk. Slaa, ameahidi kuruhusu matumizi ya teknolojia itakayoboresha pombe ya gongo, ili itambuliwe kisheria.

Dk. Slaa alisema hatua ya kuiweka gongo katika matumizi halali ya binadamu, itakuwa na manufaa kwa taifa na kusaidia kuwapunguzia askari polisi kazi ya kufukuzana na watumiaji wa kinywaji hicho ambacho hivi sasa ni haramu.

Alisema hayo wakati akihutubia mkutano wa kampeni za Uchaguzi Mkuu uliofanyika katika uwanja wa Getrude Mongela uliopo mjini Nansio, Ukerewe.

Licha ya gongo kuwa bidhaa haramu kwa mujibu wa sheria, watu wengi katika maeneo mbalimbali nchini, hasa wa kipato cha chini wanaitumia kama kiburudisho.

Pia, Dk. Slaa alisema pombe hiyo ikiboreshwa itawaongezea kipato Watanzania wanaoitegemea kama biashara kuu na kuliingizia taifa mapato yatakayotokana na kodi.

Alisema zipo pombe kali kama konyagi ambayo kiwanda chake kilianzishwa na Rais wa kwanza wa Tanzania, Hayati Nyerere, ambayo hivi sasa bei yake ni kubwa ikilinganishwa na bia.

Dk. Slaa alisema ikiwa atashinda katika uchaguzi huo, serikali yake itatafuta na kugawa bure kwa watengenezaji wa pombe hiyo, mashine za kisasa na kusimamaia viwango vyake ili watengeneze kinywaji kinachokubalika.

Akizungumzia mauaji ya watu 14 yaliyatokea usiku wa Januri 17, mwaka huu katika kisiwa cha Izinga, Dk. Slaa aliwapa pole wafiwa na kusema kwa kiasi kikubwa, tukio hilo lilichangiwa na uzembe wa serikali ya CCM.

Alisema serikali inawajibika kuwalinda raia wake, jambo ambalo si hisani bali limeanishwa miongoni mwa wajibu wa serikali.

Dk. Slaa alisema suala la ulinzi wa raia lina maslahi kwa umma, hivyo akawataka wananchi kuondokana na tofauti za itikadi zao ili wamuunge mkono na kumchagua kuwa Rais wa Tanzania.

Habari hii imeandikwa na Restuta James, Musoma na Jovither Kaijage, Ukerewe.


SOURCE: NIPASHE

Tuesday, September 14, 2010

Mbatia: Kampeni za kashfa hazina tija kwa umma

Mwenyekiti wa chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, ametoa rai kwa wagombea katika Uchaguzi Mkuu wa kushindana kwa hoja za kimaendeleo badala ya kashfa zisizokuwa na tija kwa umma.

Mbatia anayewania ubunge wa jimbo la Kawe, alitoa rai hiyo juzi katika viwanja vya Tanganyika Packers jijini Dar es Salaam.

Alikuwa akizungumza katika uzinduzi wa kampeni za NCCR-Mageuzi, uliohudhuriwa pia na mgombea urais kupitia chama hicho, Hashim Rungwe na mgombea mwenza wake, Ally Omary.

Mbatia alisema wagombea hao wanapaswa kumtanguliza mbele Mwenyezi Mungu kila wanapokuwa jukwaani, ili hekima, umoja na amani vitumike badala ya kauli zinazoweza kuchochea chuki.

Mbatia aliwataka wapiga kura kuwa na hekima ya kuchagua viongozi bora na si kuangalia vyama wanavyotoka.

Mbatia alitaja vipaumbele vya ilani ya chama hicho, vikigusia utawala bora, sekta ya uchumi, huduma za kijamii, makundi ya watu maalumu, vyombo vya habari, mashirika yasiyo ya kiserikali na usawa wa jinsia.

Alisema ikiwa NCCR itashinda katika uchaguzi huo, asilimia 30 ya bajeti ya nchi itaelekezwa katika uboreshaji wa elimu.

Mbatia alizungumzia msongamano uliopo jijini hapa na kuahidi kutumia mbinu mbalimbali zitakazofanikisha kuondokana na kero hiyo.

Alisema ikiwa NCCR itapata ushindi serikali itaanzisha usafiri imara wa majini na kujenga gati ufukweni wa bahari.

Alisema usafiri huo utaanzia Bagamoyo-mbweni-Kunduchi-Mbezi beach-Msasani mpaka bandari ya Dar es Salaam.

Pia alisema serikali ya NCCR itaanzisha usafiri wa reli ikiwa ni mojawapo wa njia za kukabiliana na msongamano jijini humo.

Alisema usafiri wa reli utawalenga zaidi wakazi wa jijini kutoka Pugu-Gongolamboto-Vigunguti-Buguruni mpaka kituo kikuu cha kati.

Uzinduzi huo ulihudhuriwa pia na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Jordani Rugimbana na Mkuu wa Idara ya Sheria, Katiba na Haki za Binadamu wa chama hicho, Dk Sengondo Mvungi.

CHANZO: NIPASHE

Monday, September 13, 2010

Unyumba wa Dk.Slaa walipua siri za vigogo

-Baadhi ya siri za unyumba wa vigogo zaanikwa
GUMZO la unyumba wa mgombea urais wa CHADEMA, Dk.Willibrod Slaa na Josephine Mushumbusi, limeibua utata ndani ya familia za vigogo wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na hali si shwari baada ya baadhi ya mambo kuanikwa hadharani, Raia Mwema limebaini.

Suala hilo ambalo tayari limeingia katika mikono ya kisheria, limeelezwa kuwakera baadhi ya wafuasi wa Dk. Slaa wakiwamo baadhi ya viongozi ambao sasa wamebainisha wazi kwamba viongozi wa CCM “wanaishi nyumba za vioo wasirushe mawe.”

Baadhi ya viongozi wa CHADEMA wakiwamo wanasheria na wanasiasa wamelieleza Raia Mwema kwamba taarifa na matukio yanayoendelea kuhusiana na maisha unyumba wa Dk. Slaa ni ishara tosha ya CCM kukosa hoja dhidi ya mgombea wao na hivyo kutafuta hoja dhaifu zisizo na maana.

Akizungumza na kwa simu kutoka Singida alipo na Dk. Slaa, mwanasheria wa CHADEMA na mgombea Ubunge wa chama hicho Singida Magharibi, Tundu Lissu, alisema ni utamaduni wa CCM wanapoona wamezidiwa kutafuta hoja dhaifu kushambulia wagombea wenye nguvu na kwamba CHADEMA watajibu mapigo ikibidi.

Lissu ambaye amekuwa na historia ya kupambana na Serikali kuhusiana na masuala ya madini, alisema hawaoni sababu ya kujibizana na propaganda za CCM pamoja na kuwa wana taarifa nzito kuhusiana na uchafu wa viongozi wa CCM ikiwa ni pamoja na uchafu huo kuhusisha matumizi ya fedha za umma.

“Hatutaki kujibizana na propaganda zao chafu ambazo wamezizoea tangu kuanza tena kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1995 walipomtafuta Angelina kumchafua Mrema (Augustine Mrema) wakati ule Mrema akiwa na nguvu. Lakini lazima tujiulize wana uhakika gani na maisha binafsi na afya za wagombea wao?”

Alisema baada ya kumchafua Mrema mwaka 1995, mwaka 2005 waliibuka na mkakati wa kwamba Chama cha Wananchi (CUF) kilichokuwa kina nguvu kilikuwa kimeingiza nchini kontena la visu katika taarifa ambayo ilitangazwa na aliyekuwa Inspekta Jenerali wa Polisi, Omari Mahita.

Alisema pia kwamba ni mambo ya aina hii yaliyoibuka pia mwaka huohuo walipoanza kuchafuliwa wagombea wa urais katika uchaguzi wa ndani ya chama pale mwanadiplomasia Dk. Salim Ahmed Salim na aliyekuwa Waziri Mkuu, Frederick Sumaye walipochafuliwa na wana CCM wenzao.

Lissu alisema ni viongozi wachache ndani ya CCM wanaoweza kujitokeza hadharani kuzungumzia mahusiano yao ya unyumba na kwamba baadhi yao hawajawahi kuweka wazi kuhusiana na idadi ya wake na watoto walio nao nje ya ndoa zinazofahamika hadharani.

“Je, wako tayari kutueleza idadi ya wake na watoto ambao hawataki wajulikane? Je, wako tayari kutueleza jinsi viongozi wanavyothubutu kuchangia mahusiano bila aibu na baadhi yao kuhusishwa hadi katika uteuzi katika nafasi za chama na Serikali? Wanatutaka tuanze kuwataja hadharani?”, alihoji.

Akizungumzia kesi inayofunguliwa dhidi ya Dk. Slaa na Josephine, mwanamke aliyeibua mjadala, alisema kisheria hawezi kuzungumzia suala ambalo halijamfikia rasmi na kwamba anachoweza kuzungumza ni masuala ya kisiasa tu hadi hapo mawasiliano ya kisheria yakapomfikia.

Lakini habari zilizovuja kutoka CHADEMA zinasema Josephine mwenyewe anajiandaa kufungua kesi mahakamani kudai Sh bilioni mbili kwa kuchafuliwa jina na Lissu alikataa jana Jumanne kuzungumzia suala hilo kwa maelezo kwamba hana taarifa hizo.

Uchunguzi wa Raia Mwema wiki hii umebaini kuwapo kwa mijadala mizito miongoni mwa watu baadhi ikiwa katika mitandao kuhusiana na maisha binafsi ya viongozi wa juu wa CCM huku majina na picha za wahusika vikianikwa.

Maoni ya baadhi ya waliozungumza na Raia Mwema ni kwamba habari za mahusiano ya unyumba wa watu hazina tija wakati huu kwa vile kwa hakika hakuna atakayesalimika miongoni mwa viongozi wengi zikianza kutangazwa hadharani. Wanatoa mwito kwamba vyombo kama Tume ya Uchaguzi na Msajili wa Vyama viingilie kati kurejesha kampeni katika masuala ya msingi, yaani kero za kweli za Watanzania na Tanzania ijayo.

Akizungumzia hali hiyo, Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Rajabu Kiravu, alisema ofisi yake haiwezi kuchukua hatua wala kukemea hadi itakapopata malalamiko rasmi kutoka kwa vyama ama wagombea, na kwamba hakuna malalamiko yoyote yaliyokuwa yamewasilishwa kwake.

Kwa upande wake Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, alisema Baraza la Ushauri la Vyama vya Siasa, limetolea kauli suala hilo bila kufafanua.

Tendwa ambaye ni Katibu wa Baraza hilo, amenukuliwa akisema kwamba baraza hilo limekemea tabia ya baadhi ya vyama kuchafuana badala ya kutangaza sera za vyama husika.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Timu ya Kampeni ya CHADEMA, Profesa Mwesiga Baregu, ameliambia Raia Mwema kwamba mgombea wao (Dk. Slaa) anaendelea na kampeni bila kujali propaganda chafu zinazoenezwa na CCM dhidi yake.

“Sisi kwa upande wa mgombea wetu hana muda wa kampeni chafu na badala yake anaendelea kuchanja mbuga na kutangaza sera kwa wananchi na kuwalezea ufisadi wa CCM na Serikali yake na jinsi atakavyowashughulikia mafisadi atakapoingia madarakani,” alisema Profesa Baregu.

Profesa Baregu alisema chama cha siasa ama mgombea anayeanza kujadili mambo binafsi ya mshindani wake anakuwa amepoteza mwelekeo na kwamba ni dalili za kuishiwa kwa hoja.

Akitoa mifano ya Rais Mstaafu wa Marekani Bill Clinton na Rais wa sasa wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, Baregu amesema CCM wameishiwa hoja na kwamba wanazidi kusaidia kumuinua kisiasa Dk.Slaa badala ya kumharibia.

“Wanadhani wamchafua lakini kwa kweli wanatusaidia sana kumpigia kampeni. Mambo binafsi hayana nafasi katika siasa za sasa na muliona mfano wa Clinton na Lewinsky (Monica) na juzi juzi kule Afrika Kusini Zuma aliibuliwa kashfa ya ngono lakini matokeo yake ndiye Rais, na sisi tunaamini Dk. Slaa ndiye ataibuka mshindi,” alisema.

Tayari mtu anayejitambulisha kuwa mume wa ndoa wa Josephine, Aminiel Mahimbo, ameibuka na kulifikisha katika vyombo vya sheria suala hilo akidai fidia ya Sh bilioni moja.

Akizungumzia suala hilo na kunukuliwa na vyombo vya habari, Dk. Slaa alisema hana wasiwasi na kufunguliwa kesi na kutaka Mahimbo aulizwe wakati anaporwa mkewe yeye alikuwa wapi.

Dk. Slaa aliliambia gazeti moja la kila siku kwamba hizo ni kampeni chafu za kutaka kumharibia katika kipindi hiki na kwamba zinafanywa na CCM na kudai kuwa chama hicho kimemnunulia gari Mahimbo ili amchafue.

Tayari Dk. Slaa amekwisha kubainisha kwamba Josephine ndiye mke wake mtarajiwa baada ya kuishi na Rose Kamili na kuzaa naye watoto bila ndoa na kwamba hana tatizo naye, hali iliyojidhihirisha kwa wanawake wote wawili kupanda jukwani kumpigia kampeni.

Rose ambaye alikuwa Diwani wa CCM, amekihama chama hicho na kujiunga na CHADEMA ambako ameamua kugombea ubunge jimbo la Hanang kupitia chama hicho cha upinzani dhidi ya mgombea wa CCM, Dk. Mary Nagu.

Rose, mwanaharakati na mwanasiasa aliyeiongoza CCM katika Kata ya Basotu Hanang akiwa Diwani kwa miaka 16, ameelezwa kutoa upinzani mkali dhidi ya Dk. Nagu.

Rose alikaa jukwaa moja na Josephine katika kampeni za Dk. Slaa hadi mgombea huyo wa urais alipoondoka Hanang kwenda Mbulu kuendelea na kampeni.

Habari kutoka kwa watu walio karibu na Josephine wameliambia Raia Mwema kwamba mke huyo mtarajiwa wa Dk. Slaa amebeba siri nzito kuhusu vigogo wa CCM ambao wamekuwa wakifanya naye mawasiliano kadhaa katika siku za karibuni.

“Josephine ana siri nzito ambayo atalazimika kuianika hadharani kwa ushahidi pale itakapobidi na hapo hakutakuwa na wa kulaumiwa,” anasema kwa ufupi mtu huyo wa karibu na Josephine ambaye hakutaka kutajwa jina gazetini.

Suala la unyumba wa Dk. Slaa lilianza mara baada ya CHADEMA kuzindua kampeni zake katika viwanja vya Jangwani na kutaja viongozi wa CCM kuwa wanahusika na wizi wa fedha za EPA, kauli ambazo Katibu Mkuu wa CCM Yussuf Makamba alidai kwamba ni matusi dhidi ya viongozi wa chama chao. Makamba ndiye aliyeanza kwa kusema kwamba Dk. Slaa anasumbuliwa na ndoa yake kabla ya yeye kudaiwa kwamba alifukuzwa ualimu kwa aibu.

Chanzo: Raia Mwema

Wednesday, September 8, 2010

DR. SLAA AFUNGULIWA MASHTAKA MAHAKAMA KUU


MGOMBEA urais kwa tiketi ya CHADEMA, Dk. Willbrod Slaa (pichani), amefunguliwa kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaami, akidaiwa fidia y ash. bilioni moja kwa madai ya kunyang’anya mke wa mtu.

Kesi hiyo namba 122 ya mwaka 2010, ilifunguliwa jana mahakamani hapo na Aminiel Mahimbo kwa kupitia ofisi ya mawakili ya Amicus.

Mahimbo anadai kuwa, Dk. Slaa kamnyang’anya mkewe wa ndoa Josephine Mushumbusi.

Kwa kupitia nakala ya hati ya madai, Mahimbo anadai fidia ya sh. milioni 200 kutokana na hasara alizozipata baada ya mdaiwa huyo, kumtangaza mkewe wa ndoa Josephine kuwa mchumba wake na sh. milioni 800 ikiwa ni hasara ya jumla aliyopata.

Mlalamikaji huyo, anadai Septemba 7, 2002 alifunga ndoa na mwanamke huyo katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ushirika wa Kijitonyama na kuishi maeneo mbalimbali ikiwemo Kimara, Baruti, Dar es Salaam.

Pia anadai katika maisha yao ya ndoa wamebahatika kuwa na watoto wawili ambao ni Upendo aliyezaliwa Mei Mosi, 2003 na Precious aliyezaliwa Machi 14, 2007.

Mahimbo alidai, ndoa kati yake na Josephine haijavunjwa na chombo chochote na kwamba, bado ni mke wake halali.

Kwa mujibu wa hati hiyo, Mahimbo alidai hivi karibuni, mkewe alikuwa na safari za mara kwa mara na aliamini ni za kikazi. Josephine ni mfanyabiashara ambaye anaendesha kampuni iitwayo Green World Clinic.

Alidai katika tarehe na mahali tofauti, Dk. Slaa alimtambulisha mwanamke huyo kuwa ni mkewe, suala ambalo si kweli.

Mlalamikaji huyo alidai, uhusiano uliopo kati ya watu hao wawili umemfanya adhalilike na kunyanyasika katika jamii na anaiomba mahakama kumzuia Dk. Slaa kuendelea kujihusisha kimahusiano na mkewe.

Anaiomba mahakama kumwamuru Dk. Slaa kumlipa bilioni moja na kulipa gharama za kuendeshea kesi.

Mahimbo amedai ameambatanisha na cheti cha ndoa na Josephine, picha za harusi, vyeti vya kuzaliwa vya watoto na nakala za vipande vya magazeti zilizopigwa wakati Dk. Slaa akimtambulisha mwanamke huyo kuwa ni mkewe.

Monday, September 6, 2010

Takukuru yageuka `bubu` kwa vigogo waliohusishwa rushwa kura za maoni

Utata umetanda kuhusu hatima ya watuhumiwa wa kashfa za rushwa katika mchakato wa kura za maoni za Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Idadi kubwa ya watu wakiwemo viongozi wa serikali katika ngazi tofauti waliojitokeza kuomba ridhaa ya kuwania ubunge, walikamatwa ama kuhojiwa kutokana na rushwa.

Wagombea wa ubunge na udiwani kupitia chama hizo walishiriki kampeni zilizofanyika kati ya Julai 22 hadi 31, mwaka huu na kura zikapigwa Agosti Mosi, mwaka huu.

Wakati wa mchakato huo, makamanda wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) wa mikoa mbalimbali, walitoa taarifa za kukamatwa ama kuhojiwa kwa wana-CCM waliotuhumiwa kwa rushwa.

Miongoni mwa waliotajwa ni aliyewahi kushika nafasi ya uwaziri kwa nyakati tofauti, Joseph Mungai na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka (TFF), David Mwakalebela, ambao walifikishwa mahakamani.

Pia alikuwepo Katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM (Uvccm) mkoa wa Iringa, Fadhili Ngajilo, aliyefikishwa mahakamani kutokana na tuhuma za rushwa.

Mkoani Kilimanjaro, mkanganyiko umeibuka katika ofisi ya Takukuru, baada ya Kamanda wa taasisi hiyo aliyehamishiwa hapa hivi karibuni, kutoa taarifa tofauti na zile za awali kuhusu wagombea waliotuhumiwa kwa rushwa.

Kamanda wa Takukuru mkoani hapa, Laurance Swema, ambaye amehamishiwa mkoani alisema hana taarifa rasmi kuhusu kukamatwa kwa wagombea watatu wa nafasi za ubunge na udiwani, makada wa CCM na viongozi wengine wakati wa kura za maoni.

Alisema suala hilo analisikia na kulisoma kupitia vyombo vya habari, na kwamba hana taarifa za kiofisi.

Kamanda huyo aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati akiongea na NIPASHE kwa njia ya simu.

NIPASHE ilitaka kujua hatua zilizofikiwa ikiwemo kufikishwa mahakamani, dhidi ya watuhumiwa waliokamatwa na Takukuru wakati wa mchakato wa kura za maoni ndani ya CCM.

Alisema ana muda mfupi tangu ahamishiwe mkoani hapa akitokea Dar es Salaam, na kati ya mambo aliyokabidhiwa ofisini, hajaelezwa juu ya watuhumiwa wa rushwa wakati wa kura za maoni.

“Mimi ndio nimehamishiwa hapa kutokea Dar es Salaam na kwa sasa nipo likizo, nimekuja kuchukua familia yangu...sijasikia jambo hilo ofisini kwangu zaidi ya kusoma kwenye vyombo vya habari ambavyo mmeandika nyie,”alisema.

Hivi karibuni, aliyekuwa Kamanda wa Takukuru mkoani hapa na ambaye amehamishiwa mkoani Manyara, Alexanda Budigila, alikaririwa akisema kuwa bado wanaendelea na upelelezi wa matukio hayo.

Budigila alisema watuhumiwa waliokamatwa ama kuhojiwa watafikishwa mahakamani ikiwa uchunguzi utawezesha kupatikana kwa ushahidi.

“Bado tunaendelea na uchunguzi wetu, baada ya kukamilika watafikishwa mahakamani na kushtakiwa kwa mujibu wa sheria, siku tunayowapeleka mahakamani tutawajulisha wanahabari,”alisema.

Waliokamatwa wakidaiwa kutoa rushwa ni pamoja na aliyeibuka mshindi wa pili kwenye ubunge wa Viti Maalum mkoani hapa, Betty Machangu ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.

Wengine ni Katibu wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) mkoani hapa, Mariam Kaaya, Katibu wa UWT wilaya ya Moshi, Hadija Ramadhani,mfanyabiashara wa Moshi mjini, Hawa Sultani na dereva wa gari alilokuwa akilitumia mbunge huyo, SwaleheTwalibu.

Watuhumiwa hao walikamatwa katika nyumba ya kulala wageni ya Safari Resort, ambapo kwa mujibu wa Takukuru, walikuwa wakigawa rushwa ya fedha na vitu kwa wajumbe kwa kila mmoja kuingia ndani.

Tarifa zilidai kuwa mgombea huyo na wafuasi wake walikuwa wakigawa kati ya Sh 50,000 na 100,000, kanga, asali, vipeperushi na kadi za wajumbe wa Mkutano Mkuu wa UWT mkoa.

Hata hivyo, Mkuu huyo wa wilaya alikanusha madai ya kutoa rushwa na badala yake alisema walikwenda kwenye hoteli hiyo kwa ajili ya kupata chakula.

Machangu alidai kuwa walipokosa mahali pa kukaa, waliamua kuchukua chumba kimoja ili wakae kwa utulivu.

Akasema kuna dalili kwamba maadui zake wa kisiasa walihusika katika kutoa taarifa zilizosababisha kuzingirwa na maofisa wa Takukuru.

Pia Takukuru iliwakamata wagombea udiwani wa kata ya Shirimatunda, Elines Mwacha na watu saba kati ya 30 waliodaiwa kuwa mabalozi, wajumbe wa vijiji na makatibu wa CCM katika kata ya hiyo ambao wanadaiwa walikuwa wakila na kunywa na mgombea huyo.

Takukuru ilimkamata pia mgombea udiwani wa kata ya Majengo, Idd Juma, wakati akiwa na wanachama wa CCM na wenyeviti wa mitaa ya kata hiyo zaidi ya 15, katika baa ya Peters Club iliyopo eneo la Majengo kando kando mwa barabara kuu ya Moshi -Tanga.

Mkoani Arusha, Kamanda wa Takukuru mkoani hapa, Ayub Akida, amesema watuhumiwa waliokamatwa ama kuhojiwa kutokana na rushwa wakati wa kura za maoni, bado hawajafikishwa mahakamani.

Akihojiwa hivi karibuni, Akida, akasema uchunguzi bado unaendelea na kwamba utakapokamilika, atatoa maelezo kwa umma.

Waliokamatwa ama kuhojiwa kutokana na tuhuma za rushwa wakati wa kura za maoni mkoani Arusha, ni mbunge aliyemaliza muda wake Felix Mrema pamoja na wanachama 21 wa CCM.

Tukio hilo lilitokea usiku nyumbani kwa mwanachama mmoja eneo la Olamuriaki, kata ya Sombetini mjini hapa baada ya maofisa wa Takukuru kuivamia nyumba hiyo.

Watuhumiwa hao walihojiwa na Takukuru siku moja baadaye, kisha kuachiwa kwa dhamana.

Akizungumzia tukio hilo, Akida akasema walipata taarifa ya kuwepo kwa mkutano wa wanachama hao muda wa usiku na kwamba walikuwa wakiutilia shaka.

Alisema maafisa wake waliizingira nyumba hiyo na kufanikiwa kuwatia mbaroni ingawa wanachama wengine walikimbia.

Mkoani Dodoma, kukamatwa kwa mkazi mmoja wa wilaya ya Kondoa, Ibrahim Mfala akigawa fulana na kofia bure.

Naibu Kamanda wa Takukuru mkoani hapa, Sosteness Kibwengo, alikaririwa wakati wa mchakato akisema kuwa Ibrahim alikamatwa akigawa fulana hizo zilizokuwa na nembo ya CCM.

Aidha, Takukuru waliwakuta watu zaidi ya 40 ndani ya nyumba ya balozi eneo la Msalato lililopo halmashauri ya manispaa ya Dodoma Mjini wakidai kuwa wanamsubiri mgeni kutoka mjini.

Kamanda wa Takukuru mkoani hapa, Eunice Mmari, alikiri kupata taarifa za kuwepo kwa mpango wa mgombea mmoja wa ubunge jimbo la Dodoma Mjini, aliyeandaa Sh. 470,000 kwa ajili ya kuwagawia wanachama 47 wa mtaa wa Nduka uliopo kata ya Chamwino.

Alipoandikiwa ujumbe mfupi wa maneno ukitaka aelezee wamefikia wapi kuhusiana na uchunguzi huo, ujumbe ulionyesha kupokelewa lakini haukujibiwa.

Alipoulizwa Afisa Uhusiano wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Doreen Kapwani, juu ya uchunguzi wa tuhuma za wagombea wanaodaiwa kutumia rushwa wakati wa kura za maoni za CCM, alisema kwa mujibu wa sheria ya taasisi hiyo, hawaruhusiwi kuzungumzia mwenendo wa uchunguzi unaofanywa na taasisi hiyo kabla ya suala husika kufikishwa mahakamani.

Habari hii imeandikwa na waandishi wetu kutoka Kilimanjaro, Dodoma na Arusha.

CHANZO: NIPASHE

Friday, September 3, 2010

Jino kwa jino CUF, CCM na CHADEMA

-Makamba aambiwa hajui maana ya matusi
-Kashfa ya EPA bado mwiba kwa CCM
WAKATI vumbi la kampeni likiendelea kutimka, Chama Cha Wananchi (CUF) kimelalamikia mwenendo wa kampeni wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM), malalamiko yanayohusisha kauli za vyama hivyo na matumizi ya fedha.

Mbali na malalamiko hayo, Mgombea Mwenza wa CUF, Juma Duni Haji, amedai kukutana na vituko alivyoviita vya Serikali ya Rais Jakaya Kikwete.

Kwa mujibu wa Duni Haji, vituko hivyo ni pamoja na kukuta shule yenye Mwalimu mmoja ambaye ndiye Mwalimu Mkuu na alipomuuliza kwa nini anajiita Mwalimu Mkuu, aliambulia kicheko kutoka kwa mwalimu huyo.

Akizungumza na Raia Mwema kwa simu kutoka mkoani Kagera, Msemaji wa Kampeni za CUF, Mbarara Maharagande, alishangazwa na ujasiri wa CCM kutumia mabilioni ya fedha kiasi cha kupindukia kwenye kampeni zake, wakati huduma za jamii zikizidi kuwa duni kwenye maeneo wanakojinadi.

“Athari kubwa ambayo inatukabili ni matumizi makubwa ya fedha kwa upande wa CCM, tupo njiani kuelekea Bukoba Vijijini ni dhahiri fedha nyingi zimetumika na hii ni njia mojawapo ya kukandamiza demokrasia,”

Alipoulizwa kwamba matumizi ya fedha hizo inawezekana ikawa kwa mujibu wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi inayotaja kiwango hadi Sh bilioni 50, Maharagande alisema kwa vyovyote vile na hasa kwa kuzingatia mazingira ya Tanzania, demokrasia inaathirika.

“Wamesambaza mabango kila kona, fulana zitagawiwa karibu kwa kila Mtanzania…najiuliza inakuwaje mabilioni yamwagwe kiasi hicho wakati huduma za jamii kule wanakoenda kuomba kura zikiwa zimezorota. Dawa hospitalini hakuna hata karatasi za kuandika taarifa za wagonjwa lakini karatasi za kampeni zimesambazwa hadi vyooni,” alisema Maharagande na kuongeza kuwa wana matarajio makubwa kwamba Profesa Ibrahim Lipumba mgombea urais kwa tiketi ya CUF atashinda na kuunda serikali licha ya matumizi hayo makubwa ya fedha kwa upande wa CCM.

Katika hatua nyingine, Maharagande alikilalamikia CHADEMA akisema kimekuwa kikitumia lugha za kashfa dhidi ya wagombea wengine bila kujali ni wa CUF au chama kingine.

Alibainisha kuwa kitendo cha mgombea urais wa CHADEMA, Dk. Wilibrod Slaa kuzungumzia posho, mishahara na mafao ya wabunge kuwa ni makubwa na kutumia ajenda hiyo kwenye kampeni ni usaliti.

Alisema Dk. Slaa ni sehemu ya viongozi waliopitisha mafao hayo kwa kuwa alikuwa Naibu Kiongozi wa Upinzani pamoja na Mbunge wa CUF, Hamad Rashid Mohamed na kwamba Dk. Slaa mwenyewe alichukua mafao na mishahara hiyo ya wabunge anayodai ni mikubwa.

Mbali na kulalamikia hoja hiyo ambayo inaelekea kukikera CUF, Maharagande alisema CHADEMA pia imejihusisha na vitendo vya vurugu dhidi ya chama chake.

“CHADEMA walimshambulia mgombea wetu wa ubunge Tarime (Charles Mwera) na hivi karibuni wametoa lugha za kashfa kwa wagombea wa chama kingine….huu si ustaarabu, tunawashauri waache mwenendo huo,”

Alipoulizwa ni kwa nini ameanza kuwa na mwelekeo wa kutetea wagombea wa CCM ambao hivi karibuni ndio waliodaiwa kushambuliwa na viongozi wa CHADEMA, alisema CUF ina haki ya kutoa msimamo wake kuhusu masuala ya msingi yanayoweza kuathiri mwenendo wa nchi.

Malalamiko dhidi ya CHADEMA yamekwishatolewa na CCM, kupitia mwenyekiti wa kampeni za chama hicho, Abdulraham Kinana, akidai kusikitishwa na maelezo ya wakili mwandamizi nchini, Mabere Marando aliyesema Mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete, Rostam Azizi na Edward Lowassa wanahusika kwenye wizi wa mabilioni ya fedha kutoka Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) Benki Kuu ya Tanzania.

Katika mazungumzo yake na Raia Mwema Jumanne wiki hii, Kinana alishauri CHADEMA watumie hoja kushawishi wapiga kura na si kuzusha kashfa, kuhangaika kuweka pingamizi au kukimbilia mikutano na waandishi wa habari, akisisitiza ni muhimu kukimbilia kujinadi kwa wapiga kura ili kueleweka na kuchaguliwa.

“Siku hizi za awali kwa mujibu wa kampeni zetu kuna kila dalili za ushindi mkubwa kwa sababu tunaeleza tulichofanikiwa kufanya na tutakachofanya tukiendelea kuchaguliwa, wananchi wanatuelewa vizuri,”

“Hali hiyo ni tofauti na wenzetu ambao wanaendeleza yale ya miaka 15 iliyopita ya kufanya kampeni za kuzua kashfa, waeleze watafanya nini,” alisema Kinana.

Katika hatua nyingine, Mgombea Mwenza wa CUF Juma Duni Haji alilieleza gazeti hili kwamba Watanzania waelewe kuwa hata wakiipa CCM miaka mingine 100 ya kutawala hawataweza kuwa na maisha bora.

“Kuna silaha mbili zinazotumiwa na CCM kushinda. Kwanza, masikini na mtu mjinga ndiye anayetawalika. Pili, tajiri hawezi kutawalika. Kwa hiyo wanatambua hizi silaa na wanahakikisha watu wanabaki kuwa masikini na wajinga ili waendelee kutawala.

“Tumefika kwenye shule moja tumekuta ina wanafunzi 900 lakini walimu wanne, kwenye shule nyingine mwalimu mmoja huyo huyo amejiita Mwalimu Mkuu, ukimuuliza kwa nini ajipe cheo hicho anacheka tu,” alisema Duni.

Wakati huo huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kampeni za CHADEMA, Profesa Mwesiga Baregu, amemjibu Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba na Kinana, akisema kwamba hakuna kiongozi wala mgombea wa chama chao aliyetoa matusi ama kufanya vurugu bali kinachotokea ni CCM kutapatapa.

Akizungumza na Raia Mwema kwa njia ya simu jana, Profesa Baregu amesema anashangazwa na kauli kwamba CHADEMA imetoa matusi na kufanya vurugu katika kampeni zake za hivi karibuni.

“Tangu tulipokuwa kwenye mkutano wa kuzindua kampeni, hakuna mzungumzaji aliyetoa matusi ama kufanya vurugu. Wanashindwa (CCM) kutenganisha kati ya matusi na kusema ukweli, maana kilichozungumzwa ni kwamba kesi za EPA zilizopo mahakamani hazitoshi na waliohusika moja kwa moja hawajaonekana na wakatajwa. Hakuna matusi hapo,” alisema Baregu.

Baregu alizungumzia pia kuhusu kauli ya Makamba kudai kwamba Mgombea Urais wa CHADEMA, Dk. Wilbroad Slaa haaminiki akisema kwamba hayo maneno hayo ni dalili ya kutapatapa.

“Kuna mazungumzo mengine kama ya Makamba anaposema Dk.Slaa haaminiki na kwamba kaasi dini na kaasi mke wake. Hayo sijui ana uhakika gani? Slaa hana ugomvi na Kanisa Katoliki na ndiyo maana alihusika kupanga safari ya Papa (John Paul II) alipokuja Tanzania.

“Hapa ukweli ni kwamba alishindwa taratibu za upadri na ni uaminifu si ukosefu wa uaminifu ndiyo maana aliomba ruhusa ya Kanisa Roma na akakubaliwa, kusema ukweli ndiyo uaminifu na ndiyo maana alikubalika. Anataka awe mnafiki aende kanisani mchana halafu usiku aende mtaani kubangaiza,” alisema Baregu.

Thursday, September 2, 2010

UNIFEM KUWAPATIA WAGOMBEA WANAWAKE MBINU ZA KUSHINDA UCHAGUZI


NA MWANDISHI MAALUM-NEW YORK

Wakati kampeni za kuwania nafasi za urais, ubunge na udiwani zikiwa zinaendelea kushika kasi nchini Tanzania. Mfuko wa Umoja wa Mataifa kwaajili ya Maendeleo ya Wanawake (UNIFEM), umetangaza kuendesha mafunzo ya uwezeshaji kwa wanawake waliojitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi Octoba.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Naibu Mkurugenzi wa UNIFEM kwaajili ya maendeleo ya Kikanda Afrika ya Mashariki na Pembe ya Afrika, Ni Sha. Inaeleza kuwa, mafunzo hayo yatakayoendeshwa katika kanda saba za uchaguzi yatafanyika mwezi huu wa septemba,lengo likiwa ni kuwajengea uwezo na kuwapa wanawake mbinu na mikakati ya kushinda uchaguzi.

“ Mafunzo haya yanalenga kuwawezesha wanawake wanaowania nafasi za uongozi na uwakilishi katika uchaguzi mkuu utakaofanyika nchini Tanzania mwezi octoba, kuboresha mbinu za uzungumzaji katika mikutano ya hadhara, namna bora ya kushirikiana na kuwasiliana na vyombo vya habari, uratibu wa kampeni zao, namna ya kujieleza, uhamasishaji wa jamii na mbinu za ushawishi” anafafanua Ni Sha katika taarifa yake kwa vyombo vya habari.

Wagombea hao wanawake pia watajifunza kuhusu nafasi ya mwanamke katika siasa za Tanzania, masuala mbalimbali ya kisiasa yanayohusiana na uchaguzi wa mwaka huu, majumu ya Bunge , Baraza la Wawakilishi , Halmashauri, Sheria na Taratibu mbalimbali zinazohusu uchaguzi.

Taarifa hiyo ya UNIFEM, inabainisha pia kwamba, pamoja na Katiba ya Tanzania kutenga asilimia 30 ya viti vya ubunge kwaajili ya wanawake, katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, ni wanaweke 17 waliojitokeza kuwania nafasi za ubunge kati ya wagombea 232.

UNIFEM imekwisha kuwapatia mafunzo wakufunzi 30 watakao endesha mafunzo hayo, ambayo mbinu zake za ufundishaji tayari zimekwisha kufanyiwa majaribio na kukubalika. Mafunzo ya wakufunzi hayo yalifanyika jijini Dar es Salaam kati ya tarehe 12 na 14 mwezi wa uliopita (wa Nane).

Katika hatua nyingine, UNIFEM kwa kushirikiana na UNESCO katika mwezi huu wa tisa pia itatoa mafunzo kwa waratibu wa vituo vya radio za jamii katika miji ya Arusha, Unguja na Pemba kwa lengo la kutoa ufahamu na uelewa kuhusu taarifa za wagombea wanawake katika maneo yao. Waandishi pia watafundishwa mbinu za kuandika habari zenye kutoa nafasi sawa na haki kwa wagombea wanawake.