Monday, April 19, 2010

Wadau wauchambua muswada wa Sheria mpya ya Madini

MUSWADA wa Sheria ya Madini wa mwaka 2010 ambao kwa mujibu wa ratiba ya mkutano wa 19 wa Bunge unatarajiwa kuwasilishwa leo, jana ulichambuliwa vikali na wadau wa sekta ya madini akiwemo Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira.

Wazungumzaji wengi akiwemo Waziri Wasira wamesema muswada huo haujali wachimbaji wadogo wala kutetea maslahi ya Taifa.

“Nchi inapata nini na wananchi watapata nini?” Alihoji Waziri Wasira na kuongeza kuwa lazima sheria iamue kwa makusudi kabisa kusaidia wachimbaji wadogo ambao ndio msingi mkubwa wa maendeleo ya sekta ya madini kwa siku za usoni.

Waziri huyo ambaye alisema wazi, alizungumza kama mdau wa madini akiwa hana elimu ya sheria, alisema suala la madini ni suala nyeti nchini na kwa hali yoyote sheria inayotarajiwa kutoa mwongozo wa madini, lazima ijibu hoja muhimu za manufaa kwa Taifa na wananchi.

“Je haiwezekani kuwawezesha watu maskini, wawekezaji wa ndani?” Aliuliza Waziri Wasira ambaye alisema kwamba ni kuwawezesha wawekezaji wa ndani ni muhimu huku akitoa mfano wa Sweden ambayo alisema uchumi wake unaotegemea madini kwa kuwezesha wachimbaji wake wadogo wazawa.

Alisema alipokuwa katika mkutano wa Davos nchini Switzerland, Februari mwaka huu, alifanya mazungumzo na Waziri wa Madini wa Sweden ambaye hakumtaja jina lakini akasema Waziri huyo alimweleza wazi kwamba ni lazima kuweka mizania na kusaidia wawekezaji wadogo au la sivyo Taifa linaweza kubakia na mashimo kama litategemea wachimbaji kutoka nje.

Waziri Wasira alisema wazi kuwa sheria lazima ijibu hoja za sera, na ilani ya uchaguzi ambapo inategemewa na wachimbaji wadogo kuendelezwa na kuwa msingi wa uchumi hali ambayo kwa sasa sheria hiyo haina.

Soma zaidi

No comments: