Wednesday, April 21, 2010

Wabunge wazidi kumbana Magufuli

Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. John Magufuli, ameendelea kubanwa na wabunge wanaotaka baadhi ya vipengele kikiwemo cha usajili wa mifugo kiondolewe katika muswada ya Sheria ya Utambuzi, Usajili na Ufuatiliaji wa Mifugo.

Dk. Magufuli aliamua kuutoa muswada huo na ule wa Maeneo ya Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo za mwaka 2010 bungeni na kuurudisha tena katika Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji baada ya wabunge wengi kuipinga Alhamis iliyopita.

Alipourejesha tena katika kamati hiyo, wabunge walipata nafasi nyingine ya kuujadili baada ya wizara hiyo kuufanyia marekebisho lakini bila muafaka.

Katika kikao hicho kilichomalizika juzi usiku, Mbunge wa Simanjiro(CCM), Christopher Ole Sendeka, alisema wameshindwa kuelewana na Dk. Magufuli kwa sababu hakutaka kutambua maeneo waliyotaka yafanyiwe marekebisho.

Aliiomba kamati huyo ambayo ilitegemea kuketi jana, kuangalia na kutafakari kuacha kukubali wazo la kuurejesha tena bungeni.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Ileje (CCM), Gedion Cheyo, alisema kamati yake itajadili na kutoa maamuzi kwa manufaa ya taifa yatakayoboresha huduma katika sekta hiyo.

Akizungumza awali kabla ya kuanza kwa kikao hicho, Dk. Magufuli alisema kipengele cha usajili wa mifugo kimeongezewa muda kutoka siku saba hadi siku 30. Alisema pia mfugaji halazimiki kwenda kusajili mwendo mrefu bali shughuli za usajili zitafanyika vijijini hata kama ni anapokwenda kuogesha mifugo yake. Awali, akichangia katika kikao hicho, Ole Sendeka, alitaka sheria hiyo kurudishwa kwa wadau kwa kuwa wafugaji wengine hawakushirikishwa katika majadiliano ya kutengeneza miswaada hiyo.

Mbunge wa Njombe Kaskazini (CCM), Jackson Makwetta, alisema sheria hizo zina mapungufu makubwa na kwamba hazitasaidia taifa kwenda mbele. Mbunge wa Kiteto (CCM), Benedict Ole Nangoro, alisema changamoto katika sekta hiyo zipo nyingi ambazo zinatakiwa kutatuliwa ili kuwezesha taifa kwenda mbele.

Mbunge wa Kalambo (CCM), Ludovick Mwananzila, alishauri kuwepo kwa benki maalum na utaratibu wa kuweka bima kwa wakulima na wafugaji ili panapotokea tatizo la kufa kwa wanyama waweze kupata mtaji wa kuanzia. Mbunge wa Rufiji (CCM), Profesa Athuman Mtulya, alisema ufugaji wa kuhamahama ni haramu na unaweza kujenga jangwa na kutaka kutengwa maeneo maalum.

Mbunge wa Bukombe (CCM), Emmanuel Luhahula, alisema maeneo mengi ya vijiji yamejaa na kuitaka serikali kutotumia sheria ya vijiji kugawa maeneo badala yake igawe yenyewe.

No comments: