Thursday, April 8, 2010

Tamasha la Nyerere kuanza Jumatatu

MTOTO wa aliyekuwa Rais wa kwanza wa Ghana Dk Kwame Nkurumah, Samia, anatarajia kuwa mgeni rasmi katika Tamasha la pili la ‘Kigoda cha Taaluma ya Mwalimu Nyerere’ litakaloanza Jumatatu ijayo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM).

Profesa wa ‘Kigoda cha Taaluma ya Mwalimu Nyerere' katika Chuo Kikuu hicho, Issa Shivji amewaeleza waandishi wa habari leo kuwa, tamasha hilo litakwisha Aprili 15.

Profesa Shivji amesema, wameandaa tamasha hilo kwa mara ya pili kwa kuwa walipata mafanikio katika tamasha la kwanza lililokuwa na kauli mbiu isemayo Binadamu Wote ni Sawa na Afrika ni sawasawa.

Tamasha hilo lilifanyika kuanzia Aprili 13, likaisha Aprili 17 mwaka jana.

Profesa Shivji amesema, kauli mbiu ya mwaka jana ilileta mtazamo ambao bado ni thabiti katika mapambano ya kukamilisha uhuru na ukombozi wa watanzania dhidi ya ukandamizaji na unyonyaji wa mfumo wa kibeberu.

Amesema, mada kuu ya mwaka huu itakuwa ni Azimio la Arusha na kwamba, wamechagua mada hiyo ili kuenzi fikra na falsafa ya Mwalimu Julius Nyerere kwa kuwa ni kielelezo cha historia ya ukombozi nchini.

Kwa mujibu wa Shivji, tamasha hilo litawahusisha watafiti wa masuala mbalimbali ya kijamii watakaowasilisha utafiti wao na kuyawasilisha mapendekezo serikalini ili kuleta mfumo unaohitajika katika nchi nyingi.

“Katika miongo miwili iliyopita Azimio la Arusha limesahaulika na kugeuzwa kama ni tukio la kihistoria lisilokuwa na umuhimu katika zama hizi za utandawazi, sasa ni juu ya kizazi hiki kipya kama Azimio lingali hai au la?” amesema. Azimio la Arusha lilianzishwa mwaka 1967.

No comments: