Thursday, April 22, 2010

Wadau wadai mshahara mpya ni mzigo

INGAWA Serikali imeonesha kuwa sikivu na kusikiliza kilio cha wafanyakazi na kuamua kuongeza kima cha chini cha mishahara kwa sekta binafsi, wadau wa sekta hiyo wanasita kuikubali.

Hali hiyo inatokana na kinachoelezwa kuwa fedha hizo ni nyingi na ni vigumu kwa waajiri wengi wa sekta hiyo kulipa mishahara hiyo mipya kutokana na gharama za uendeshaji kupanda.

Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) imesema utekelezaji katika kulipa mishahara mipya kwa asilimia 100 kama ilivyotangazwa na Serikali utakuwa mgumu na huenda ukaua viwanda nchini.

Aidha, matokeo yake yanaweza kusababisha watu kupunguzwa ajira kutokana na uchanga wa sekta hiyo kwa kuwa gharama za uendeshaji zitapanda.

Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Dk. Evance Rweikiza, alisema hayo jana Dar es Salaam wakati akizungumza na gazeti hili, alipotakiwa kutoa maoni ya sekta hiyo juu ya kupanda kwa mishahara kama ilivyotangazwa juzi na Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya.

Waziri Kapuya alitangaza nyongeza hiyo alipozungumzia hatua iliyofikiwa na Serikali baada ya kumalizika kwa mazungumzo ya Shirikisho la Chama cha Wafanyakazi (TUCTA), Baraza la Ushauri la Uchumi na Jamii (LESCO) na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) kuhusu madai ya wafanyakazi.

Profesa Kapuya alisema kiwango hicho kitaanza kulipwa wakati wowote kuanzia sasa na kwa upande wa wafanyakazi wa Serikali walitakiwa kuvuta subira kwa kuwa mchakato unaendelea serikalini na Aprili 25 mwaka huu, wadau watakutana kwa maafikiano zaidi.

Dk. Rweikiza alisema baada ya kupata taarifa hizo katika vyombo vya habari, TPSF inajipanga kuwasiliana na wafanyabiashara ili kutoa tamko, ingawa inatambua kuwa kulipa mishahara mizuri ni jukumu lao, ili wafanyakazi waweze kuwa na tija, ila gharama za uendeshaji ni tatizo kwa sekta hiyo.

“Sekta binafsi ni changa, haina fedha na pia gharama za uendeshaji ni kubwa, hata Serikali yenyewe haiwezi kupandisha mishahara yake kwa asilimia 100,” alisema Dk. Rweikiza.

Alisema suala la kupatikana kwa umeme wa uhakika nchini ni tatizo, kodi ni kubwa na hata mazingira ya biashara nayo ni magumu na kutekelezwa kwa mshahara huo ni sawa na kuua viwanda na kuzalisha kundi lingine lisilokuwa na ajira kutokana na wengi kukumbwa kupunguzwa kazi.

Alisema kabla Waziri Kapuya hajatangaza nyongeza hiyo, alitakiwa kukutana na wahusika kujadiliana wafikie muafaka, ili isije kuzaa mgongano kama ilivyokuwa nyongeza ya mshahara ya mwaka 2007.

“Katika hili busara zaidi zitawale, hatua hii inaweza kuzalisha mgogoro kati ya waajiri na wafanyakazi, ni vyema wakutanishwe na ngazi husika kabla ya kutangazwa,” alisema Dk. Rweikiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Dk. Aggrey Mlimuka, alisema hajauona waraka wa Waziri unaotangaza mishahara hiyo, hivyo hawezi kutoa maoni yoyote na ieleweke kuwa kila jambo lina utaratibu wake.

Alisema upo utaratibu wa kuongeza mishahara hata kama ni katika kima cha chini, ambapo hata Notisi ya Serikali (GN) bado haijatoka.

“Mimi nimeisoma taarifa hiyo kwenye magazeti, siwezi kutamka lolote, kwanza suala la kupandisha mishahara lina utaratibu wake unaopaswa kufuatwa,” alisema Dk. Mlimuka.

1 comment:

Njonjo OK said...

I am doing research on blogs and I would like to send u few questions. Can u help? If you are willing please send me your email, mine is "njonjo.kweja@gmail.com" I am njonjo mfaume, of University of Dar es Salaam, School of Journalism.