Tuesday, April 20, 2010

Wabunge wakosa imani na Kenya, Uganda

WABUNGE wametaka raia wa Kenya na Uganda walioajiriwa katika sekta mbalimbali nchini, kabla ya kuanza kwa Itifaki ya Soko la Pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki, warudishwe makwao.

Pia wameitaka serikali kuhakikisha inawanyang’anya ardhi raia wa nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki walionunua ardhi nchini na irudishwe mikononi mwa Watanzania.

Wakijadili azimio la Itifaki ya Soko la Pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyowasilishwa na Waziri Dk. Diodorus Kamala, wabunge hao walisema haiwezekani raia hao wa nchi nyingine wajazane kwenye ajira za nchini wakati kuna Watanzania wengi hawana ajira.

Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela (CCM) ametaka kufanyike kwa sensa katika hoteli na sekta nyingine kubaini raia wa Kenya na Uganda wanaofanya kazi nchini na warudishwe makwao kusubiri kuanza utekelezaji wa Itifaki hiyo.

“Tunao vijana wengi tu hapa nchini wamesoma vizuri na wanaongea Kiingereza vizuri, lakini ukienda kwenye mahoteli waliojazana ni Wakenya, hawa naomba warudishwe makwao wasubiri mpira uanze tucheze sawa,” alisema mbunge huyo.

Kwa upande wa ardhi, alisema serikali ifanye utafiti kubaini raia wa kigeni hasa wanaotoka kwenye nchi za Rwanda, Burundi, Kenya na Uganda walionunua ardhi katika mikoa ya mipakani wanyang’anywe ardhi hiyo.

“Ardhi ya nchi ndio mali yetu, wenzetu hawa wana matatizo ya ardhi, serikali itambue ardhi hii ni kwa ajili ya Watanzania, hivyo serikali ikafanye tafiti mipakani na kama kuna ardhi imeshanunuliwa kinyemela na wenzetu hawa irudishwe,” alisema.

Mbunge wa Masasi, Raynald Mrope (CCM), aliishambulia Kenya kuwa ndio chanzo cha kuvunjika kwa jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki mwaka 1977 na akaonya kuwa vitendo vya Wakenya vinatishia uhai wa jumuiya ya sasa hasa vya kuibia rasilimali Tanzania kama madini ya tanzanite.

Alisema Serikali ya Kenya inawatia kiburi raia wao kuendelea kuibia Tanzania hivyo akaitaka serikali iwakemee haraka likiwemo hili suala la kupinga Tanzania kuuza meno ya tembo katika mkutano wa Cites huko Doha nchini Qatar.

Mbunge wa Makete, Dk. Binilith Mahenge alisema Tanzania sasa hivi inazalisha wasomi wengi kila mwaka na isipokuwa makini katika utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja, vijana wengi wanaweza kujikuta hawana ajira.

Alitaka vyuo vikuu vinavyotoa elimu kuhakikisha vinawapa mafunzo na ujuzi vijana hao ili wamudu ushindani katika soko hilo. Pia aliwataka wajasiriamali kuzalisha bidhaa bora ambazo zitakubalika katika nchi zingine za jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM), alisema kama ajira wataachiwa wageni hao kuingia holela, vijana wa Kitanzania wataenda wapi. Alitaka serikali ihakikishe kwenye sekta ya utalii inawapunguza raia hao wa Kenya ili Watanzania nao wapate ajira hizo.

Lakini alionya kuwa katika utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja, Wakenya wamejiandaa kujenga hoteli za nyota nne hadi tano katika sehemu mbalimbali nchini, hali itakayowezesha kumiliki uchumi katika maeneo hayo.

Soma zaidi

No comments: