Wednesday, March 31, 2010

Wataka bajeti ya matatizo ya wanawake iongezwe

WANAWAKE 500 wanakufa nchini Tanzania kila mwaka, kutokana na matatizo ya ujauzito na mengineyo ya wakati wa kujifungua; na serikali imeombwa kupunguza haraka matatizo hayo.

Hayo yalisemwa na Mjumbe wa Bodi ya Ushauri ya Taasisi ya Utu Mwanamke, Abubakar Karsan, kwenye mkutano ulioandaliwa na taasisi hiyo kwa waandishi, jijini Dar es Salaam jana.

Pia, Karsan alisema kwamba bajeti inayotengwa, kwa ajili ya kupambana na matatizo ya wanawake ni ndogo, hivyo inatakiwa iongezwe.

Alisema katika maeneo mengine wajawazito wanapofika hospitalini, hulipishwa katika baadhi ya huduma, ambazo wanatakiwa kupewa bure: Alitolea mfano wa huduma ya kuwekewa mashuka safi vitandani, kuongezewa damu, kupigwa sindano za kupunguza maumivu au kuwekewa ‘dripu’.

Karsan alitaka waandishi kuongeza kasi ya kuripoti masuala ya afya ya uzazi na fistula katika magazeti, redio na televisheni, ili kuongeza uelewa wa wananchi ; na pia kuifanya serikali itekeleze mipango yake ya muda mfupi na mrefu ya kuboresha afya ya wanawake.

Mgeni rasmi katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Utu Mwanamke, Christine Matovu, alisema taasisi hiyo imepania kushirikiana na wadau wengine, mfano vyombo vya habari, kuhimiza uboreshaji wa afya ya uzazi na upunguzaji wa vifo vya wajawazito nchini.

Kuna vikwazo vingi vinavyochangia mjamzito kupoteza maisha wakati wa kujifungua, kama vile umbali wa kufikia huduma za dharura za uzazi, ukosefu wa fedha za maandalizi ngazi ya familia, ukosefu wa usafiri, huduma isiyo bora kwa mjamzito na ukosefu wa watumishi wenye ujuzi kwenye vituo vya kutolea huduma.

No comments: