Monday, March 1, 2010

Kikwete: Kununua uongozi sasa basi

RAIS Jakaya Kikwete, amesema Sheria ya Gharama za Uchaguzi ambayo atasaini muswada wake karibuni ili ianze kazi, ikitekelezwa ipasavyo itazuia kugeuza uongozi kuwa kitu cha kununuliwa kama bidhaa na wenye fedha.

Akihutubia Taifa jana katika hotuba yake ya mwisho ya mwezi, Rais Kikwete alisema chimbuko la kutungwa sheria hiyo ni mwenendo usioridhisha wa matumizi ya fedha katika uchaguzi nchini.

“Kuna matumizi mabaya ya fedha katika uchaguzi ndani ya vyama vya siasa na baina ya vyama vya siasa katika chaguzi za kiserikali,” alisema Rais Kikwete aliyetumia hotuba yake hiyo kuzungumzia Muswada huo wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi uliopitishwa na Bunge katika Mkutano wake wa 18 mwezi uliopita mjini Dodoma.

Aidha, amesema itakomesha kabisa tabia mbaya inayoanza kujitokeza ya wapiga kura kugeuza kura yao kama bidhaa ya kuuza kwa wagombea.

“Hivi sasa kwa sababu ya kutokuwepo ukomo, wako watu wenye pesa ambao wanafanya matumizi kupita kiasi. Wapo wanaopitiliza au hata kukufuru na kuwadhalilisha wenzi wao wasiokuwa na uwezo kama wao,” alieleza Rais Kikwete.

Wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Takukuru mjini Mwanza wiki iliyopita alisema atasaini muswada huo kuwa sheria kwa mbwembwe ili kuwabana wanaotumia fedha kupata uongozi.

Alisema sheria hiyo mpya imetungwa kwa nia ya kupata majawabu kwa tatizo la matumizi mabaya ya fedha katika shughuli za uchaguzi.

“Tunatambua kuwa matatizo haya si mageni, yamekuwepo tangu miaka mingi huko nyuma na hata historia ya Bunge letu ina ushahidi wa ushindi wa baadhi ya wabunge kutenguliwa kwa makosa ya rushwa.

“Lakini, siku hizi matatizo ya matumizi mabaya ya fedha yamekuwa makubwa zaidi na yanakua kwa kasi inayotishia kugeuzwa kuwa ndiyo utaratibu wa kawaida au utamaduni katika chaguzi zetu,” alisema na kuongeza:

“Ni hali ambayo haifai kuachwa kuendelea na kuzoeleka. Hatuna budi kuchukua hatua za dhati kurekebisha mambo na kulirejesha taifa katika mstari ulionyooka.”

Alisema serikali iliamua kuwa hatua muafaka ya kuchukua ni kutunga sheria ya kuongoza na kudhibiti matumizi katika uchaguzi.

“Sheria hii ikitekelezwa ipasavyo itazuia kugeuza uongozi kuwa ni kitu cha kununuliwa kama bidhaa na wenye pesa au wanaoweza kupata pesa za kufanya hivyo. Aidha, itakomesha kabisa tabia mbaya inayoanza kujitokeza ya wapiga kura kugeuza kura yao kama bidhaa ya kuchuuza kwa wagombea,” alieleza Rais Kikwete. Alisema ametumia muda mwingi katika hotuba yake kuelezea mambo ya msingi yaliyomo katika sheria hiyo, akilenga mambo matatu muhimu.

“Kwanza, kuwathibitishia Watanzania wenzangu kwamba tunalitambua tatizo la rushwa katika uchaguzi na tunayo dhamira ya dhati ya kupambana nalo. Kukemea peke yake hakutoshi, lazima tutumie nguvu ya sheria kudhibiti vitendo vya rushwa na kuwaadhibu ipasavyo wahusika,” alisema Rais Kikwete.

Soma zaidi

No comments: