Tuesday, March 16, 2010

Hatma ya Liyumba kortini Aprili 9

UPANDE wa mashitaka katika kesi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba, umefunga ushahidi wake na kuiachia Mahakama kuamua kama mshitakiwa ana kesi ya kujibu au la.

Mahakimu wanaosikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Edson Mkasimongwa, Lameck Mlacha na Benedict Mwingwa, wamepanga kutoa uamuzi wa kama mshitakiwa ana kesi ya kujibu au la Aprili 9 mwaka huu.

Mara ya mwisho upande huo uliodai kuwa utakuwa na mashahidi wawili wa mwisho huku mmoja wao akiwa nje ya nchi, jana uliiambia mahakama kuwa umefikia uamuzi wa kufunga ushahidi ili kesi iendelee, ombi ambalo lilikubaliwa na Mahakama.

Mwendesha Mashitaka Juma Ramadhan alidai “shauri lilipangwa kuendelea kusikilizwa, lakini baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi wanane wa upande wetu na vielelezo 13, tumefikia uamuzi wa kufunga ushahidi na kuiacha kesi iendelee kwa mujibu wa sheria.”

Wakili wa Liyumba, Majura Magafu, aliiomba Mahakama kufanya majumuisho wakati huo, kwa kuwa kwa upande wa utetezi ulikuwa tayari umepinga ombi la Jamhuri kwa maelezo kwamba ni vema majumuisho yapangiwe siku nyingine, ili yatolewe ili kuwe na rekodi nzuri ya mahakama.

Mahakama ilikubaliana na upande wa Jamhuri na kupanga kupokea majumuisho ya upande wa utetezi Machi 22 mwaka huu na upande wa Jamhuri uwasilishe Machi 29 mwaka huu.
Liyumba anatuhumiwa kutumia vibaya madaraka na kuisababisha Serikali hasara ya Sh bilioni 200 kwa kufanya mabadiliko katika mradi wa ujenzi wa majengo pacha ya BoT.

Shahidi wa saba wa Serikali, Harold Herbert Webb, aliyekuwa na jukumu la kukadiria gharama za ujenzi katika mradi huo kupitia kampuni yake ya Webb and Uronu, alidai mahakamani katika mabadiliko hayo fedha zote zilitumika.

Hata hivyo, alidai taarifa kamili juu ya gharama za mradi huo haijakamilika wala hawajaiwasilisha. Naibu Gavana wa BoT, Juma Reli alidai mahakamani pia kuwa hatambui hasara iliyotokea katika benki hiyo kutokana na mradi huo.

No comments: