Tuesday, March 2, 2010

HALI YA WANAWAKE BADO NI NGUMU - DK. MIGIRO


Ikiwa ni miaka kumi na tano sasa tangu kupitishwa kwa Tamko la Beijing kuhusu Hali ya Wanawake, imeleezwa kuwa pengo la usawa wa kijinsia kati ya mwanamke na mwanaume bado ni kubwa. Na kwamba hali hiyo ipo katika nchi zilizoendelea na zinazoendelea.

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dkt. Asha-Rose Migiro ameyasema hayo wakati alipokuwa akifungua mkutano wa 54 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu Hali ya Wanawake.

Ajenda kuu ya mkutano huo kwa mwaka huu, pamoja na mambo mengine, ni kufanya tathimini ya Tamko la mkutano wa nne wa Beijing na mpango wake wa utekelezaji. Mkutano uliofanyika mwaka 1995 rais wake walikuwa alikuwa Mhe, Getrude Mongela ambaye hivi sasa ni mbunge wa jimbo la Ukerewe ni mmoja ya washiriki wa mkutano huu.

Mkutano huo wa wiki mbili umeanza siku ya jumatatu na unafanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, na kuhudhuriwa na wanawake akiwamo makamu wa rais wa Ghambia ambaye ni mwanamke, mawaziri, wabunge, makatibu wakuu na makundi kutoka asasi zisizo za kiserikali.

Akitoa mfano, Migiro anaeleza kuwa bado idadi kubwa ya maskini ni wanawake kuliko wanaume, wasioujua kusoma au kuandika wengi ni wanawake kuliko wanaume, hata wanaofanya kazi katika mazingira magumu, kwa ujira mdogo na bila kinga au bima yoyote ni wanawake zaidi kuliko wanaume.

Kama hiyo haitoshi, Naibu Katibu Mkuu anabainisha kuwa hata mtizamo kuhusu masuala ya wanawake bado ni hasi ingawa kuna mwamko kidogo, na kwamba utekelezaji wa mambo mengi bado unamtizamo wa kibaguzi. Huku kukiwa na utofauti kati ya upitishwaji wa sheria na utekelezaji wa sheria hizo.

Anasema Migiro. “ Bado wanawake wengi ni maskini, wanaofanya kazi ngumu au za majumbani ni wanawake na watoto wakike , robo tatu ya wanawake hawajui kusoma wala kuandika na hali hii haijabalikia kwa zaidi ya miaka 20 sasa“.

Kuhusu nafasi ya uwakilishi katika vyombo vya kutunga na kupitisha sheria, Migiro anasema kasi yake si ya Kuridisha kwani hadi mwaka 2009 ni nchi 25 tu ambazo zimeweza kufikisha lengo la kuwa na asilimia 30 ya wabunge wanawake.

Kwa upande wa huduma za afya ya uzazi, Naibu Katibu Mkuu, anaeleza kwamba, bado ni eneo ambalo halijawa na nafuu yoyote, idadi ya vifo vitokanavyo na uzazi bado ni kubwa. vifo ambavyo siyo tu havipashwi kutokea lakini pia vinaweza kuzuilika.

“ Kwa hiyo, wakati tunaona kuwa kuna dalili zuri za mafanikio mbalimbali kuhusu hali ya wanawake miaka 15 baada ya tamko la Beijing, ukweli ni kwamba bado hakuna mabadiliko ya kuridhisha na kujivunia.

Pamoja na mapungufu hayo, Naibu Katibu Mkuu ametumia fursha hiyo kuwapongeza na kuwashukuru wanawake, katika nafasi zao mbalimali kwa kazi kubwa wanaoifanya ya ubinifu wa kuzishinikisha na kuziwajibisha serikali zao zitekeleze sera, sheria na mipango inayolenga kuleta usawa na uwezeshwaji wa wanawake.

Akasema jitihada zao hizo zimeweza kulete mwamko na uelewa miongoni mwa viongozi wanawake kwa wanaume ya kuwa suala la usawa wa kijinsia na uwezeshwaji wa mwanamke na mtoto wa kike si jambo la kupita na badala yake ni moja ya nguzo muhimu katika upatikanaji wa maendeleo endelevu, ukuaji wa uchumi, amani na usalama.

Akasema yeye na Katibu Mkuu Ban Ki Moon wamedhamiria kuhakikisha kwamba Umoja wa Mataifa unaweka mazingira bora yatakayoziwezesha serikali na asasi za kijamii kuhakikisha kuwa masuala ya usawa wa jinsia na uwezeshaji wa wanawake yanaingizwa katika Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs).

1 comment:

Anonymous said...

Nadhani Mama Migiro ndiye anayepaswa kufanya hali ya akina mama iwe nyepesi, yupo kwenye chombo kikubwa na chenye nguvu duniani na ana nafasi kubwa sana ya kuweza kusababisha mabadiliko maana mfumo dume umekithiri zaidi huko huko kwenye mashirika ya umoja wa mataifa(UN). Hili hauwezi kulikwepa mheshimiwa kazi ni yako pia uwakomboe wanawake wenzako kimapinduzi.