Monday, March 8, 2010

Wanawake walilia faragha na waume zao

WANAWAKE wanaoishi katika makambi ya waathirika wa mafuriko Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, wamesema wanahofu kubwa juu ya kuvunjika kwa ndoa zao kutokana na kutengwa na waume zao kwa muda mrefu kufuatia adha ya mafuriko iliyowakumba mwishoni mwa mwaka jana na mwanzoni mwa mwaka huu.

Wakiongea na HabariLeo jana, katika kambi ya Mazulia (mojawapo ya kambi zinazowahifadhi), waathirika hao walisema hofu hiyo imekuja baada ya kutengana na wazazi wenzao tangu mwezi Januari mwaka huu hadi sasa.

Walisema makazi yao ya sasa hayaruhusu faragha inayostahili. Wanawake hao walisema wanaishi familia nne katika hema moja hivyo kuwalazimu kuishi wanawake pamoja na watoto wao wa kike peke yao , huku waume zao wakiishi katika mahema mengine na watoto wa kiume.

Wamesema hali hiyo imekuwa ikiwaathiri sana kisaikolojia kutokana na mazoea ya hapo awali ya kuishi na wazazi wenzao pamoja, na kueleza kuwa hali hiyo imekuwa ikiwakosesha raha kutokana na kuingiwa na hofu ya kuhatarisha ndoa zao.

“ Tangu tumehamia kwenye haya mahema tumekuwa na mawazo sana juu ya hizi ndoa zetu…tutaishi hivi hadi lini, maisha haya kwa kweli ni magumu sana , japokuwa serikali inajitahidi kutupatia chakula, lakini ndoa zetu zipo matatani” walisema.

Walisema licha ya kuhofia kuporomoka kwa ndoa hizo, pia wamekuwa na hofu kubwa ya kupata magonjwa ya zinaa ikiwa ni pamoja na kupata maambukizo mapya ya virusi vya Ukimwi kutokana na wanaume hao kupata nafasi ya kutoka nje ya ndoa zao kutokana na visingizio vya kuishi tofauti na wake zao.

“Kama unavyojua hawa wakina baba kipindi hiki kwao wanaona ni neema, kwa kuwa wana uhuru wa kuzurura na kurudi kwenye mahema muda wanaotaka kwa kuwa hatupo nao, wanafanya maamuzi yao, jambo ambalo ni hatari sana linaweza huko baadaye likatuletea magonjwa ya zinaa hata maambukizi ya Ukimwi” walisema kwa masikitiko.


Wanawake hao walisema kutokana na adha hiyo ya mafuriko hivi sasa gharama za nyumba za kupanga zimepanda mara mbili, na kueleza kuwa chumba cha bei ya shilingi elfu tano hivi sasa ni shilingi elfu kumi, huku bado kukiwa na uhaba mkubwa wa nyumba za kupanga.

Waliongeza kuwa kutokana na kupanda gharama za nyumba hizo, ili hali wakiwa na kipato kidogo wanalazimika kuendelea kuishi kwenye mahema hayo ili kuweza kupunguza gharama zaidi za maisha.

Wakizungumzia juu ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo ilianza tangu Machi mosi, walisema hawawezi kuifurahia siku hiyo kutokana na matatizo yanayowakabili hususani katika kipindi hiki kigumu ambacho wamelazimika kutengana na wazazi wenzao kufuatia adha hiyo ya mafuriko.

Aidha kwa upande wake Mwenyekiti wa Kambi hiyo Said Madogoya alisema imelazimu familia hizo kuishi kwa mtindo huo kutokana na uhaba mkubwa wa mahema unaowakabili, na kueleza kuwa mahema hayo yasingetosha kuhifadhi familia moja katika kila hema kutokana na uchache huo.

Kambi hiyo ya Mazulia ina idadi ya mahema 744 yaliyojengwa, ikiwa ni sambamba na vyumba 57 vilivyogawanywa ndani ya kiwanda cha Mazulia.

Huku wanawake wengine duniani leo wakiadhimisha sikukuu yao, wanawake wa Wilaya ya Kilosa wataingia wakiwa na dhiki kubwa za kifamilia.

No comments: