Monday, March 22, 2010

Malaigwanani wamtetea Lowassa

MBUNGE wa Monduli Edward Lowassa ametetewa na wazee wa jamii ya Wamasai (Laigwanani) kuwa bado ni kiongozi wao kwani tararibu zote za kumchagua zilifuatwa ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha Malaigwanani wa ndani na nje ya nchi.

Kauli hiyo ilisemwa na Malaigwanani kutoka katika wilaya za Mkoa wa Arusha waliofanya kikao katika kitongoji cha Nanja wilayani Monduli mkoani Arusha kutafakari hali halisi ya mwenendo wa baadhi ya Malaigwanani kutumiwa na wanasiasa kupotosha ukweli.

Akizungumza mara baada ya kikao hicho Katibu wa Malaigwanani Sigit Ole Kibiriti alisema kitendo cha baadhi ya Malaigwanani kuhoji uteuzi wa Lowassa aliyeteuliwa kuwa Alaigwanani ni ukiukwaji mkubwa wa taratibu.

Ole Kibiriti alisema mchakato wa kumteua Lowassa kuwa Alaigwanani ulizingatia sifa zote za mila ya jamii ya Kimasai ikiwemo upendo, huruma, unyenyekevu na mwenye kujali jamii. Sifa nyingine ni pamoja na kukubalika katika jamii kuwa Lagwanani wao na kutotiliwa shaka, uwe mtu unayeweza kukabiliana na majukumu mbalimbali ndani ya jamii na awe na uwezo wa kuwaunganisha watu unaowaongoza na pia uwe na maono ya mbali vitu ambavyo Lowassa anavyo.

''Sisi Malaigwanani wa Maa tunasikitishwa na hali hiyo na kuhoji kama kweli waliotamka ni viongozi wa Maa ama ni vibaraka? Na kama ni viongozi wa Maa kweli basi wanatumiwa na wanasiasa kuchafua mila za Kimasai pasipo kujua,'' alisema Ole Kibiriti.

Mbali ya hilo katika jamii ya Maa Kisongo ndio wenye mamlaka yote ya kimila na ndio makao makuu ya mila na desturi ya Maasai na ndio wenye mamlaka ya kumteua Oloiboni, Alaunoni, Oloboruengeene na viongozi wengine wa kimila.

Ole Kibiriti aliwataka malaigwanani kuacha kutumiwa kuchafua na kuvuruga utaratibu wa kimila na inasikitisha kusikia maneno ya kuvuruga taratibu za kimila kwa kutumiwa na wanasiasa.

Malaigwanani waliohudhuria kikao hicho cha siku moja ni kutoka katika wilaya za Monduli, Arumeru, Simanjiro na Longido .

No comments: