Monday, July 14, 2014

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Kutembelea Asasi Zinazotoa Msaada wa Kisheria



Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Kutembelea Asasi Zinazotoa Msaada wa Kisheria jijini Dar Es Salaam
--------------------------------------
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Angellah Jasmine Kairuki (MB) anatarajia kufanya ziara ya kikazi ya siku tano kuanzia Jumatatu, Julai 14  hadi Ijumaa 18, 2014 katika jiji la Dar Es Salaam akitembelea asasi mbalimbali zinazotoa huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi kwa lengo la kujionea huduma zinazotolewa na asasi hizi ikiwa ni pamoja na kukutana na wananchi wanaopata huduma hii. 

Pamoja na kujionea huduma hizi Mh. Naibu Waziri anatarajiwa kujionea ufanisi wa kazi zinazofanywa na asasi hizi, changamoto zinazowakabili pamoja na kupokea maoni, ushauri na kubadilishana mawazo ili kujua jinsi ambavyo serikali inaweza kuboresha utoaji wa huduma hii.

Katika ziara hiyo, Mhe. Kairuki anatarajia kutembelea jumla ya asasi 13 ikiwa ni pamoja na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Taasisi ya Haki za Binadamu na Mazingira (Envirocare), Kamati ya Msaada wa Kisheria ya Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam na Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Nyingine ni pamoja na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Kituo cha Msaada wa Kisheria kwa Wanawake (WLAC) na Kituo Kinachoshughulikia Maslahi ya Wanawake na Watoto (TWCWC).

Taasisi nyingine atazozitembelea ni Kituo cha Msaada wa Kisheria kwa Wajane na Watoto  (CWCA), Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA), Kituo cha Msaada wa Kisheria cha Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Nyumba ya Amani na Ofisi ya Mfuko wa Huduma za Kisheria (Legal Services Facility).

Mheshimiwa Kairuki anatarajia kumaliza ziara yake siku ya Ijumaa, Julai 18, 2014 kwa kutembelea Sekretariati ya Msaada wa Kisheria Tanzania ijnayoratibu shughuli za utaoji wa Msaada wa Kisheria Tanzania na kisha kufanya mkutano wa majumuisho na waandishi wa habari katika ukumbi wa mikutano wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria kuanzia saa 5:00 asubuhi.

No comments: