Tuesday, August 2, 2011

MKUU WA SHULE NA MAKAMU WAKE WAPOKEZANA KUFUNDISHA SHULE NZIMA YA MSINGI MCHUCHUMA LUDEWA

Mwalimu mkuu msaidizi wa shule ya Msingi Mchuchuma wilaya ya Ludewa mkoani Iringa Bw.Joseph Thomas Lugome (58) akionyesha darasa la saba ambalo limekuwa likisomewa pia na wanafunzi wa darasa la sita kwa kupokezana na darasa la saba kutokana na shule hiyo yenye wanafunzi zaidi ya 200 kuwa na walimu wawili pekee

SHULE ya msingi Mchuchuma katika wilaya ya Ludewa mkoani Iringa yenye wanafunzi 208 wakiwemo wanafunzi wasichana 90 na wavulana 118 imekuwa ikifundishwa na mkuu wa shule na makamu mkuu wa shule pekee ambao wote ni wanaume .

Uchunguzi uliofanywa na timu ya waandishi wa habari za mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP ) mkoani Iringa umebaini kuwepo kwa hali hiyo ambayo pia imekuwa ikiwapa wakati mgumu walimu hao hasa pindi wanafunzi wa kike wanapougua na kuhitaji msaada wa kupelekwa katika matibabu .

Hata hivyo kutokana na upungufu mkubwa wa walimu katika shule hiyo ambayo inaelezwa kujengwa juu ya madini ya mchuchuma na linganga ,umekuwa ukikwamisha kwa kiasi kikubwa ufaulu wa wanafunzi katika shule hiyo na kupelekea baadhi ya watoto kuacha shule kwa kutokana na kukosa walimu wa kuwafundisha .

Mmoja kati ya wazazi wa wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo Augustino Haule alisema kuwa kwa upande wake alikuwa na watoto wawili waliokuwa wakisoma katika shule hiyo ila mmoja wa kike ambaye alikuwa darasa la saba amelazimika kumwachisha shule baada ya muda mwingi kushida mitaani baada ya walimu kutofundisha mara kwa mara.

Haule alisema kuwa mbali ya walimu kuwa wachache katika shule hiyo ila bado mazingira ya shule hiyo yamekuwa yakichangia watoto kuacha shule kutokana na muda mwingi kufanya kazi za kupika na kuchota maji ya walimu umbali wa zaidi ya kilomita 2 kutoka katika shule hiyo.

Pia alisema kuwa ni vema serikali kuifunga kabisa shule hiyo hadi pale itakapolipatia ufumbuzi tatizo la upungufu wa walimu kuliko serikali kuendelea kuwaacha wanafunzi zaidi ya 200 kufundishwa na walimu wawili pekee tena wote wakiwa ni wanaume.

Mwalimu mkuu mssaidizi wa shule hiyo Joseph Lugome alithibitisha uhaba huo wa walimu katika shule hiyo na kuwa hadi sasa kwa zaidi ya wiki mbili mwalimu amebaki peke yake baada ya mwenzake kupata matatizo ya kiafya.

Alisema kuwa katika shule hiyo wanafunzi 47 ni darasa la saba ambao wanangoja kufanya mtihani wa Taifa wa kuhitimu elimu ya msingi na kati ya wanafunzi hao wasichana ni 24 na wavulana ni 25 huku wanafunzi wa darasa la nne katika shule hiyo ni 10 pekee wasichana wakiwa 11 na wavulana 8.

Hata hivyo alisema kuwa kutokana na shule hiyo kutokuwa na maji wanafunzi wamekuwa wakipagiwa zamu ya kuchota maji ya walimu umbali wa kilomita zaidi ya 2 kutoka katika shule hiyo ili kutoka nafasi ya walimu kufundisha wanafunzi wengine .

Kwani alisema kuwa iwapo walimu wataondoka na kwenda kutafuta maji basi upo uwezekano wa wanafunzi kuendelea kukosa vipindi .

Lugome alisema kuwa wakati mwingine shule hiyo imekuwa ikifungwa kwa muda iwapo wanafunzi zaidi ya mmoja wataugua na walimu hao kufanya kazi ya kuwabeba mgongoni wanafunzi hao wagonjwa na kuwapeleka zahanati iliyopo kijiji cha jirani kilichopo umbali wa zaidi ya kilometa zaidi ya 12 kijiji cha Nkomang'ombe.

Pamoja na mazingira hayo ya kufundisha yakiwa magumu bado mwaka jana shule hiyo darasa la saba ambalo lilikuwa na wanafunzi 36 wanafunzi 8 walifaulu kujiunga na elimu ya sekondari.

Aidha alisema kuwa mbinu za ufundishaji ambazo zimekuwa zikitumiwa katika shule hiyo yenye walimu wawili ni pamoja na kuunganisha madarasa kwa kufanya darasa la kwanza na la pili ndani ya chumba kimoja na darasa la tatu na la nne kuwa ndani ya darasa moja na darasa la sita wamekuwa wakisoma kwa kupokezana na wale wa darasa la saba.

Mwalimu Lugome alisema kuwa tatizo la utoro kwa wanafunzi limekuwa ni sugu kwa kipindi cha masika zaidi kutokana na wanafunzi kutoka mbali na shule hiyo umbali wa zaidi ya kilomita 2 na kuwa kutokana na mvua na mito kujaa maji wa wanafunzi ambao wamekuwa wakifika shule ni 100 ama 90 pekee na sehemu kubwa hushindwa kufika shule.

Afisa elimu wa wilaya ya Ludewa Robart Hyella amethibitisha kuwepo kwa tatizo la uhaba wa walimu katika shule za msingi ndani ya wilaya hiyo na kuwa shule zinazoongoza kwa upungufu wa walimu ni zile za pembezoni mwa wilaya hiyo .

No comments: