Wednesday, June 9, 2010

Ufisadi wa kutisha ushuru wa forodha

-Vigogo wawakingia kifua mawakala wa ukwepaji kodi
-Ni wafanyabiashara watatu wa Kihindi
-Wajificha katika kuchangia kampeni za CCM 2010


WAKATI bajeti ya Serikali inasuasua kutokana na uhaba wa fedha za ndani, familia moja ya Dar es Salaam inayomiliki kampuni inayojihusisha na biashara ya bidhaa za nyumbani imejiingiza katika uwakala wa forodha kwa staili ya aina yake ikiwa ni pamoja na kujikita katika kuwasaidia wafanyabiashara wengine kukwepa kodi; huku wahusika wakijiwekea kinga kwa wanasiasa, Raia Mwema imeelezwa.

Biashara hiyo ya aina yake ya uwakala wa ukwepaji kodi, imeelezwa kuipotezea serikali mabilioni ya shilingi ambazo zilistahili kukusanywa kutoka kwa wafanyabiashara mbalimbali wanaoingiza bidhaa mbalimbali kutoka China na Dubai; huku baadhi ya wanasiasa wenye nguvu serikalini na familia zao wakiwa nyuma ya uhalifu huo.

Vyanzo vya habari ndani ya serikali vimelieleza Raia Mwema kwamba familia hiyo yenye vijana watatu wenye asili ya kiasia ilirithi biashara ya wazazi wao ya kuuza plastic carpets (mazulia ya plastiki), door mats (mikeka ya milangoni), taulo, mapazia na mashuka na baadaye kuamua kuingia katika “uwakala wa ukwepaji kodi”.

Habari za ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) zimeeleza kwamba mamlaka hiyo imekuwa ikifuatilia kwa makini suala hilo pamoja na kuwapo taarifa za uhakika kwamba maofisa waandamizi wa mamlaka hiyo wamekuwa wakishirikiana na wafanyabiashara hao kukwepa kodi.

Mbali ya kuwahusisha watumishi wazito ndani ya TRA, vijana hao wameelezwa kuingizwa katika orodha ya “wachangiaji wakubwa” wa Chama cha Mapinduzi (CCM) pamoja na kuwa karibu na wanasiasa binafsi ndani ya chama hicho tawala.

Kamishna Mkuu wa TRA, Harry Kitilya, hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo kwa maelezo kwamba hayuko katika nafasi ya kufahamu kila kitu kinachoendelea ndani ya mamlaka hiyo kwa nafasi yake kwa kuwa kila eneo linaongozwa na kamishna wake na “kwa suala hilo anayepaswa kuzungungumzia ni Kamishna wa Forodha.”

Pamoja na kuelezwa kwamba TRA wanazo taarifa za ukwepaji kodi huo na kwamba wamekwisha kuanza uchunguzi, Kitilya alisema: “hilo suala liko chini ya Kamishna wa Forodha na mwenzake Kamishna wa Uchunguzi ambao ndio wanapaswa kulitolea ufafanuzi.”

Raia Mwema ilipomweleza Kitilya kwamba habari za kampuni hiyo kukwepa kodi zimeshawahi kumfikia na ofisi yake kuzitolea maelekezo, alisema, “Ndio kwanza leo unanieleza kuhusu kampuni hiyo, mimi sina taarifa kabisa labda uwatafute Kamishna wa Forodha na wa uchunguzi.”

Hata hivyo, maofisa wa ndani ya TRA wamelieleza Raia Mwema kwamba wafanyabiashara hao vijana wakiongozwa na kaka yao (jina tunalihifadhi kwa sasa), walikuwa wakiagiza bidhaa hizo kutoka nje kupitia bandari ya Tanga kati ya mwaka 2000 hadi 2004 mahali ambako walianza kuwa “mawakala wa ukwepaji kodi”.

“Kutokana na kuzoeleka kwao kwa maofisa wa forodha katika bandari ya Tanga wakati huo, walianza pia kupokea nyaraka za waingizaji wengine wa mizigo tofauti, na kuwasaidia kuivusha kwenye ofisi za Forodha kwa njia za ujanja ujanja.

“Wakati huo hawakuwa na kampuni ya uwakala, walitumia kampuni mbalimbali za kukodi na kutokana na kukua kwa biashara yao na ‘uwakala wao pori’, walijizatiti wakaanzisha mtandao wa kazi kwa kunyoosha au kusafisha njia tangu mizigo inapotoka Tanga hadi kwa wateja Dar es Salaam,” anasema mtoa habari wetu ambaye anafahamu kwa kina mitandao ya ukwepaji kodi.

Imeelezwa kwamba katika ‘kusafisha njia’ walitumia fedha kujitambulisha kwa maofisa forodha na polisi waliokuwa barabarani kudhibiti magendo kwenye vituo muhimu vya udhibiti kama Segera na Kabuku mkoani Tanga; Chalinze na Kibaha mkoani Pwani na kuendelea hadi wakaguzi wengine ndani ya jiji la Dar es Salaam.

“Lakini mwaka 2004 hali ya hewa ya bandari ya Tanga ilibadilika kwa Idara ya Forodha kuziba mianya ya rushwa lakini kwa kuwa vijana hawa walikwisha kuzoea kudanganya katika ulipaji ushuru, ilibidi wahamishie shughuli zao kwingine. Wakaelekeza nguvu zao zote Holili, Kilimanjaro, wakifanya yaleyale waliyokuwa wakiyafanya bandarini Tanga,” anasema mtoa habari wetu.

Sooma zaidi

No comments: