Friday, October 24, 2008

Mrejesho wa Semina za kila Jumatano (GDSS): Ushawishi na Utetezi

Idadi ya washiriki ilikuwa 128 kati yao wanawake walikuwa 72 na wanaume 56 kutoka sehemu tofauti kama vile Asasi za kiraia, vikundi vya kujitolea kupambana na maambukizi ya Ukimwi na VVU, wanafunzi kutoka taasisi za elimu ya juu, waandishi wa habari, FemAct, taasisi za walemavu, makundi maalumu na jamii kwa ujumla.

Kwa kuongozwa na mtoa mada (Anna Sangai), washiriki walijadili maana, mikakati / nyenzo, aina, madhumuni na taratibu katika ushawishi na utetezi ili kushawishi watunga sera na watekelezaji kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii iliyokandamizwa kwa kubadilisha sheria na kanuni.

Mada kuu mbili (mikakati na nyezo) zilijadiliwa kwa kina na kuwekwa bayana kutokana na umuhimu wake katika ushawishi na utetezi

Kuhusu mikakati, mtoa mada alikubaliana wazi kuwa lazima kuwepo dira ili kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii. Ili kukabiliana na changamoto kutoka kwa watunga sera na watekelezaji, yafuatayo lazima yazingatiwe: - Ufahamu / Elimu ya sheria, sera na mipango lazima vizingatiwe ili kufikia na kutekeleza mchakato mzima wa ushawishi na utetezi.

Kuhusu nyenzo, mtoa mada aliainisha njia tofauti kama vile mawasilianao ya nje na ndani kwa wadau wenyewe, elimu kwa makundi yanayostahili, jamii kuwa na ufahamu wa elimu, sanaa na michezo bila kusahau vyombo vya habari.

Mtoa mada aliendelea kuhafiki kwamba njia zote zilizotajwa na nyingine nyingi zinaweza kutumika kusaidia kupinga aina yoyote ya ukandamizaji.

Washiriki walipewa nafasi ya kujadili katika makundi, zikachaguliwa mada tano (5) ili kutathmini kiwango cha uelewa wa suala la ushawishi na utetezi. Mada zilizochaguliwa ni:- Ukimwi na VVU, Afya ya uzazi, Maji, Elimu na Unyanyasaji wa kijinsia.

Mwezeshaji na makundi yote kwa pamoja yalihitimisha kwa kupendekeza kuchagua ujumbe mbalimbali na kuwasilisha kwa mwezeshaji kwa kuupitia na kisha kupeleka kwenye vyombo vya habari kama njia mojawapo ya ushawishi na utetezi ili kuleta mabadiliko ya kweli.

2 comments:

Anonymous said...

mafunzo haya ya ushawishi na utetezi yafanyike kila mara kwa sababu itasaidia wanaharakati kuweza kuchukua hatua katika maeneo yao wanayotokea pindi wanapoona uvunjifu wa haki za binadamu.

Anonymous said...

Ipo haja ya elimu hii kupelekwa na vijijini ili kuwasaidia wapigania haki za kijamii walioko huko ambao ndio wengi sana kulinganisha na hapa na mjini. hongera waaandaaji wa shughuli hii, ni kazi nzuri.