Wednesday, April 25, 2012

Spika: Mawaziri msiwachukie wabunge

SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Anne Makinda, amewapoza mawaziri kutokana na mashambulizi yaliyowakabili katika mkutano wa Bunge ulioahirishwa juzi akiwataka wasijenge chuki na uhasama dhidi ya wakosoaji.

Aidha, uelewa mdogo wa kanuni umeendelea kulisumbua Bunge, hali ambayo Makinda juzi katika kuahirisha mkutano wa saba wa Bunge, aliwataka wabunge kusoma na kukariri kanuni hizo.

Akizungumzia nafasi ya wabunge na namna walivyoshambulia mawaziri kadhaa, Makinda alisema yaliyosemwa ni kwa nia njema na hayapaswi kuwa kiini cha chuki na uhasama.

Aliwataka mawaziri kutambua, kwamba wana dhamana na lengo la wabunge ni kuhakikisha viongozi hao wanafanya vizuri katika utendaji wao. Alisema wachangiaji wengi wanapotoa hoja zikiwamo za shutuma, dukuduku lao huishia bungeni.

“Yaliyojadiliwa yote ni kwa nia njema. Isiwe kiini cha chuki na uhasama. Msibebe chuki ndani ya roho zenu. Msichukue hasira mpaka mkapasuka mifupa. Mnaambiwa namna ya kufanya kazi vizuri. Mkichukulia kwamba ni uadui, mtapata shida,” alisema Makinda na kusisitiza juu ya dhana nzima ya cheo ni dhamana kwa kuongeza: “Kama husemwi wamseme nani na wewe ni Waziri?”

Akizungumzia umuhimu wa wabunge kuelewa kanuni, Makinda alitoa mfano kwamba wapo wabunge waliompelekea barua wakitaka iundwe Kamati Teule licha ya kwamba kanuni ziko wazi juu ya suala hilo.

Alisema Kiti cha Spika lazima kibebe lawama kutokana na wakati mwingine kulazimika kutolea uamuzi wa masuala ambayo baadhi hawaridhiki nayo, ikiwa ni pamoja na kulazimika kuchagua watu wachache wa kuchangia hoja kutokana na idadi kubwa ya wabunge wanaojitokeza.

Wakati huo huo, alivitaka vyombo vya habari kufanya utafiti kabla ya kuandika masuala mbalimbali akivitaka visishiriki katika ushabiki unaojitokeza ndani ya Bunge, badala yake, vijikite kuchunguza.

Kauli ya Spika kuwaasa wabunge kutochukulia hasira yanayosemwa bungeni, imekuja baada ya kujitokeza msuguano mkali baina ya wabunge na mawaziri kadhaa, ambao walitakiwa kujiuzulu hali iliyosababisha kuwasilisha taarifa ya nia ya kupiga kura ya kutomwamini Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, ni miongoni mwa mawaziri hao ambaye juzi katika kujitetea dhidi ya kuhusishwa na kashfa ya ufisadi katika ugawaji vitalu vya uwindaji, aliishutumu Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, kuwa haikumtendea haki.

Aliilalamikia Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM), kwamba haikumshirikisha wala kumpa nafasi ya kujibu tuhuma ilizozitoa juzi bungeni dhidi yake huku akisema “Mungu yupo”.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Lembeli, alimjibu Maige akimtaka ajibu hoja badala ya kuzungumzia mchakato. Lembeli aliliambia Bunge, kwamba Kamati ilifanya kazi kwa mujibu wa kanuni na yote yaliyo katika taarifa yake, ni ya kweli.

“Nimtoe hofu Maige, kwamba Mungu ni mmoja, yupo kwa ajili ya watu wote na kazi yake ni kusimamia haki... yako mengi ambayo hatukuyasema. Kamati inasimamia wizara tatu. Kati ya hizo, wizara inayoipa shida ni ya Maliasili. Imejaa watendaji walio na jeuri. Na pengine ndiyo maana hata Maige hajapata taarifa ya Kamati yetu,” alisema Lembeli.

Taarifa ya Kamati ilihusu uchunguzi kuhusu utaratibu uliotumika katika kukamata na kusafirisha twiga wawili nchi za nje na utaratibu uliotumika kugawa vitalu vya uwindaji wa kitallii kwa msimu wa 2013-2018.

Naye Halima Mlacha anaripoti kuwa Chama cha Wananchi (CUF) kimesema kiko kwenye mchakato wa kuzungumza na vyama vingine vya upinzani vya siasa, ili kufanya maandamano makubwa nchi nzima kumshinikiza Rais Jakaya Kikwete awachukulie hatua mawaziri waliotuhumiwa kuhusika na ubadhirifu bungeni.

Pia chama hicho kimemshauri Waziri Mkuu Mizengo Pinda ajiuzulu kutokana na kutopatiwa nyenzo za kushughulikia sakata hilo na Rais Kikwete.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Profesa Lipumba, alisema amekuwa akipokea ujumbe mfupi kutoka kwa wanachama mbalimbali wa chama hicho wakitaka yafanyike maandamano kushinikiza hatua zichukuliwe dhidi ya mawaziri hao.

“Kwanza napenda kumpongeza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa kufanikisha kutoa ripoti iliyofichua ubadhirifu na wizi wa fedha za umma lakini pia nimesikitishwa na kushindwa kuchukuliwa hatua dhidi ya mawaziri waliotuhumiwa,” alisema Lipumba.

Alisema kwa sasa kinachohitajika ni kwa Serikali kuwajibika katika masuala yanayoibuliwa ya ubadhirifu wa fedha za umma. “Hili sakata la juzi bungeni limeonyesha wazi kuwa mawaziri wanahitaji kuwajibika lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.”

Alisema kuwajibika kwa mawaziri hao kuko mikononi mwa Rais Kikwete ambaye hata hivyo alishindwa kumpatia nyezo Waziri Mkuu za kuwawawajibisha wale wote waliotuhumiwa bungeni kuhusika na ubadhirifu na wizi wa fedha za Serikali.

“Ndio maana tunamshauri Pinda ajiuzulu yeye kwa kuwa yeye ndio msimamizi mkuu wa mawaziri wengine wanapoharibu anapaswa kuwachukulia hatua lakini hana nyenzo za kufanya hivyo,” alisisitiza.

Mawaziri hao ni Waziri wa Fedha Mustafa Mkulo, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hadji Mponda, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Cyril Chami na Naibu wake, Lazaro Nyalandu.

Mawaziri wengine wanaohusishwa na ubadhirifu huo ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika Dk. Jumanne Maghembe, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, Waziri wa Nchi Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Mkuchika na Waziri wa Maliasili na Utalii Ezekiel Maige.

No comments: