Tuesday, December 4, 2012

TGNP: Madawati ya Kutetea Jinsia Yasimamiwe

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), umetoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa madawati yaliyowekwa katika vituo mbalimbali vya polisi nchini, ambayo yanatetea haki za jinsia yanasimamiwa kikamilifu ili kupunguza unyonyaji na unyanyasaji nchini.

Wito huo ulitolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Usu Mallya, jijini Dar es Salaam katika mjadala wa kupinga ukatili wa kijinsia, kauli mbiu ya mtandao huo ni ‘Tokomeza Ukatili wa Kijinsia, Jitokeze kutoa maoni ya Katiba Mpya’.

“Madawati haya yawe ni ya kusaidia na kukomesha ukatili wa kijinsia, hivyo ni jukumu la serikali kuhakikisha kwamba kesi zote ambazo zinafunguliwa zinasimamiwa kikamilifu,” allisema Mallya.

  Usu alisema Mikoa ya Singida na Mara inaongoza kwa kiasi kikubwa kwa ukatili wa kijinsia hususani katika suala la ukeketaji na sababu nyingine ambayo inachangia ni ukosefu wa mgawanyo sawa wa matumizi ya rasilimali za taifa.

Alisema ukatili wa kijinsia una sura tofauti na kwamba hali hiyo inaongezeka kila uchao kutokana na kutokuwepo kwa sera makini za kiuchumi zinazowalinda wanawake katika kumiliki mali.

No comments: