Monday, August 25, 2014

TGNP WASHIRIKIANA NA WAJIKI KUPIGA VITA UKATILI WA KIJINSIA MWANANYAMALA



TGNP WASHIRIKIANA NA WAJIKI KUPIGA VITA UKATILI WA KIJINSIA MWANANYAMALA

JAMII imetakiwa kuunaganisha nguvu kupiga vita vitendo vya Ukatili wa Kijinsia majumbani na katika mazingira ya kazi na kushirikiana na jeshi la polisi ili watuhumiwa wanaofanya ukatili waweze kufikishwea kwenye vyombo vya sheria.


Maandamano yakiwa yamekaribia

Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya siku ya rangi ya chungwa duniani, iliyoadhimishwa na TGNP Mtandao kwa kushirikiana na Taasisi na Wanawake katika Jitihada za Maendeleo (WAJIKI)  katika viwanja vya Minazini  Mwananyamala Kinondoni Jijini Dar es salaam, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi alisema kuwa Jamii ya Tanzania inatakiwa kujiuliza ni kwanini kuna ongezeko kubwa la matukio ya ubakajai, vipigo, udhalilishwaji wa wanawake na wasichana  wakati huu zaidi.
 
Wanawake na wanaume wakiwa pamoja kwenye maandamano
Alisema kuwa wanaharakati wa masuala ya Ukatili wa Kijinsia wanafanya maadhimisho hayo katika ngazi ya Jamii kushiriki kupiga vita aina yoyote ya ukatili wa kijinsia, wakivaa mavazi ya rangi ya chungwa kuonesha kuwa wanapinga kikamilifu bila uoga kila aina ya ukatili wa kijinsia wanaofanyiwa wanawake na wasichana.

“Pamoja na juhudi zinazofanyika za kuwapeleka watoto wa kike shule bado kuna tatizo la udhalilishwaji na ukatili mkubwa wanaofanyiwa,  ubakaji unaenda hadi kwa vitoto vichanga,  tunajiuliza kama watoto waodogo wanaobakwa wanakosa gani?  Hawa wabakaji wanatoka wapi? Kwanini hawaishi pamoja na kwamba kuna wanaokamatwa na kuchukuliwa hatua kali?”alisema Liundi
 
Washiriki wa GDSS wakiwa na Mabango kwenye maandamano yaliyofanyika Mwananyamala kupinga Ukatili wa Kijinsia
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji (TGNP) Lilian Liundi akiwaongoza wananchi katika maandamano ya kupinga ukatili wa kijinsia
Alisema kuwa Mimba za utotoni ni tatizo kubwa ambalo linakwamisha na kufifisha kabisa ndoto ya motto wa kike ya kupata elimu na kufikia ndoto nzuri.

Aliongeza kuwa Utafiti uliofanywa na TGNP Mtandao katika mikoa ya Mbeya, Shinyanga, Morogoro na Dar es salaam, umebaini kwamba kuna tatizo kubwa la kimfumo ambalo limesbabisha maelfu ya wasichana kukosa masomo kutokana na ukatili wa kijinsia.

Liundi alisema kuwa hatuwezi kuondoakana na umasikini wakati idadi kubwa ya wasichana hawaendi shule au wamekatishwa masomo kwasababu taifa linatakiwa kuwa na watu waliosoma na wanaoweza kupambana na changamoto za kiuchumi wakiwa na uelewa wa kuchambua na kupambanua masuala yanayowazunguka. Lazima kupambana na biashara haramu ya watoto wa kike ili kuwapa fursa ya kusoma na kujenga uchumi pale walipo wakifanya kazi zenye staha.

 Kwa upande wake Mwenyekiti wa WAJIKI, Janeth Mawinza alisema kuwa  hakuna mtu mmoja mmoja au kikundi au taasisi moja inayoweza kupambana na kumaliza kabisa tatizo la Ukatili wa Kijinsia bila kuunganisha nguvu.
Alisema kuwa  WAJIKI chini ya Kituo cha Taarifa na Maarifa Mwananyamala wamafanikiwa kupambana na kesi nyingi za Ukatili wa Kijinsia na hadi kuzifikisha mhakamani kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kati ya wananchi, viongozi wa serikali ya mtaa, kata, Jeshi la Polisi Kinondoni na Idara ya Ustawi wa Jamii Manispaa ya Kinondoni.
“Ukatili mkubwa unaendelea katika Jamii, yetu, matukio tuliyoyaibua ni machache, tunahitaji ushirkiano wa kutosha kutoka kwa Jamii ili kukomesha kabisa matukio haya na jeshi la polisi liendelee kutusaidia kuchukua hatua pale tunapowapa taarifa.  Zaidi ya wasichana 100 sasa wameshafanyiwa ukatili katika eneo hili na bado hatujaweza kupata taarifa zote”alisema mawinza

Kwa upande wake Mkuu wa dawati la Jinsia Mkoa wa Polisi Kinondoni, Prisca Komba alisema kuwa  askari polisi atakayejaribu kupuuza kesi ya ukatili wa kijinsia atachukuliwa hatua za kinidhamu na kuwataka mawakili au waendesha mashtaka wa serikali kutumia muda kusoma kwa umakini taarifa za maelezo na vielelezo vilivyoko kwenye majalada ya kesi za ukatili wa Jinsia zilizofunguliwa ili  haki iweze kupatikana mahakamani.
“ Ninawataka askari Polisi wote kuwa makini, na kutokuwasumbua wahanga wa ukatili wa kijinsia, na  waendesha mashtaka au mawakili wa serikali kuchukua muda kuyasoma majalada ya kesi hizi za ukatili ili kutokuhitimisha kesi hizi kiholela na kuwapa washtakiwa uhalali wa kuwa huru wakati wametenda kosa. Wewe polisi jiulize kama aliyefanyiwa ukatili angekuwa mwanao, mama yako, Binti yako ungefanya nini? “alihoji Komba.

Pamoja na kutoa tena namba zake za simu kwa umma ambazo  ni 0655664979 ili apigiwe kupewa taarifa za ukatili wa kijinsia kwa wasichana na wanawake, aliwataka madaktari wa vituo vya afya na hospitali za umma wanaowafanya wahanga wa Ukatili wa Kijinsia vipimo kukubali kujitokeza mhakamani kutoa uahshaidi pindi wanapohitajika.

Katika juhudi za kutokomeza ukatili wa kijinsia, Julai 2012 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa kupitia kampeni yake ya UNiTE (Tushikamane kutokomeza Ukatili kwa Wanawake) alitunuku kila tarehe 25 ya kila mwezi iwe siku ya Orange (Orange Day au siku ya rangi ya Chungwa). Katika siku hii watu huvaa nguo za rangi ya chungwa na kupinga ukatili dhidi ya Wanawake aidha kwa kuelimisha ama kuhamasisha jamii kuungana katika vita dhidi ya ukatili wa Wanawake. Mada ya mwezi huu ni ‘Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Mtoto wa Kike’


No comments: