Thursday, February 17, 2011

Albino walalamikia urasimu hospitalini

MWENYEKITI wa Chama cha Albino mkoa wa Mwanza, Alfred Kapole ameiomba Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kuweka utaratibu maalumu wa kutoa matibabu kwa watu wenye ulemavu wa ngozi ili kuondokana na usumbufu wanaoupata katika vituo vya afya.

Alisema kuwa kumekuwepo na usumbufu mkubwa ambao albino huupata wanapokwenda katika hospitali mbalimbali mkoani Mwanza kwa ajili ya kupata matibabu .

Miongoni mwa usumbufu ni pamoja na kuamriwa kutoa fedha za kufungulia faili na kulipia gharama za kumwona tabibu.

“Kwa kweli sisi walemavu wa ngozi,tunaiomba Serikali ituangalie katika hili, kwani nasi pia tuliwachagua, pia wakati wa kampeni za uchaguzi walisema kuwa endapo tutawachagua wakaingia madarakani sisi walemavu tutapatiwa matibabu bure.

Lakini ukweli ni kwamba tunapata usumbufu tunapofika katika hospitali kwa ajili ya kutibiwa,"alisema Kapole.

Alisema kuwa utaratibu ambao uliwekwa na Serikali awali kwa ajili ya Albino kupata matibabu, ulikuwa ni kupata barua kutoka kwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa na baadaye
barua hiyo kuidhinishwa na Mkuu wa Wilaya na mhusika kwenda moja kwa moja hadi hospitali husika kwa ajili ya matibabu.

Hata hivyo Mwenyekiti huyo alisema kuwa pamoja na kupata vibali hivyo, wanapofika hospitalini huwa wanapata usumbufu ambao huwakatisha tamaa ya kupatiwa matibabu.

Alisema, “mimi sioni kama kuna haja ya vibali kwa kuwa sisi ulemavu wetu unaonekana wazi, sasa huwa naona ajabu tunapofika hospitali tunaambiwa tuoneshe kibali ambacho kinatutambulisha kuwa ni walemavu jamani huu si ni urasimu kabisa."

No comments: