Monday, March 29, 2010

Yona agombana na Wamarekani


-Yumo Balozi wa zamani wa Marekani Charles Stith
-Ni kuhusu mradi wa nyumba Kunduchi, Dar

FAMILIA ya aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini katika Serikali ya Awamu ya Tatu, Daniel Yona, iko katika mvutano unaomhusisha aliyekuwa Balozi wa Marekani nchini, Mchungaji Charles Stith. Katika mvutano huo, Serikali ya Tanzania imeshtuka dakika za mwisho, ikishangaa na kuahidi kuchukua hatua stahili, Raia Mwema imebaini.

Mvutano huo unahusisha moja kwa moja kundi la wawekezaji wa Marekani waliokuwa tayari kuwekeza mamilioni ya dola nchini katika mradi wa ujenzi wa nyumba nafuu, kwa makubaliano mahsusi na kampuni ya Yona.

Yona, ambaye kwa sasa anashitakiwa katika Mahakama ya Kisutu kwa tuhuma za kutumia vibaya madaraka alipokuwa Waziri, amejikuta katika mvutano baada ya kutaka kujitoa katika makubaliano ya uuzaji wa eneo kwa kampuni ya Kimarekani ya Enterprises Homes Tanzania Ltd (EHTL).

Kampuni ya Yona inayoitwa Devconsult International Ltd iliingia mkataba na Enterprises Homes Tanzania Ltd kuuza ardhi yenye hati namba (Plot No). 384, Block ‘A’ Kunduchi kwa bei ya Dola za Marekani 650,000 (zaidi ya Sh milioni 650).

Lengo la EHTL kwa kushirikisha wadau wengine ni kufanikisha ujenzi wa awali wa nyumba 45 za gharama nafuu, ambazo ni sehemu ya ujenzi wa nyumba nafuu mpya 5,000 utakaokamilika mwaka 2012.

Mradi huo wa aina yake unalenga kusaidia ndoto ya Serikali kuwapatia wananchi makazi bora ya gharama nafuu, lakini habari zinasema kampuni iliyokusudia kununua ardhi hiyo kwa familia ya Yona, ilishindwa kutimiza masharti ya mkataba wa awali ikiwa ni pamoja na kulipa fedha kabla ya kukabidhiwa eneo husika.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopo, mfadhili wa mradi huo kupitia EHTL ni kampuni binafsi ya Marekani, Overseas Private Investment Corporation (OPIC), pamoja na taasisi nyingine za fedha zikiwamo Benki ya Eurafrican Bank na taasisi ya mikopo Ghana.

Kila nyumba ilipangwa kugharimu dola za Marekani 100,000 (zaidi ya Sh milioni 100) au pungufu ya kiwango hicho. Mkataba wa mkopo wa kuuziwa nyumba hiyo kwa mlalahoi wa Tanzania utadumu kwa miaka 15.

Hata hivyo, hivi karibuni Devconsult iliamua kujitoa katika mpango huo na hivyo kuhatarisha malengo yaliyokusudiwa, baada ya kampuni hiyo ya kina Yona kushindwa kuwashawishi wawekezaji hao kulipa fedha husika kwa mujibu wa mkataba.

Lakini pamoja na kitisho hicho, Wawekezaji wa Marekani wenye malengo hayo bado hawajakata tamaa isipokuwa wamekuwa wakifanya kampeni wakidai kwamba ni vigumu kuendesha shughuli za kiuwekezaji nchini Tanzania bila kueleza ukweli kwamba walishindwa kulipa fedha kwa wakati kama walivyokubaliana katika mkataba.

Taarifa kutoka kwa wawekezaji hao zinabainisha kuwa wana matumaini familia ya Yona itarejea katika mpango huo ili hatimaye kuufanikisha, huku kukiwa na taarifa za suala hilo sasa huenda likaingia katika mkondo wa kimahakama.

Habari zaidi zinasema kwamba mbali ya kuwa familia ya Yona kutaka kuuza eneo hilo, mmoja wa wanafamilia naye aliingizwa katika kampuni hiyo ya Wamarekani kama mwana hisa kwa nia ya kufanikisha malengo ya ujenzi wa nyumba hizo huku kukiwa na watu wengine maarufu nyuma yao.

Wakati mvutano huo ukiendelea, takwimu nchini hasa za Benki Kuu zinabainisha kuwa mahitaji ya nyumba bora Tanzania yemefikia nyumba milioni 2.

Dar es Salaam pekee, wastani wa mahitaji ya viwanja kwa ajili ya ujenzi ni 20,000 lakini uwezo wa utoaji kwa mwaka ni 700, na hivyo takriban asilimia 97 ya mahitaji hayatekelezwi.

Soma zaidi

No comments: