Thursday, December 17, 2009

RAIS ANA MAMLAKA KISHERIA

Siku moja baada ya Waziri wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe kusema Rais Jakaya Kikwete hawezi kutumia mamlaka yake kuwabana mafisadi, baadhi ya wanasheria nchini, akiwamo Profesa Issa Shivji, wamepinga kauli hiyo kwa kusema sio kweli.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam wanasheria hao walisema rais anaweza kuwabana mafisadi kwa kutumia mamlaka yake ndani ya chama na serikali.

Profesa Issa Shivji alisema Rais Kikwete anaweza kupambana na watuhumiwa wa ufisadi kwa kuwavua madaraka walionayo katika chama au serikali.

Gwiji hilo la Sheria na Mwenyekiti wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere, alisema kama watuhumiwa watakuwa watumishi wa serikali au watendaji katika mashirika ya umma, rais anaweza kuwawajibisha kwa kutumia sheria na kanuni za utumishi wa umma.

Kumwajibisha mtuhumiwa sio iwe kumpeleka mahakamani, unaweza kuchukua hatua za awali ikiwemo kumvua nyadhifa zote. Kama ni mwanasiasa au mtumishi katika serikali na mashirika ya umma, unaweza kumwajibisha kwa mujibu wa sheria za umma," alisema Profesa Shivji.

Alisisitiza kusema Rais Kikwete hana uwezo wa kuwabana mafisadi sio kweli na watanzania wanatakiwa kuelewa hivyo kwamba rais anaweza.

Kauli ya Profesa Shivji iliungwa mkono na Profesa Abdallah Safari, aliyetia ngumu akisema sheria za nchi ikiwemo ya utawala, inampa uwezo na mamlaka rais kupambana na vitendo vya ufisadi ndani ya serikali yake na hata katika chama chake.

No comments: